Tuesday 22 September 2015

NI HAKI YAKO KULIPWA HELA YA MFUKO WA HIFADHI YA JAMII UNAPOFUKUZWA KAZI.


Image result for HIFADHI  YA  JAMII

                
NA  BASHIR  YAKUB - 

Hela  ya  mifuko  ya  hifadhi ya jamii  ni  hela  ambayo  mwajiriwa  hukatwa  kiasi  kadhaa katika  mshahara  wake na  mwajiri  hutoa  kiasi  kadhaa  na  kuhifadhiwa  katika  mfuko uitwao  mfuko  wa hifadhi ya  jamii. Mfuko  wa  hifadhi  ya jamiii ni  kama NSSF, PSPF, LAPF, GEPF  n.k. Hii ndio  mifuko  ya  hifadhi  ya   jamii. Ipo  mifuko  ya  hifadhi  ya jamii  ambayo  huhudumia  mashirika  ya  umma  na  ipo  mingine  ambayo  huhudumia  mashirika  binafsi, makampuni  binafsi  na  sasa  ipo  inayohudumia  hata wajasiriamali  wadogo  ambao  sio  kampuni  wala  shirika.

1.LENGO  LA  MIFUKO  HII.

Lengo  kuu  ni  kumpunguzia  mtumishi  au  mfanyakazi  machungu  ya  maisha pindi  anapostaafu  au  kuacha   kazi.  Ni  kumwezesha  mtu   kuweza  kukabiliana  na  maisha  yake  baada  ya  kutokuwa  na  kazi  iliyokuwa  ikimwingizia  kipato. Ni  kumfanya  asikose  hata  matumizi  ya  kawaida  kama  chakula, malazi, mavazi   na  hata  matumizi  kama  ada  za  shule  ,matibabu  n.k. Mifuko    hii  haipo  Tanzania tu  bali  ni  ajenda  ya  dunia.  Ukienda  ulaya, Amerika, Asia  na  kote  Afrika utaikuta.

2.   HAKI  YA  MWAJIRIWA  KUSAJILIWA  NA  MIFUKO  HII.

Ni  haki  ya  kila  mwajiriwa kuwa  amesajiliwa  na  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii.  Ni  jukumu  la  kila  muajiri  kuhakikisha  kila  mwajiriwa  wake  amesajiliwa  katika  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii.  Suala  la  mfanyakazi  kusajiliwa  katika  mfuko  wa  hifadhi  si  hiari  au  hisani  kwa  mwajiri.  Ni  lazima   afanye  hivyo  kwakuwa  ni  takwa  la  kisheria.  Wapo  wafanyakazi  wengi  wameajiriwa  kwa  mikataba  lakini  hawajasajiliwa  na mifuko  hii.  Kufanya  hivyo  ni  kukiuka  haki  ya  mfanyakazi.  Kusajiliwa  na  mfuko  wa  hifadhi  ni  katika  mambo ambayo  yanatakiwa  kufanywa  awali  kabisa  ajira  ya  mtu  inapoanza.  Ni  wajibu  wako  mfanyakazi  pia  kuhakikisha   unamkumbusha  mwajiri  wako  kufanya  hivyo  na/au  ikishindikana  waweza  kumchukulia  hatua.

3. NI KOSA  LA  JINAI  KUTOMSAJILI  MWAJIRIWA  KATIKA  MFUKO  WA  HIFADHI.

Ukisikia  makosa  ya  jinai  ni  yale  makosa  ambayo  mtu  hushitakiwa  na  Jamhuri.  Ni makosa ambayo  mnatendeana wawili  lakini  anayeshitaki  ni  Jamhuri/serikali. Ni makosa  ambayo  ukipatikana  na  hatia  adhabu  zake  huwa  ni  vifungo, faini  na  wakati  mwingine  kuchapwa  bakora.  Kwa  maana  hii  mwajiri  yeyote ambaye   amekataa  kumsajili  mfanyakazi  wake  katika  mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii  anakuwa  ametenda  kosa  la  jinai  ambapo  anastahili  kuadhibiwa. Kosa  hili  limeingizwa  katika  makosa  ya  jinai  kutokana  na  umuhimu  wa mifuko hii.  Lakini  pia ni  kutokana  na  ukweli  kuwa  waajiri  wengi  wasingependa  kuwasajili  waajiriwa  wao  kwakuwa  wao  hutakiwa  kuchangia  asilimia  kadhaa  ya  fedha  kila  mwezi . Kwakuwa  wasingependa  wachangie  fedha  hizi  ndio  maana  ikaingizwa  kwenye  jinai  ili  wa  kuogopa  na  aogope.

4.   KULIPWA  HELA  YA  HIFADHI  UNAPOFUKUZWA  KAZI.

Wapo  wanaojua  kuwa  mtu  anapofukuzwa  kazi  kwa  makosa  basi  hupoteza  haki  ya  fedha  hizi   za  mfuko  wa  jamii  ambao  amekuwa  akizichangia.  Hili  si  kweli.  Kuacha  kazi  kwa  kustaafu,  kufukuzwa  kazi,  kumaliza mkataba  au  kuvunjiwa  mkataba  vyote  kwa  pamoja  hutoa  nafasi  kwa  mwajiriwa  kupata  haki  yake  ya  fedha  za hifadhi  ya  jamii.  Ni  wajibu  wa  mwajiri  kuhakikisha  mfanyakazi  kabla  ya  kuondoka  ofisini  kutokana  na  sababu  nilizotaja  anamshughulikia  kuhakikisha anapata  fedha  zake  za  hifadhi  ya  jamii.  Ikiwa  fedha  hizi  hazikutolewa   basi  ni  haki  ya  mfanyakazi  kumfungulia  mashtaka   mwajiri  kumtaka  amlipe  fedha  hizo.  Fedha   hizi  ni  moja ya stahili  anazostahili  mwajiriwa  pindi  anapomaliza  kipindi  chake  cha  utumishi  aidha  kwa  kufukuzwa  kazi,  kuvunjiwa  mkataba  au  vinginevyo.  Ni  haki  na  ni  lazima  fedha  hizo kulipwa.

5. JE MFANYAKAZI ANA  HAKI  YA  KUCHAGUA  MFUKO  ANAOUTAKA.

Mifuko  ya  hifadhi  ya  jamii ipo  mingi  na  hutofautiana  masharti  pamoja na  faida. Hilo  linaibua swali la  nani  ana  haki  ya kuchagua  mfuko  kati  ya  mwajiri  na  mwajiriwa. Kimsingi  sheria  haijaweka  wazi nani  kati  ya  hawa  wawili  ana  haki  ya  kuchagua  mfuko. Hii  ina maana  suala  la  mfuko upi  utumike  laweza  kuwa  suala  la  maelewano  baina  ya  mwajiri  na  mwajiriwa wakati  wa  kuingia  mkataba. Hata  hivyo  mazoea(practise)  imekuwa  ni  mwajiri  ndiye  humchagulia  mwajiriwa  mfuko.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



0 comments:

Post a Comment