Monday 10 August 2020

MKURUGENZI WA KAMPUNI HARUHUSIWI KUFUNGUA KESI KWA NIABA YA KAMPUNI.

 

Appointment of Directors: Managing Director, Shareholders, Resolution


NA  BASHIR  YAKUB -  

Kampuni zote, ziwe kubwa au hata zile zenye watu wawili au zile za familia huwa na wakurugenzi wake(Directors). Kampuni ikiwa na watu wawili utakuta hao hao ndio wanahisa na haohao ndio wakurugenzi. Basi yote ni sawa na inaruhusiwa kisheria.

Hata hivyo, kampuni hiyo hata kama ni ya watu wawili au ya familia mke na mme ama vinginevyo, mkurugenzi yeyote katika hiyo kampuni haruhusiwi kufungua kesi kwa niaba ya kampuni. Anaweza kufungua kesi kama yeye binafsi kwa kutumia jina lake lakini si kwa niaba ya kampuni na kwa kutumia jina la kampuni.

Kwa mfano kampuni inaitwa MECCO CO. LTD. Hawezi kufungua kesi kwamba MECCO CO. LTD inamshitaki fulani yaani MECCO CO. LTD vs SHABAN. Hataruhusiwa kutumia jina la kampuni namna hiyo. Hii ni hata kama kampuni imetendewa kosa fulani ambalo kampuni ni lazima ishitaki. Bado hataruhusiwa kufanya hivyo. Na hii ni kwa maafisa wote wa kampuni wakiwemo wanahisa,mameneja, katibu wa kampuni(company secretary), mwanasheria wa kampuni na afisa yeyote yule wa kampuni.

Kitu pekee chenye mamlaka ya kushitaki kwa niaba ya kampuni na kwa kutumia jina la kampuni ni maamuzi ya bodi ya kampuni(Board Resolution). Maamuzi haya ya bodi hufanywa na wakurugenzi wa kampuni kwa niaba ya kampuni na baada ya kupata ridhaa ya wanahisa.

Kama hakuna maamuzi ya jumla ya bodi ya wakurugenzi ya kampuni (Board Resolution)  ya kuamua kampuni kushitaki basi mkurugenzi yeyote, ama mwanahisa, ama afisa yeyote wa kampuni hawezi hata kidogo kushitaki kwa niaba, na kwa jina la kampuni.

Katika maamuzi ya mahakama kuu yaliyotolewa na Jaji Maghimbi tarehe 6/3/2020 katika kesi ya ardhi No. 147/2018 kati ya Evarist Steven Swai na Msafiri Enterpises Co. Ltd  vs The Registered Trustee of Chama cha Mapinduzi na wengine wawili, mahakama kuu imeifuta kesi iliyofunguliwa na mkurugenzi wa kampuni kwa niaba ya kampuni kwasababu ya kutokuwa na Maamuzi ya jumla ya bodi ya wakurugenzi(Body Resolution).

Mahakama imesema kuwa,hata kama kampuni husika inaonekana kuwa ni ya familia, na kuwa mkurugenzi aliyefungua kwa niaba ya kampuni kuonekana ndiye pia mwenye hisa kubwa katika kampuni hiyo kuliko wote, bado hana mamlaka ya kufungua kesi kwa niaba na kwa kutumia jina la kampuni kama hana Maamuzi ya jumla ya Bodi ya Kampuni(Body Resolution).

Mahakama imesisitiza kuwa alitakiwa kwanza aitishe kikao cha wakurugenzi, wakae na watoe maamuzi kwa kuandaa nyaraka ya maamuzi ya bodi ya wakurugenzi(Body Resolution) ambayo itakua inampa mamlaka, na kuridhia kampuni kushitaki. Kinyume cha hivyo ni kosa ambalo adhabu yake ni kesi kufutwa,kulipa gharama, ama vinginevyo.

Katika uamuzi huu mahakama haikuwa inatoa uamuzi mpya  bali maamuzi ya namna hii ndio msimamo wa mahakama na sheria kwa mda mrefu  na hapa ilikuwa ikisisitiza tu msimamo wake.

Sababu za kutoruhusu kila mkurugenzi,ama mwanahisa, ama afisa mwingine kushitaki kwa niaba ya kampuni bila Maamuzi ya bodi, ni kuondoa uwezekano wa kila mmoja kutumia jina la kampuni kushitaki jambo ambalo linaweza kuitia hasara kampuni, lakini pia kuepuka kutumia jina la kampuni vibaya,kuepusha kuiingiza kampuni kwenye migogoro isiyoisha nk.

Kwa wenye makampuni ambao wanahitaji kushitaki kwa kutumia majina ya kampuni,hasa makampuni madogo ya wajasiriamali ambayo pengine kwao hili ni geni, yawapasa wakae kikao cha wakurugenzi, wapitishe maamuzi ya jumla(Body Resolution) ya kuruhusu kampuni kushitaki, na maamuzi hayo yawe katika maandishi/nyaraka maalum iitwayo,”COMPANY/DIRECTORS BODY RESOLUTION”.

Nyaraka hiyo ni lazima iambatanishwe kwenye mashtaka(Plaint) ili wakati kesi inafunguliwa iwe ushahidi kuwa maamuzi ya kampuni kushitaki yalipitia hatua hii muhimu kisheria.  Basi tufanye hivyo.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

 

0 comments:

Post a Comment