Monday 10 August 2020

KOSA LA KUJIPATIA MALI KWA NJIA YA UDANGANYIFU LINATUMIWA VIBAYA NA POLISI.

 

Mtuhumiwa wa kifo cha Mowzey Radio mikononi mwa Polisi - Bongo5.com


NA  BASHIR  YAKUB - 

Yapo mambo ambayo kwa mujibu wa sheria sio kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu. Hata hivyo polisi kwenye vituo vyao wamekuwa wakilazimisha mambo hayo kuwa kosa hilo la kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu kwasababu wanazozijua wao, mojawapo ikiwa ni mchongo kutoka kwa mlalamikaji.

Masuala ya watu kudaiana hela ama migogoro ya ardhi  kama mtu mmoja kuwauzia watu tofauti ardhi moja si masuala ya polisi, na wala si makosa ya kujipatia pesa ama mali kwa njia ya udanganyifu.

Tumesema mara nyingi kuwa, mamlaka ya polisi ni  kushughulikia masuala ya jinai tu. Masuala ya kudaiana hela ni masuala ya madai na sio jinai. Kwa msingi huu yapo nje kabisa ya mamlaka yao. Masuala ya kudaiana hela yanaongozwa na sheria ya mikataba Sura ya 345, pamoja na Sheria nyingine za fedha na rehani, wakati masuala ya migogoro ya ardhi yanaongozwa na Sheria namba 4 na 5 za ardhi, Sheria ya Usajili wa ardhi na nyinginezo mtambuka.

Kwahiyo makosa haya na mengine yanayofanana na haya hayawezi kuitwa ya kujipatia mali ama fedha kwa njia ya udanganyifu. Mara nyingi makosa haya yamekuwa yakipelekwa huko kwenye kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu kwa makusudi ili kumkomoa mtu ili awekwe ndani nk.

Vifungu vya 301, na  302, vya Kanuni za Adhabu, Sura ya 16, vinaelezea kosa la kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu kumaanisha ujinai. Mfano wa makosa ya kujipatia mali ama fedha kwa njia ya udanganyifu ni wale wanaotuma SMS au kupiga simu na kusema umejishindia kitu fulani na hivyo utume hela ili upate kitu hicho, na pesa kweli zikatumwa kwake, huku jambo hilo sio kweli. Fedha hiyo itakuwa imepatikana  kwa njia udanganyifu.

Au mtu anakwambia lete hela nikuletee mali fulani au nakuagizia japan huku akijua sio kweli. Fedha hizo akizipokea na asilete alichoahidi zitakuwa zimepatikana kwa njia ya udanganyifu. Mifano kama hiyo ndiyo ya kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu.

Aidha, tunasisitiza tena kuwa masuala ya kudaiana hela, au ugomvi wa ardhi hayaingii kwenye jinai ya kujipatia pesa/mali kwa njia ya udanganyifu, bali ni madai. Na hivyo, ni kosa kabisa askari yeyote katika kituo chochote kujihusisha na masuala ya madai, labda iwe kwa ushauri. Kama askari atachukua masuala haya ili awashauri au awapatanishe hiyo itakua ni sawa. Ila kama atayachukua ili afungue jalada la kesi hilo ni kosa.

Mahakama kuu ya Tanzania imeshatoa maamuzi mengi kuelezea jambo hili na moja ya maamuzi ya hivi karibuni ni katika Madai ya Rufaa Namba 23/2017 kati ya RIBENT RWECHUNGURA vs PONSIAN MUTAYABARWA ambapo Jaji  KAIRO alisema ni makosa mgogoro  wa ardhi kufunguliwa polisi.

 

Sehemu husika ambapo yafaa upeleke masuala hayo ni mahakamani moja kwa moja. Ukiulizia mahakamani au ukampata Wakili utaelekezwa utaratibu mzima wa hapo mahakamani.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

 


0 comments:

Post a Comment