Monday 10 August 2020

UNAPOMPA WAKILI KESI YAKO HAKIKISHA UNAFUATILIA.

 Journalism in blood: Mawakili 618 waapishwa katika viwanja vya Law school


NA  BASHIR  YAKUB  - 

Usimpe wakili kesi yako akusimamie halafu ukalala nyumbani na kujisahau. Ni lazima uhakikishe unafuatilia kujua kinachoendelea. Na kufuatilia sio lazima kila  siku kesi inapoitwa mahakamami nawe uwepo,laa hasha. Hii ni kwasababu kama utalazimika kila kesi inapoitwa na wewe uwepo mahakamani kwa namna fulani tunaweza kupoteza maana ya kumweka wakili. Ninachomaanisha ni kuwa, ni muhimu ukawa unapata mrejesho wa mara kwa mara kujua kinachoendelea, hata kwa kupiga simu.

Umuhimu na ulazima wa kufuatilia unatokana na ukweli kuwa kesi ni yako. Kesi sio ya wakili. Wakili yeye ni mwakilishi tu. Kwa msingi huu ikiwa kuna jambo litakwenda mrama madhara yanakuja kwako mwenye kesi na sio kwa wakili.

Mfano mmoja wapo  upo kwenye kesi ya   Edga Msola vs Dr. Edward Wilson Ngale na Philip Japhet Mangula,Maombi Namba 442/2018.  Katika kesi hii ndugu Edga alimpa wakili kazi ya kuandaa na kupeleka mahakamani mawasilisho ya hoja za rufaa(submission in support of grounds of appeal). Hata hivyo inaonekana muda aliopewa wakili kupeleka mawasilisho hayo uliisha bila kupeleka.

Matokeo yake rufaa nzima ikafutwa. Pia inaonekana hayo yalifanywa bila Ndugu Edga ambaye ni mwenye kesi kujua. Na hii ilitokana na kuamini kwake kuwa kesi anayo wakili na hivyo kila kitu atafanya yeye. Hata hivyo baadae Ndugu Edga alikuja kujua kuwa rufaa yake imefutwa kwa kushindwa kupeleka mawasilisho mahakamani.

Kutokana na hilo akamtafuta wakili mwingine ambaye aliamua kupeleka maombi ya kuomba rufaa iliyofutwa kusajiliwa upya(re-admission). Katika maombi hayo hoja na sababu kubwa aliyoitoa ndugu Edga ili rufaa yake iliyotupwa iweze kukubaliwa kusajiliwa upya ni kuwa, alimuamini na kumkabidhi wakili wake kazi yote  na hivyo hakujua kama wakili alishindwa kupeleka mawasilisho na hivyo kupelekea kesi yake kufutwa.

Kwahiyo aliishawishi mahakama kuwa hilo halikuwa kosa lake bali la wakili, na hivyo kufutwa rufaa yake kwa kosa la wakili sio jambo la haki , na  kwasababu hiyo aliiomba mahakama ikubali kusajili upya rufaa yake ili aweze kusikilizwa anasema nini kwenye hiyo rufaa.

Maamuzi ya mahakama katika hili ilisema kuwa, sababu ya kuwa wakili hakufanya kitu fulani sio sababu ya msingi ya kuishawishi kukubali kusajili upya rufaa yake. Kwa msingi huu haya maombi yake ya kuomba rufaa yake irejeshwe nayo yakatupwa.

Maana yake kwa kosa lile la wakili la kutopeleka mawasilisho kwa wakati limesababisha huyu ndugu Edga apoteze rufaa yake moja kwa moja kwakuwa amekataliwa hata kuirudisha. Kama alikuwa na haki ya kushinda kwenye rufaa maana yake amepoteza hiyo haki.

Na wakati mahakama  ikitupa maombi yake ya kurejesha rufaa ilisisitiza kuwa, pamoja na kuwa kesi yake alimkabidhi wakili bado alikua na wajibu wa kufuatilia kujua kinachoendelea huko mahakamani. Ilisema kama angefuatilia angejua kinachoendelea na hivyo kumuweka katika nafasi nzuri ya kuchukua hatua mapema.

Kitendo chake cha kutokufuatilia mpaka haya yote yakatokea mahakama ilikiita uzembe kwa upande wa ndugu Edga ambaye ndiye mwenye kesi. Na hapa ndipo ninapowashauri kuhakikisha mnafuatilia kesi zenu hata kama zipo kwa wakili kwasababu madhara yanakuja kwenu.

Nimesema kuwa hii haimaanishi kuwa mawakili hawafanyi kazi zao vizuri, hapana. Isipokuwa wakili naye ni binadamu, anaweza kupitiwa, anaweza kukutwa na dharula iliyo nje ya uwezo wake kama ugonjwa ghafla,kufiwa ama naye akawa mzembe.

Kwa hiyo myazingatie hayo.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

 

 


0 comments:

Post a Comment