Monday 10 August 2020

MNAPOUZIWA KIWANJA KIMOJA WATU WAWILI, NANI ANAKUWA MMILIKI HALALI ?.

 

MBUNGE WA MVOMERO AMOS MAKALLA ATEMBELEA ENEO LA MGOGORO WA ARDHI KINYENZE


NA  BASHIR  YAKUB - 

Mtu mmoja anadai yeye amenunua kiwanja, na mwingine naye anadai amenunua kiwanja hichohicho. Na wote hawa wawili kila mmoja anadai kuwa ameuziwa kiwanja na mtu huyohuyo mmoja, na wote wana nyaraka za mauziano zenye jina na sahihi za huyohuyo muuzaji.

Maelezo yote katika makala haya yatakuwa yanarejea misingi ya sheria katika maamuzi ya mahakama kuu katika kesi ya JOVENT CLAVERY RUSHAKA NA DEVOTA YIPYANA MPONZI  dhidi ya BIBIANA CHACHA,Land Case No. 303/2016. Makala haya yanahusu pia nyuma na mashamba.

1.NANI MNUNUZI HALALI KATI YA WAWILI.

Ni hivi, pale ambapo watu wawili wameuziwa kiwanja kimoja kutoka kwa mtu mmoja basi mmiliki halali anakuwa yule aliyenunua wa kwanza. Suala la msingi iwe tu kuwa yule aliyenunua wa kwanza awe alinunua kwa kufuata utaratibu wa kisheria.

Ikithibika kuwa mnunuzi wa kwanza ana ushahidi wa kununua kwa kufuata utaratibu wa kisheria basi yeye ndiye anakuwa mmiliki halali. Na hapa hata kama baada yake kuna wanunuzi wengine kumi, bado yeye atabaki kuwa mnunuzi halali na mmiliki halali.

Kwa msingi huu, wale waliomfuatia katika kununua watakuwa si wanunuzi halali na hawatakiwi kudai umiliki wa kiwanja hicho. Ni muhimu kueleza hili kwa uwazi ili watu waelewe na waache kuwa wanagombana.

2. KWANINI MNUNUZI WA PILI HAWI HALALI.

Mnunuzi wa pili au mwingine yeyote anayemfuatia hawi halali kwasababu hadhi ya umiliki(good title) aliyokuwa nayo muuzaji anakuwa ameishaipoteza kwa kumuuzia yule wa kwanza. Kawaida unapokuwa na mali unakuwa na hadhi ya umiliki(good title), hadhi ambayo unaweza ukaitoa kwa kuiuza, kuitoa zawadi, au kuirithisha. Hadhi hiyo ukishaitoa kwa njia yoyote kati ya nilizosema hapa kwa mtu mwingine unakuwa umebakiwa huna kitu. Maana yake ukiitoa kwa njia ya kuuza,huna kitu tena cha kuuza baadae, labda kiwe kingine na sio kilekile. Kwahiyo akija mtu wa pili naye ukamuuzia kitu hichohicho maana yake umemuuzia kitu ambacho huna, na wewe mnunuzi wa pili umenunua kitu kutoka kwa mtu ambaye hana. Tafsiri rahisi anakuwa amekuuzia hewa.

3. NAMNA YA KUTAMBUA MNUNUZI WA KWANZA.

Namna pekee ya kujua nani mnunuzi wa kwanza na ni aliyefuatia ni kwa kila mmoja kuonesha mkataba wake wa mauziano na kutizama tarehe. Tarehe iliyotangulia ndiyo ya mnunuzi wa kwanza na tarehe zinazofuatia ni za wanunuzi wengine waliofuata.

Mashahidi walioshudhudia nao ni muhimu kuthibitisha hili. Lakini hawa ili wathibitishe ni lazima kuwe na mkataba wa mauziano. Hii ni kwasababu sheria inakataza kununua ardhi bila maandishi. Ardhi ikinunuliwa bila maandishi ni sawa na kusema haijanunuliwa. Kwa hiyo mashahidi watakuja kuthibitisha tarehe iliyo katika maandishi.  Hivi ndivyo tunavyojua nani aliyetangulia kununua.

4.  NINI AFANYE MNUNUZI WA PILI.

Haki aliyonayo mnunuzi wa pili au mwingine yeyote aliyefuatia ni  haki za aina mbili. Kwanza ni haki ya madai ya pesa yake ya manunuzi kwa ukamilifu pamoja na fidia kutoka kwa muuzaji aliyeuza mara mbili. Hili anaweza kulidai kawaida au akaitumia mahakama  na atapata haki hiyo.

Haki ya pili ni kumfungulia jinai ya utapeli mtu huyohuyo aliyeuza mara mbili. Hapa muuzaji anaweza kukabiliwa na adhabu ya kifungo, faini, pamoja na fidia.  Aidha aliyeuziwa mara ya pili anaweza kuamua kuchukua hatua hizi zote mbili kwa pamoja, yaani akamfungulia madai akidai kurudishiwa hela yake pamoja na fidia, na wakati huo huo akamfikisha polisi kwa ajili ya kesi nyingine ya jinai kwa ajili ya adhabu ya kifungo nk. Kwahiyo atachagua kuchukua mojawapo au zote mbili kwa pamoja.

Pamoja na hayo, kama inawezekana kufanya mazungungumzo na huyo muuzaji kurudisha hela yako pamoja na fidia za usunbufu basi ni bora zaidi. Na wakati mwingine aliyetapeliwa anaweza kufidiwa kwa kupewa kiwanja kingine ikiwa ataridhika nacho.

5. HALI IKOJE KAMA MNUNUZI WA PILI AMESHATAFUTA HATI MILIKI KWA JINA LAKE.

Mfano nyote mliuziwa kiwanja ambacho hakijapimwa, lakini  yule mnunuzi wa pili tayari akajiwahi na kutafuta hatimiliki, na yule mmiliki wa kwanza akabaki tu na mkataba wa mauziano. Na tunajua pengine hatimiliki ina hadhi kubwa kuliko mkataba wa mauziano.

Hali hii haibadilishi msimamo wa sheria katika hili. Bado mnunuzi wa kwanza mwenye mkataba wa mauziano anaendelea kuwa mmiliki halali dhidi ya mnunuzi wa pili mwenye hati miliki. Kwa maana hiyo hatimiiliki yake haimsaidii chochote katika hili.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

                                            

 

 


0 comments:

Post a Comment