Wednesday, 30 September 2015

AMRI YA KUTOUZA NYUMBA YA MKOPO HAIKATIWI RUFAA.

|0 comments

Image result for mahakama

NA  BASHIR  YAKUB - 

Mara  kadhaa  mkopaji  anaposhindwa  kulipa  mkopo  hukimbilia  mahakamani  ili  kuona  kama  anaweza  kupata unafuu  hasa linapokuja  suala  la  wakopeshaji  wake  kutaka  kuuza    nyumba/kiwanja  alichoweka  rehani.  Ni  ukweli  usiopingika  kuwa  hatua  hii  imewasaidia  wengi  hasa  wale  wanaowahi.  Yapo  makala   tuliwahi  kuandika kuhusu  hatua  za kuchukua  hasa  inapotokea  kuwa  nyumba  yako  inataka  kuuzwa.
 Makala  yalieleza  namna na hatua  za  kufuata ili  kuokoa  nyumba.  Kwenda  mahakamani  kuzuia  nyumba  isiuzwe  baada  ya  kushindwa  kurejesha  kiasi  cha  rejesho  sio ukorofi  isipokuwa ni  kutekeleza  lililo  ndani  ya  sheria hasa  pale panapo sababu  za  msingi  za  kufanya  hivyo.  

Mahakama  za  ardhi  za  wilaya  na  mahakama  kuu  hasa  ya  ardhi  ndizo  mahakama  zenye  mamlaka  katika  kutoa  mazuio  haya  kutegemeana   na thamani  ya  nyumba/kiwanja  na kiasi  cha  deni  kilichohusishwa  katika  muamala  huo. Swali  kwetu ni  kama  baada  ya  kuwa  umeenda  mahakamani  na  kubahatika  kupata  zuio la kutouzwa  nyumba  yako, je  upande  wa  wakopeshaji  wanaweza kukata  rufaa  kupinga  amri  hiyo na  kufanikiwa. Majibu  ya  swali  hili ndio  makala  ya  leo.

1.HAKI  YA  RUFAA.

Kifungu  cha  74   cha  sura  ya  33 Sheria  mwenendo  wa  madai kinaeleza  rufaa  katika  amri  mbalimbali  za  mahakama.  Kifungu  kilieleza  wazi  kuwa  kutakuwa  na  rufaa  kutoka  mahakama  za  wilaya  na  zile  za  hakimu  mkazi  ambapo  rufaa  hizo  zitatakiwa  kwenda  mahakama  kuu. Kwa  wasiojua  maana  ya rufaa,  hii  ni hatua  ya  kupeleka  malalamiko  mbele  zaidi  baada  ya  kuwa  hukuridhishwa  na  uamuzi  wa  mahakama   iliyoamua  shauri  lako katika  hatua  za  awali.

Nje  ya hilo  kifungu  cha  78  cha  sheria  hiyohiyo  kiliruhusu  pia  kufanyika kwa  marejeo  iwapo  mtu  hakuridhika  na  maamuzi  ya  amri  ya  mahakama.  Marejeo  ni  hatua  ya  mahakama   kuitisha  faili  tena  na  kupitia  kilekile  ilichoamua  ili  kujiridhisha  na  uhalali  wake.  Hii  hutokea  baada  ya  upande  wa  pili  kuomba  hilo kufanyika.  Kwahiyo  ilikuwa  ikiwezekana  kutolewa  amri  ya  kuzuia  nyumba  kuuzwa  halafu  baadae  faili  likaitishwa  tena  na  kurudiwa  na  kutolewa  amri  nyingine  ambayo  inaweza  kuwa ileile  ya kutouzwa au  ikabadilishwa  ikawa  amri  mpya  ya  kuuza.

2.   SHERIA  YA  UKOPAJI  FEDHA  NA  KUWEKA  REHANI.

Mwaka  2008  ilikuja  sheria  ambayo  iliitwa  kwa  jina  la sheria  ya  ukopaji  fedha  na  kuweka  rehani.  Sheria  hii  inazungumzia  masuala  yote  nyeti  yanayohusu   kukopeshwa  fedha  na  kuweka  rehani  mali . Ni  sheria  inayoratibu  masuala   yahusuyo  kuuzwa  kwa  mali  zilizowekwa  rehani na  kutouzwa  kwake. Inazungumzia  haki  za  mkopaji  na  mkopeshaji  halikadhalika  wajibu  wao  wote  katika  nafasi  zao.  Kutokana na  ujio  wa  sheria  hii  masuala  kadhaa  katika  sheria  ya  ardhi  ya 1999  sambamba  na  sheria  ya  mwenendo  wa  madai sura ya  33  zimelazimika  kufanyiwa  marekebisho  ili  kukidhi  malengo  kadhaa .

3.  AMRI  YA  KUTOUZA  NYUMBA  YA  MKOPO  HAIKATIWI  RUFAA.

Hapo  juu  tuliona  kuwa  awali  ilikuwa  ni  ruhusa kwa  mtu  kukata  rufaa   hata  kwa  amri  iliyotolewa  kuzuia  nyumba/kiwanja    cha   mkopo  kuuzwa.  Mahakama  ya  wilaya  ingeweza  kutoa  amri  kuwa  nyumba  fulani isiuzwe  hata  kama  mkopaji  yuko  nje  ya  makubaliano  kwasababu  kadha  wa  kadha. Hata  hivyo   ilikuwa  ni haki  ya  mkopeshaji ambaye  ndiye  hutaka  kuuza  nyumba  kukata  rufaa  na  kupinga  amri  hiyo. Kama  amri  hiyo  ingetolewa  mahakama  ya  wilaya  au  ya  hakimu mkazi basi  mkopeshaji  angeweza  kukata  rufaa  kwenda  mahakama  kuu.  Na  huko   ingewezekana  kutolewa  uamuzi  uleule  au  uamuzi  mpya  ambapo  pengine  amri  ya  kutouzwa  ingebatilishwa  na  kuruhusu  uuzaji  kuendelea.

Kwa sasa kutokana  na   sheria hii  ya  masuala  ya  ukopeshaji fedha  na rehani  kifungu  hiki  kimefanyiwa  marekebisho  na  sasa  ni  kuwa  amri  ya  mahakama  iwe  ya  wilaya  au  mahakama  kuu  ikishapita  na  kutoa  zuio  la  kutouzwa  nyumba  ya  mkopaji   basi   huwezi  tena  kukata  rufaa  kupinga  jambo  hilo.  Amri  hiyo  ikishatolewa  basi  inakuwa  imetolewa. Ni  kutokana  na  hilo  kichwa  cha  makala  haya kimekuwa ,  amri  ya  kutouza  nyumba  ya  mkopo  haikatiwi  rufaa.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



Tuesday, 29 September 2015

HAKI ZA MKOPAJI KABLA YA KUUZA MALI YAKE - 2

|0 comments



Image result for MNADA  WA NYUMBA
NA  BASHIR  YAKUB - 

Niliwahi  kuandika  kuwa , mkopo  sawa  lakini  haki  za  mkopaji  zilindwe. Nikasisitiza  kuwa  kushindwa  kurejesha  mkopo  wote  au  sehemu  yake  hakuondoi  haki   za  kisheria  alizonazo  mkopaji. Katika  hilo  nilizungumzia  taratibu  mahsusi  za  kisheria  zinazotakiwa  kufuatwa  wakati  taasisi  ya  fedha  inapofikia uamuzi  wa  kuuza  dhamana  ya  mkopaji, nyumba/kiwanja.  Mara  nyingi  ukiukaji  wa  haki  za  mkopaji  hutendwa  na  taasisi  iliyotoa mkopo  au  kampuni  za  udalali (brokers)  ambazo  hupewa  kazi  ya  kunadisha  mali  ya  mkopaji.

Wakati mwingine yawezekana  kabisa  taasisi  ya  fedha  ikawa  imefuata  taratibu  zote za  kisheria  lakini  tatizo  likajitokeza  kwa  dalali (brokers)  aliyepewa  kazi  ya  mnada. Na  hivi  ndivyo  ambavyo  imekuwa  ikijitokeza   na  hiyo  ni  kwasababu  moja  tu,  kuwa  hawa  hupenda  kujipatia  faida  kubwa  na  ya  haraka katika  mali  inayonadishwa. Ni  katika  kufanya  hivyo hujikuta wamekiuka  haki  na  taratibu  za  uuzaji  kwa  ujumla.   Kwa  ufupi  haki  na  wajibu  ni  vitu  vya  kuzingatia  sana katika  miamala  ya  mkopo  hasa  ikizingatiwa  kuwa  jambo  hilo  huhusisha  fedha  na  mali  kama  nyumba  ambamo  wakati  mwingine  ndimo  yalimo  makazi yetu.

1.WAJIBU  WA  MTOA  MKOPO.

Sheria ya  rehani  ya  mwaka 2008 imeeleza  vizuri  baadhi  ya  wajibu  walionao  watoa  mkopo. Tutaangalia  baadhi.

( a ) Kwanza  kabisa  ni  wajibu  wa  mtoa  mkopo kuhakikisha  anatafiti  na  kujua  iwapo  mtu  anayechukua  mkopo  ana  mke  au  ana mme. Hii  ni  kwasababu  kwa  mujibu  wa  sheria  ikiwa  nyumba  au  kiwanja  kinachowekwa  rehani  ili  kupata  mkopo  ni  cha  familia  kwa  maana  cha  wanandoa  basi  ni  lazima  wanandoa  wote  wawe  wameridhia  na  wote kwa  pamoja  watasaini waraka  maalum  kuthibitisha  ridhaa  zao.  Ikiwa  taasisi  ya  mkopo  haikufanya  utafiti  na  kujiridhisha  na  hili  basi  madhara  yatayopatikana   yatawaathiri  wao kwakuwa  utakuwa  ni  uzembe  kwa  upande  wao.  Hairuhusiwi  mwanandoa  mmoja kutumia  mali  ya  familia  kama  dhamana  bila  ridhaa  ya  mwingine.

( b ) Pia  mtoa  mkopo  ana  wajibu  mwingine  wa  kuhakikisha  mali  inayowekwa  kwake  kama  rehani  haijawekwa  rehani  sehemu  nyingine  yoyote,  haina  mgogoro  wowote  katika  mahakama  yoyote  ya  sheria, haina  zuio  lolote( caveat), na  wala  si  ardhi  ambayo  iko  katika  mpango  fulani wa serikali  ambao utatekelezwa  muda  mfupi  kabla  ya  deni  kuisha  au  hapo  baadae  kidogo. Hii  humuepusha  mtoa  mkopo  kutoingia  katika mgogoro  na  mamlaka  nyingine    hasa  za  serikali au  watu binafsi  ambao  wanaweza  kuwa  na  maslahi  katika  ile  ardhi  kabla  yake.

( d ) Wajibu  mwingine  muhimu  ni  kuhakikisha  wanamweleza  mchukua  mkopo  hali  halisi  kuhusu  huo  mkopo,  ikiwa  ni  pamoja  na  athari  zake  atakaposhindwa  kulipa, taratibu  za  marejesho,  uhuru  wa  kuongeza  mkopo na  ukomo, na  kila  kitu ambacho  ni  sehemu  ya  muamala  wa  mkopo.

2.  HAKI  ZA  MCHUKUA  MKOPO/MKOPAJI.

( a ) Iwapo  kuna  badiliko  lolote  katika  taratibu  za  ulipaji  deni  husika, riba  yake au  mabadiliko  yoyote  katika  tarehe  ya  marejesho  ni  haki  ya  mchukua  mkopo  kujulishwa  kwa  maandishi  maalum. Taasisi  kubwa  za  fedha  zimekuwa  zikilitekeleza  hili tofauti  na  taasisi  ndogo   ambazo  ndio  nyingi  kwa  sasa. Katika  taasisi  ndogo  isikushangaze siku  ya  kurejesha  mkopo  ukaambiwa kuwa  deni  limeongezeka  kwasababu  hii  na  hii  na  hivyo  hii  pesa  uliyoleta  haitoshi. Wanakiuka  sana  haki  za wakopaji.

( b ) Ardhi  iliyowekwa rehani  inaendelea  kuwa  haki  ya mchukua  mkopo  ikiwa  yule  aliyenunua  ardhi   hiyo kwa  njia  ya mnada  hajamalizia  hela  ya  malipo  ya  mnada  kama ilivyokubaliwa. Wako  watu  huweza  kulipa 25% tu  wakati  wa  mnada  na  kushindwa  kumalizia  salio. Hii  ikitokea  maana  yake  ni  kuwa  umiliki  bado  unakuwa kwa  mchukua  mkopo  na  muda  wowote  humo katikati   anaweza  kutafuta  hela  na /au  kufanya  vinginevyo  kukomboa  nyumba  yake.

( c ) Haki  ya  kupewa  taarifa  ya  siku  sitini  kabla  ya  mauzo  ni  haki  ambayo  huwa nairejea  mara  kwa  mara  kutokana  na  umuhimu  wake . Si tu  kutokana  na  umuhimu  wake  bali  pia  kutokana  na  namna  ambavyo  huwa  haizingatiwi  na  wengi hasa  wanadishaji (brokers).

( d ) Mkopaji  ana  haki  ya  kulipa  rejesho na  riba  kwa  viwango  vya  fedha  vinavyotambulika  na  kukubaliwa  kisheria. Baadhi  ya  taasisi fedha  hasa zile  ndogo  zimekuwa  zikijipangia  viwango  vya  marejesho  na  riba  ambazo  ni  kubwa  kupita  kiasi  huku  zikiwa  zimekiuka  taratibu za viwango  vya  fedha.  Hii  ni  pamoja  kuongeza  viwango  hivyo  kinyemela  huku  wakilenga  kujipatia  faida  kubwa .
Kwa  leo  ni  hayo.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



UPENDELEO WA KISHERIA KWA NYUMBA YA MAKAZI KABLA YA KUNADISHWA

|0 comments


Image result for nyumba  ya  familia

NA  BASHIR  YAKUB - 

Kisheria  haizuiwi  kuweka  rehani  nyumba  ya  makazi  kwa  ajili  ya  kupata  mkopo  kutoka  taasisi  yoyote  ya  fedha. Jambo la msingi  sana  ni  kuwa  watoa  mkopo   wajiridhishe   na  umiliki  wa  nyumba  hiyo  hasa  kwa  kuangalia ikiwa  ni  mali  ya  familia  au  hapana ili wachukue  hadhari  za  kisheria.
Nyumba  ya  makazi  ni  ipi.  Nyumba  ya  makazi  ni  ile  nyumba  ambayo  inatumiwa  na  binadamu  kuishi  lakini  zaidi  wanaoishi  mle  ndani  iwe  ni  familia  ya  mchukua  mkopo.  

Yawezekana  nyumba  ikawa  ni  ya makazi kwa  watu  wengine  lakini  ni  ya  biashara  kwa  mchukua  mkopo. Kwa  mfano  nyumba  za  kupanga  ambapo  mwenye  nayo  anaishi  kwingine   na nyumba  iko  kwingine ikiwa  na  watu  wengine. Nyumba  ya  namna  hii  haitaingia  kwenye  nyumba  ya  makazi  kwa  tafsiri  hii.  Hata  hivyo  haitarajiwi  mchukua  mkopo  kuhamia  kwenye  nyumba  ambayo  sio  ya  makazi  kwa  makusudi  na kuifanya  ya  makazi  akilenga   kuhadaa  ili  kupata  upendeleo  wa  mahakama.  Akifanya  hili  atakuwa  amedanganya  na  ni  kosa  kama  tutakavyoona.

1.MAKOSA  YA  KISHERIA  KWA  MKOPAJI.

( a ) Sheria  ya  masuala  ya  rehani  ya  2008  inamtaka  mkopaji  kutofanya  udanganyifu  wa  aina  yoyote  kwa  taasisi inayotarajia  kumpa mkopo. Moja  ya  udanganyifu  ni  kama  ilivyoelezwa  hapo  juu  lakini  pia  upo  udanganyifu  mwingine  mwingi  ambao hufanywa  na  wakopaji. Kwa  mfano  kuweka  rehani  nyumba  moja  kwa  taasisi  tofauti,  kudanganya  nyumba  sio  ya  familia  wakati  ni  ya  familia  na  udanganyifu  mwingine  mwingi  ambao  hulenga  kumnufaisha  mkopaji.  

2. ADHABU  YA  KUTENDA KOSA  LA  UDANGANYIFU  KATIKA  KUCHUKUA MKOPO.

Kisheria  tendo  likishakuwa  kosa  ni  lazima  iwepo  adhabu  yake.  Vivyo  hivyo  mkopaji  kumdanganya  mkopeshaji  nalo  ni  tendo  ambalo  huadhibiwa. Sheria  inasema  kuwa  hatia  ya udanganyifu  wa mkopaji   inapotangazwa  basi  adhabu  yake  ni  kulipa  faini  ambayo  ina  thamani  ya  nusu ya  mkopo  aliokuwa  amechukua. Hii  ina  maana kuwa,  kama  alichukua  mkopo  wa  milioni  200  basi  faini  yake  ni  milioni 100  halikadhalika  kama  alichukua  milioni  kumi  basi  faini  yake  ni  milioni tano.

Ikiwa  hana  hizo  hela  basi  itatakiwa  kwenda  jela  kutumikia  kifungo  kisichopungua  miezi  kumi  na  mbili. Kifungo  kisichopungua  miezi  kumi  na  mbili  maana  yake kinaweza  kuzidi miezi  kumi  na  mbili kutegemea  na  ukubwa  wa tatizo  lenyewe.  Hivyo  wakopaji  wajihadhari  na  kutoa  taarifa  za  uongo  hasa  kudanganya  kuwa  mali  si  ya  familia  au  kutumia  mali  moja  kuchukulia  mkopo  sehemu  zaidi  ya  moja n.k.

3.  UPENDELEO  KWENYE  NYUMBA  YA  MAKAZI

( a ) Sheria  inasema  kuwa   iwapo  itabainika  kuwa  nyumba   iliyowekwa  rehani  ni ya  makazi  na  mkopaji  analeta  zuio la  kutouzwa   nyumba  hiyo  basi  mahakama  ikijiridhisha  na  hilo  inaweza  kukubali  ombi  hilo.
Mahakama  itakubali  ombi  hilo  la  kuzuia  nyumba  kuuzwa  kwa  kuzingatia  kiwango  cha  hela  kilichosalia  yaani kile kiasi  ambacho   mkopaji  ameshindwa  kulipa. Mara  kadhaa  hutokea  kuwa  mkopaji  amelipa  kiasi  kikubwa  na  kusalia na  deni  la kiasi  kidogo  ambacho  kwa   akili  ya  kawaida  tu  na kutokana  na  mazingira  yaliyopo  akipewa  muda  mwingine  anao  uwezo  wa  kulipa  na  kumalizia  kabisa  deni. Ni  katika  mazingira  haya  zuio  la  kutouzwa  nyumba   ya  makazi  litakubaliwa.

( b ) Hili  litakwenda  sambamba  na  kuangalia  iwapo  wajibu  wa  mkopaji  uliowekwa  katika  mkataba  wa  mkopo unaweza  kuzungumzika. Ikiwa  mkopaji  alikuwa  mgonjwa  sana  na  ushahidi  upo  na  hivyo  alishindwa  kuendelea  na  biashara  na  hivyo  kutokurejesha, na sasa  ana  afya  njema  na  anaweza  kufanya  biashara  na  kurejesha, basi  wajibu  wake ikiwa  unaweza kurekebishika  kwa  namna  hiyo  au  namna  nyingine mahakama inaweza  kutoa  zuio  ili  kutoa  nafasi  nyingine  kwa  mkopaji.

( c ) Pia  ikiwa mahakama  itajiridhisha   kuwa  nyumba  husika  ina  thamani kubwa  kiasi  kwamba hata   mkopaji  akiongezewa  muda  mwingine  bado  akishindwa  kulipa  huko  mbeleni   nyumba  husika  ikiuzwa  mtoa  mkopo  hatakuwa  na  hasara  ataweza  kurejesha  hela  yake  yote pamoja  na  riba,  basi  zuio  la  kutouza  linaweza  kutolewa  kwa  kulizingatia  hilo.
Izingatiwe  kuwa  zuio  katika mazingira  haya  niliyoeleza   linawezekana  ikiwa nyumba  ilyowekwa rehani  ni  ya  makazi.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



Monday, 28 September 2015

UTARATIBU WA KISHERIA UNAPONUNUA ARDHI YA KIJIJI.

|0 comments

Image result for ardhi  ya  kijiji


NA  BASHIR  YAKUB - 

Tulipoandika namna  bora  na  taratibu  maalum  za  kufuata unapotaka  kununua  ardhi  tulisema  pia   kuwa   taratibu  za  ununuzi  wa  ardhi  huwa  zinatofautiana  kutegenea  na   mazingira  ya  kila  ardhi. Tukasema  unaponunua  ardhi  kwa  msimamizi  wa  mirathi  ni  tofauti  na  unaponunua  kwa  mmiliki  mwenyewe. Unaponunua  ardhi  ya  familia  ni  tofauti  na  unaponunua  isiyo  ya  familia. Vilevile  unaponunua  ardhi  ya  kijiji  ni  tofauti  na  unaponunua ardhi  isiyo  ya  kijiji.  Taratibu  hutofautiana  na  hasa  tofauti  ipo  katika  nyaraka  ambazo  zinatakiwa  kuambatanishwa  ikiwa  kama  ithibati  ya  ununuzi. Hata  uandishi  wa   mkataba  wa  manunuzi  pia  nao huwa na tofauti  katika  hili.

1.ARDHI  YA  KIJIJI  KWA  UWEKEZAJI.

Wako  watu  wamekuwa   wakinunua  ardhi  hasa  huko  vijijini  lakini  baadae  wamekuwa  wakijikuta  katika  migogoro  mikubwa  na  wenyeji. Mwamko  wa  kununua  maeneo  kama  bagamoyo, kisarawe, huko  chanika  dondwe na  maeneo  mengine  umekuwa  mkubwa  sana. Hata  hivyo  mwamko  unavyoongezeka  ndivyo  na  migogoro  inavyoongezeka. Kubwa  katika  migogoro  hii  ni  hatua  ya  wanunuzi  kutokufuata  utaratibu  wa  ununuzi aidha  kwa  kujua, kutokujua  au  kupotoshwa.
 Wakati  mwingine  ni  uelewa mdogo  miongoni  mwa  wenyeji  lakini  zaidi  ni  hili  la  kutofuata utaratibu. Mara  zote  huwa  tunasema  ni  bora  zaidi  mgogoro  unapotokea  halafu  ukukute  ulifuata  taratibu  wakati  wa  manunuzi. Bila  shaka hautakuwa  na  athari  kubwa  kwako  lakini  ni  mbaya   zaidi  ukitokea  halafu  ukukute kuna  taratibu  hukufuata kwa  bahati  mbaya  au  bila  kujua. Unakuwa  katika  hatari  ya  kupoteza. Unapokwenda  kununua  ardhi  ya  kijiji  kwasababu  yoyote  ile  hasa uwekezaji  upo  utaratibu maalum wa kufuata  nitakaoeleza.

2.  ARDHI  YA  KIJIJI  NI  NINI.

Ardhi  ya  kijiji  ni  ile  ardhi  iliyopo  katika  mipaka  ya  kijiji  fulani  ilyoainishwa  na  mamlaka  za  wilaya  husika  huku  ikiwa  na  hati ya  usajili  wa  kijiji. Ardhi  hii  hulindwa  kwa  taratibu  za  kimila  za  eneo  husika  ikiwa  ni  pamoja  na sheria  namba  4 ya  1999.

3.    UTARATIBU  WA  KUNUNUA  ARDHI  YA  KIJIJI  KISHERIA.

( 1 ) Maombi  maalum huandaliwa  na  kuwasilishwa  kwa  mtendaji  wa  kijiji  ambaye  hupatikana  katika  kila  kijiji.

( 2 ) Maombi  huandaliwa  katika  fomu  maalum  ambazo  hupatikana  katika  kila  ofisi  za  kijiji. Si  maombi  ambayo  huandaliwa  kama  barua  za  kawaida za maombi.

( 3 ) Ikiwa  mwombaji  ni  mtu  mmoja   basi   atasaini  sehemu  maalum  na ikiwa  ni  maombi  kwa  niaba  ya  famliia  basi  watu  wawili  kutoka  ile  familia  watasaini  na  ikiwa  ni  ardhi  kwa  ajili  ya  kikundi  pia  wawakilishi  wasiopungua wawili  kutoka  kile  kikundi  watasaini  kwa  niaba  ya  wengine.

( 4 ) Kama  mwombaji  ni  chama  cha  ushirika  au  kampuni  basi  inatakiwa  kuwepo  wadhamini  wawili   kwa  ajili  ya  shirika  au  kampuni  hiyo. Wanaweza  kuwa  zaidi  ya  wawili  lakini  wasipungue.

( 5 ) Kama  anayeomba  ardhi  si  mwenyeji  wa  eneo  husika  basi  atatakiwa  kuwa  na  wadhamini  wasiopungua  watano  ambao  ni  wenyeji  wa  eneo  hilo. Sharti  ni  kuwa  kati ya  hao  wadhamini  wasiwepo  ndugu  wa  mwombaji.

( 6 ) Mwombaji  atatakiwa  kuambatanisha katika  maombi  yake  tamko  linaloonesha  ardhi  nyingine  anayoimiliki  Tanzania  nje  na  hiyo  anayoomba.

( 7 )  Ikiwa  ardhi  inaombwa  kwa  ajili  ya  makazi  basi  mwombaji  atatakiwa  kuambatanisha  tamko  linaloonesha  kuwa  ataanza  ujenzi wa  makazi hayo ndani  ya  miezi  mitatu  tangu  siku  ya  kuidhinishiwa  ardhi.

( 8 ) Ikiwa  mauzo  ni heka 50 au  kuendelea  ni lazima  yaidhinishwe  na  mkutano  mkuu  wa  kijiji.

( 9 ) Baada  ya  kukamilisha  taratibu  hizo  halmashauri  ya  kijiji  itakaa  vikao  na  ndani  ya  siku  tisini itatakiwa  kutoa  majibu.
Kamwe  usikubali  kuuziwa  ardhi  ya  kijiji  na  viongozi   wa  kijiji  bila  kufuata  utaratibu  huu. Hii  hasa  ni kwa  wawekezaji  wanaochukua  maeneo  makubwa  kwa  shughuli  za  kiuchumi.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



Tuesday, 22 September 2015

NI HAKI YAKO KULIPWA HELA YA MFUKO WA HIFADHI YA JAMII UNAPOFUKUZWA KAZI.

|0 comments

Image result for HIFADHI  YA  JAMII

                
NA  BASHIR  YAKUB - 

Hela  ya  mifuko  ya  hifadhi ya jamii  ni  hela  ambayo  mwajiriwa  hukatwa  kiasi  kadhaa katika  mshahara  wake na  mwajiri  hutoa  kiasi  kadhaa  na  kuhifadhiwa  katika  mfuko uitwao  mfuko  wa hifadhi ya  jamii. Mfuko  wa  hifadhi  ya jamiii ni  kama NSSF, PSPF, LAPF, GEPF  n.k. Hii ndio  mifuko  ya  hifadhi  ya   jamii. Ipo  mifuko  ya  hifadhi  ya jamii  ambayo  huhudumia  mashirika  ya  umma  na  ipo  mingine  ambayo  huhudumia  mashirika  binafsi, makampuni  binafsi  na  sasa  ipo  inayohudumia  hata wajasiriamali  wadogo  ambao  sio  kampuni  wala  shirika.

1.LENGO  LA  MIFUKO  HII.

Lengo  kuu  ni  kumpunguzia  mtumishi  au  mfanyakazi  machungu  ya  maisha pindi  anapostaafu  au  kuacha   kazi.  Ni  kumwezesha  mtu   kuweza  kukabiliana  na  maisha  yake  baada  ya  kutokuwa  na  kazi  iliyokuwa  ikimwingizia  kipato. Ni  kumfanya  asikose  hata  matumizi  ya  kawaida  kama  chakula, malazi, mavazi   na  hata  matumizi  kama  ada  za  shule  ,matibabu  n.k. Mifuko    hii  haipo  Tanzania tu  bali  ni  ajenda  ya  dunia.  Ukienda  ulaya, Amerika, Asia  na  kote  Afrika utaikuta.

2.   HAKI  YA  MWAJIRIWA  KUSAJILIWA  NA  MIFUKO  HII.

Ni  haki  ya  kila  mwajiriwa kuwa  amesajiliwa  na  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii.  Ni  jukumu  la  kila  muajiri  kuhakikisha  kila  mwajiriwa  wake  amesajiliwa  katika  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii.  Suala  la  mfanyakazi  kusajiliwa  katika  mfuko  wa  hifadhi  si  hiari  au  hisani  kwa  mwajiri.  Ni  lazima   afanye  hivyo  kwakuwa  ni  takwa  la  kisheria.  Wapo  wafanyakazi  wengi  wameajiriwa  kwa  mikataba  lakini  hawajasajiliwa  na mifuko  hii.  Kufanya  hivyo  ni  kukiuka  haki  ya  mfanyakazi.  Kusajiliwa  na  mfuko  wa  hifadhi  ni  katika  mambo ambayo  yanatakiwa  kufanywa  awali  kabisa  ajira  ya  mtu  inapoanza.  Ni  wajibu  wako  mfanyakazi  pia  kuhakikisha   unamkumbusha  mwajiri  wako  kufanya  hivyo  na/au  ikishindikana  waweza  kumchukulia  hatua.

3. NI KOSA  LA  JINAI  KUTOMSAJILI  MWAJIRIWA  KATIKA  MFUKO  WA  HIFADHI.

Ukisikia  makosa  ya  jinai  ni  yale  makosa  ambayo  mtu  hushitakiwa  na  Jamhuri.  Ni makosa ambayo  mnatendeana wawili  lakini  anayeshitaki  ni  Jamhuri/serikali. Ni makosa  ambayo  ukipatikana  na  hatia  adhabu  zake  huwa  ni  vifungo, faini  na  wakati  mwingine  kuchapwa  bakora.  Kwa  maana  hii  mwajiri  yeyote ambaye   amekataa  kumsajili  mfanyakazi  wake  katika  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii  anakuwa  ametenda  kosa  la  jinai  ambapo  anastahili  kuadhibiwa. Kosa  hili  limeingizwa  katika  makosa  ya  jinai  kutokana  na  umuhimu  wa mifuko hii.  Lakini  pia ni  kutokana  na  ukweli  kuwa  waajiri  wengi  wasingependa  kuwasajili  waajiriwa  wao  kwakuwa  wao  hutakiwa  kuchangia  asilimia  kadhaa  ya  fedha  kila  mwezi . Kwakuwa  wasingependa  wachangie  fedha  hizi  ndio  maana  ikaingizwa  kwenye  jinai  ili  wa  kuogopa  na  aogope.

4.   KULIPWA  HELA  YA  HIFADHI  UNAPOFUKUZWA  KAZI.

Wapo  wanaojua  kuwa  mtu  anapofukuzwa  kazi  kwa  makosa  basi  hupoteza  haki  ya  fedha  hizi   za  mfuko  wa  jamii  ambao  amekuwa  akizichangia.  Hili  si  kweli.  Kuacha  kazi  kwa  kustaafu,  kufukuzwa  kazi,  kumaliza mkataba  au  kuvunjiwa  mkataba  vyote  kwa  pamoja  hutoa  nafasi  kwa  mwajiriwa  kupata  haki  yake  ya  fedha  za hifadhi  ya  jamii.  Ni  wajibu  wa  mwajiri  kuhakikisha  mfanyakazi  kabla  ya  kuondoka  ofisini  kutokana  na  sababu  nilizotaja  anamshughulikia  kuhakikisha anapata  fedha  zake  za  hifadhi  ya  jamii.  Ikiwa  fedha  hizi  hazikutolewa   basi  ni  haki  ya  mfanyakazi  kumfungulia  mashtaka   mwajiri  kumtaka  amlipe  fedha  hizo.  Fedha   hizi  ni  moja ya stahili  anazostahili  mwajiriwa  pindi  anapomaliza  kipindi  chake  cha  utumishi  aidha  kwa  kufukuzwa  kazi,  kuvunjiwa  mkataba  au  vinginevyo.  Ni  haki  na  ni  lazima  fedha  hizo kulipwa.

5. JE MFANYAKAZI ANA  HAKI  YA  KUCHAGUA  MFUKO  ANAOUTAKA.

Mifuko  ya  hifadhi  ya  jamii ipo  mingi  na  hutofautiana  masharti  pamoja na  faida. Hilo  linaibua swali la  nani  ana  haki  ya kuchagua  mfuko  kati  ya  mwajiri  na  mwajiriwa. Kimsingi  sheria  haijaweka  wazi nani  kati  ya  hawa  wawili  ana  haki  ya  kuchagua  mfuko. Hii  ina maana  suala  la  mfuko upi  utumike  laweza  kuwa  suala  la  maelewano  baina  ya  mwajiri  na  mwajiriwa wakati  wa  kuingia  mkataba. Hata  hivyo  mazoea(practise)  imekuwa  ni  mwajiri  ndiye  humchagulia  mwajiriwa  mfuko.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.