Monday 10 August 2020

NOTISI YA SIKU 14 KABLA YA KUPIGA MNADA NYUMBA.

 

NYUMBA ZA LUGUMI ZAPIGWA MNADA - HABARI MSETO


NA  BASHIR  YAKUB  - 

Hii ni moja ya sehemu ambayo wanadishaji/madalali(auctioneer)  wengi  huwa wanawakosea wadaiwa. Huwezi kufikia hatua ya kuuza nyumba au kiwanja cha mtu kabla hujampa taarifa ya siku 14, na kuhakikisha hizo siku 14 kuwa zimepita. Madalali wengi  akishapewa kazi na benki ama taasisi nyingine ya mikopo kwa ajili ya kunadisha, basi anaanza kazi ya kuuza hapo hapo,au baada ya mda mchache.

Kifungu cha 12((2) and (3) cha Sheria ya Madalali Wanadishaji sura ya 227 kinasema kuwa hakuna ruhusa kwa dalali yoyote kuuza nyumba ama kiwanja cha mtu mpaka mtu huyo awe amepewa taarifa ya siku 14, na siku hizo ziwe zimeisha.

Kumbe tunaona kuwa haitoshi tu kumpa mtu taarifa  ya siku 14, bali pia hizo siku 14 alizopewa ni lazima ziwe zimeisha. Maana yake tunahesabu siku 14 tangu ulipopokea taarifa,na baada ya huo mda ndo tunasema zimeisha.  Kuuza kunaweza kuanza siku ya 15, siku ya 14 kamili dalali hawezi kuuza nyumba yako.

Nasisitiza eneo hili kwasababu baadhi ya madalali wamekuwa na tabia ya kutoa hiyo notisi ya siku 14, lakini kabla ya muda huo kuisha  anauza nyumba/kiwanja. Hili ni kosa na kama hilo limetokea kwako basi uuzaji huo ni batili na hautambuliwi na sheria.

Katika kesi ya DOSCA DIDON KARANJA vs TPB BANK PLC, NAMIC INVESTMENT LTD na HAIDARI MOHAMMED HARIRI, Madai ya Ardhi Namba 64/2015, Dosca alipewa notisi ya kuuza tarehe 14 August 2015 na tarehe 16 August 2015, yaani siku mbili baadae, dalali akauza nyumba yake.

Dosca alifungua kesi mahakamani kulalamikia baadhi ya mambo likiwemo hili. Mahakama kuu ilitoa hukumu kuwa, hata kama alikuwa anadaiwa na benki na ameshindwa kurejesha marejesho,bado mauzo ya nyumba yake yalikuwa batili na haramu. Kwa msingi huu akarejeshewa umiliki wa nyumba yake.

Kwahiyo ni muhimu ukalijua hili  ili haki iweze kutendeka. Ni vigumu sana haki yako kutendeka kama wewe mwenyewe hujui hata hiyo haki kama unayo.Nimeandika mara nyingi kuwa kudaiwa au kushindwa kurejesha hakuna uhusiano wowote na kusigina haki za mdaiwa. Mdaiwa ana haki nyingi na lazima zizingatiwe anaposhindwa kurejesha.

Moja ya tatizo la taasisi za mikopo ni kuwapa wakopaji limkataba kama kitabu, lenye kurasa nyingi,lililoandikwa kwa kiingereza kigumu cha kisheria, kiasi kwamba hata kama unajua kiingereza bado lugha iliyo kwenye likitabu hilo itakutatiza tu. Jambo ambalo hata kama zimeelezwa haki za mkopaji mle ndani, si rahisi kuzijua  na akajifunza. Ingekuwa ni vyema zaidi mkopaji pamoja na semina za matumizi ya pesa ya mkopo, lakini pia akafundishwa haki zake hasa wakati atakaposhindwa kurejesha.

Kifungu nilichotaja hapo awali cha 12((2) and (3) cha Sheria ya Madalali Wanadishaji Sura ya 227, kinasisitiza kuwa haitoshi tu kumpa mdaiwa notisi ya siku 14, bali pia notisi hiyo iwe katika lugha inayoeleweka, na yasiwe tu maandishi katika karatasi, bali pia namna nyingine za kumjulisha zitumike.

Kwahiyo  wadaiwa yafaa myajue haya ili muwe na uwezo wa kuchukua hatua stahiki.  

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

 


0 comments:

Post a Comment