Tuesday 29 August 2017

MPANGAJI APEWE NOTISI YA MUDA GANI KUONDOKA KWENYE NYUMBA ?.


Image result for MPANGAJI ATOLEWA  VITU  NJE

NA  BASHIR  YAKUB -

Kuna  matatizo  sana   kati  ya  wapangaji  na  wenye  nyumba  kuhusu  notisi  ya  kuondoka  au  kuondolewa.  Wako  wanaosema  notisi  ni  mwezi mmoja,  wako  wanaosema  ni  miezi  mitatu  n.k.  Kama  ni kweli  ama  hapana  tutaona hapa   sheria  inasemaje.

Masuala  ya  pango  yanaongozwa  na  sheria  kuu  mbili.  Moja  sheria  ya  ardhi  namba  4  ya  mwaka  1999  na  pili  sheria  ya  mikataba  sura  ya  345.  Kwa  pamoja  sheria  hizi  mbili  husimamia   jambo  hili.

1.MIKATABA YA  PANGO.

Mikataba ya pango  inahusisha  makubaliano  ya  upangaji  kati  ya  mwenye  nyumba  na  mpangaji  au  mpangaji  na  mpangaji  mwingine  wa  pili.  Pango  laweza  kuwa la  nyumba  ya  kuishi,   kwa  ajili ya  biashara,  nyumba  ya  ibada  au  shughuli  nyinginezo.   Yote  haya  yataingia  katika  maana  ya  pango.

2.   AINA   ZA  MIKATABA  YA   PANGO.

Sheria  ya ardhi   vifungu  vya  78  na  79  inatambua   mikataba ya  upangaji  ya  muda  mrefu  na  vipindi  vifupi. Inatambua  pango  la  wiki,  mwezi,  miezi,  mwaka  na  miaka.  Imetoa  uhuru  kwa  wahusika  wenyewe  kuamua  ni  muda  gani  wangependa  kuingia  mkataba.

3.   NOTISI  YA  KUONDOKA.

Katika  vitu  muhimu  sana  katika  suala  la  pango  ni  notisi ya kuondoka   au  kuondolewa  katika  pango.  Jambo  la  kuzingatia awali  kabisa  ni  kuwa   notisi  hii  ni  muhimu  pande  zote  mbili.  Upande  wa  mwenye  nyumba  na  upande  wa  mpangaji.  Kila  mmoja  kwa  nafasi  yake  anawajibika  kutoa  notisi  kwa  mwenzake  panapo  mahitaji  ya  kuondoka  au  kuondolewa.

Ikumbukwe  notisi  si  kwa  ajili  tu  ya kuondoka  na kuondolewa   bali  pia   hutakiwa  yanapotokea mabadiliko  yoyote  katika  masharti  ya  mkataba. Hii  ina  maana  hata  kuongeza  kodi, kupanga  kukagua  nyumba, kufanya  marekebisho  n.k.  notisi  yafaa  itolewe.

4.  NOTISI  NI  YA MUDA  GANI.

Sheria  haikutamka  moja  kwa  moja  notisi  ya  kuondoka au  kuondolewa  iwe  ya  muda  gani. Kinachohitajika  na cha  lazima ni kuhakikisha  notisi inatolewa  lakini  pia  inatolewa  katika   muda   unaokadirika na  kuingia  akilini( reasonable ). 

Kwahiyo  notisi  inaweza  kuwa  muda  wowote  isipokuwa muda  huo  uwe  unaokadirika  na  kuingia  akilini.
 Ili  tujue  muda  unaokadirika     yafaa tuangalie  muda  wa  pango  ulio  katika mkataba. Kwa  mfano  mtu  mwenye  mkataba wa  miaka  mitano  huwezi  kumpa  notisi  ya kuondoka  ya   mwezi  mmoja  au  hata miwili. Lakini   mwenye  mkataba  wa  miezi  minne   au  mitatu  unaweza  kumpa  notisi  hata ya  mwezi  mmoja.  Mwenye  miezi  sita  hata  miezi  miwili  inaweza  kuwa  sawa  na  wa  mwaka  miezi  mitatu  inaweza  kuwa  sawa.

Jambo  moja  nisisitize  sana  hapa. Kwakuwa  sheria  haijataja  wazi muda  wa  notisi  ya kuondoka  ni  vema  sana  tena sana  kuhakikisha  mkataba  wenu  wa  pango unaeleza  muda  wa notisi.  Ni  muhimu  sana.  Mkataba  ueleze  wazi  kabisa   notisi  itakuwa  ni  ya  muda  gani   ikiwa  mwenye  nyumba  anataka  nyumba  yake  na  ikiwa  mpangaji  anahitaji  kuondoka.  Na  katika  kukubaliana,   muda  wowote  mtakaokubaliana  unatosha  na  unakubalika  kisheria  kwasababu  umetokana na  hiari  ya  mkataba. 

Usikubali  kusainishwa  mkataba  ambao  hauelezi  muda  wa  notisi .  Hili  litakuondolea  masahibu  baadae.
Hapo  juu  tumesema  huwezi  kumuondoa  mpangaji  kwenye  nyumba  bila kumpa  notisi.  Hili  ni  muhimu  kulirudia.  Notisi  ni  lazima  isipokuwa  muda  wa  notisi  ndio  utatofautiana.

5.  KUMUONDOA  MPANGAJI   KABLA  YA  MUDA  WA  MKATABA KUISHA.

Hili  nalo  ni  kosa  na  ikitokea  basi  mwenye  nyumba  lazima  alipe  fidia.  Hili  ni  kosa  la  kuvunja  mkataba  kama  ilivyo  kuvunja  mikataba  katika  mikataba  mingine  yoyote.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


16 comments:

  • Rama d 255 says:
    20 August 2019 at 23:03

    kipengele cha tano, kipitie vzur kwenye sheria na regulations zake zote, pia hata suala la notisi pitia regulation zake pia,

  • Unknown says:
    19 October 2019 at 10:43

    Na mpangaj anapovunja mkataba inapaswa adai pesa yake ya miez/ miaka iliobaki?

  • Unknown says:
    3 November 2019 at 06:52

    Naomba kujua veep kama mpangaji kamaliza mkataba na hakutoa taarifa za kuendelea mkataba.na mwenye nyumba anataka nyumba ake na hakumpa taarifa zakumpokonyaa nyumbaa. Sheria inasemaje

  • Unknown says:
    7 November 2019 at 04:46

    Vipi kw mpangaji mwenye deni na hana mkataba

  • Unknown says:
    3 December 2019 at 09:59

    Naomba kuuliza, Mimi ni mpangaji ila kuna mvutano kwa wasimamizi wa mirathi, shauri lao linaendelea mahakamani, msimamizi A, ambaye tumelipa kodi ya mwaka, inasadikiwa ameshindwa mahakamani, inabidi msumamizi B, anasimamia mirathi, swali: je mkataba wangu mpaka uishe ndipo mkataba mpya niingie na msimamizi B au msimamizi B anahaki ya kunitowa kwenye nyumba bila kurudishiwa kodi iliyobaki ?

  • Itugnabiol says:
    13 January 2020 at 09:39

    Ukarabati wa nyumba, utengenezaji wa miundombinu mibovu ya maji na ile ya umeme iliyochakaa ni kazi ya nani kati ya mpangaji na mwenye nyumba? Asante

  • Unknown says:
    1 May 2020 at 00:10

    Vipi kuhusu kuvunja mkataba lakini siyo kwa ghafla unakua umempa muda mpangaji je anatakiwa kulipwa fidia!
    Mbali na ile pesa atakayorudishiwa yamieziiliyobakia!

  • Unknown says:
    30 June 2020 at 07:20

    Kama mpangaji hana mkataba na makubiano mda wake umeisha sheria inasemaje.

  • Unknown says:
    25 July 2020 at 00:23

    Inakuaje kama, mkataba umeisha, makubaliano ya mwenye nyumba na mpangaji ikawa ni kulipia kwa mwezi mmoja mmoja, japo mwenye nyumba hajakukabidhi mkataba katika katika nakala ya karatasi(hard copy), na baada ya kipindi kifupi(miezi miwili), akataka kukufukuza katika nyumba yake??

  • Unknown says:
    9 October 2020 at 23:30

    Je mm ni mpangaji na nimemcheleweshea mwenye nyumba kumpa kodi mwez moja na amekuja kazn kushitaki na kazn wanataka kunichukulia hatua je ni haki kisheria kuwa ofcn kwangu Wana mamlaka ya kunichukulia hatua dhid ya mm na mwenye nyumba wangu

  • Abdallah says:
    8 May 2021 at 13:28

    Napenda kujua sheria inasemaje kuhusu mpangaji alikaa eneo kwamda wa miaka 8.bira kuvunja masharti ya mkataba kodi analipa kwa mwaka mmoja analipa kwawakati.mwanzo wa mwaka. namkataba unasema siku mpangaji akitaka kuhama atoe talifa kabla ya miezi 3) na alipie kama tulivyo kubalia pande zote mbili.nampangaji akitaka kuendelea andike barua yakujurisha.kama anaendelea hapo akusema najulisha kwa wakatigani. hilipo fika 28/12/2017 nikamjulisha kua naendelea kutumia eneo. th.30/12/2017 nikapewa notice ya masaa24. niondoke katika eneo hilo. maelezo yaliyoko kwenye notice inasema tumeamua kutopangisha tena.naomba ushauli nifanyeje hili niweze kupata haki zangu?

  • Muuminu abass says:
    27 July 2021 at 08:12

    Naomba kujua iwapo mi nimepanga khalafu baada ya mwezi 1 mwenye nyumba anakuja kuniambia kwamba chumba ishachukuliwa kwaiyo natakiwa nitoke hapo natakiwa nifanyeje

  • Unknown says:
    22 August 2021 at 21:49

    Mm kaniambia baada ya Kodi kuisha nirudishe chumba inakuaje hapo Kama nitakua cjapata chumba

  • Unknown says:
    22 August 2021 at 21:52

    Namkataba hajanipatia hii miezi sita amefanya kuandika kwenye kikaratasi nakumpa mtoto

  • Marco says:
    15 December 2021 at 20:32

    Sheria iko vipi kwenye mapangishano ya nyumba ya kuishi ambayo hayana mkata wa kwamba mpangaji atakaa mda gani Bali makubaliano yaliyopo n kwenye Kodi tu. Na badae mpangaji akakaa kwenye nyumba takriban mda wa mwaka mzima bila kulipa kwasababu tu mwenye nyumba Yuko mbali nae, ili kusudi ssa mweny nyumba apate haki ya kodi yake anatakiwa afuate vitu gan pp

  • Ajanak says:
    8 July 2023 at 23:10

    non sense hawana mamlaka hata kidogo

Post a Comment