Monday 10 August 2020

KUIOMBA MAHAKAMA KUTEMBELEA ENEO LA MGOGORO.

 

WAZO HURU: SERIKALI KUUPATIA MUAROBAINI MGOGORO WA ENEO LA ITUHA JIJINI  MBEYA-WAZIRI HASUNGA

NA  BASHIR  YAKUB - 

Ni muhimu ukiwa na kesi ya ardhi ambayo kwa maoni yako unahisi mahakama haiwezi kutoa haki inavyostahili bila kulitembelea na kulijua eneo la mgogoro(Locus in Quo) kuiomba itembelee. Sheria iko wazi na inakuruhusu wewe kuiomba mahakama kutembelea eneo la mgogoro ili kushuhudia hicho unachotaka iamini. Na hii haijalishi upo pande gani wa kesi, uwe mlalamikaji ama mlalamikiwa kila upande unayo haki ya kuomba kutembelea eneo la mgogoro.

Hatua hii ni muhimu sana kwasababu itatoa picha na mwanga wa kile ambacho unakiongelea. Itatoa taswira na ushahidi wa dhahiri. Wakati mwingine waweza kushindwa kueleza jambo vizuri  pengine kutokana na jiografia ya eneo lenyewe, kwakuwa si rahisi kuelezeka ama sababu nyinginezo. Lakini kwa mahakama kufika na kuona mazingira, basi kila kitu kitajieleza chenyewe.

Hata hivyo, huwezi kuomba mahakama itembelee eneo la mgogoro kama kesi ipo hatua ya rufaa. Hii ni kwasababu hatua ya rufaa ni hatua ambayo sheria hairuhusu ushahidi mpya kutolewa. Kwahiyo kama unahitaji kuomba jambo hili ni vema uliombe mapema kabisa kule kesi ilipoanzia.

Kwa mahakama za ardhi kesi inaweza kuwa imeanzia baraza la ardhi la kata, au imeanzia baraza la ardhi la wilaya, au imeanzia mahakama kuu. Popote itakapokuwa imeanzia unayo haki ya kuomba mahakama itembelee eneo la mgogoro ili iweze kujiridhisha katika kile unachosema.

Aidha, sio migogoro yote ya ardhi inahitaji kutembelewa na mahakama. Mgogoro kama umenyooka una ushahidi na mashahidi wa kuweza kuthibitisha na kila jambo likaeleweka, basi hamna haja ya kuomba kutembelea. Lakini ikiwa kwa mtazamo wako unaona kuna jambo hata likielezwa haliwezi kueleweka mpaka mahakama ifike na kuona basi utaomba.

Unapoomba mahakama nayo itapima na kuona iwapo kuna umuhimu wa kufanya hivyo ama hapana, bali kila kitu kinaweza kuishia ndani ya mahakama. Katika kutoa uamuzi wa kutembelea ama hapana mahakama itaongozwa na misingi ya sheria iliyowekwa ikiwemo ile iliyoelezwa katika kesi ya Evelyn Even Gardens NIC LTD and the Hon.Minister , Federal Capital Territory and Two Others, No.FCT/HC/CV/1036/2014;Motion No. FCT/HC/CV/M/5468/2017 .

 

Misingi ni pamoja na;-  Kama kutembelea eneo kutawezesha kuondoa mashaka juu ya kinachobishaniwa, Kama mgogoro unahitaji utambuzi wa mipaka, majirani na ukubwa au kiwango cha eneo,na  Kama ubishi unahusu hali halisi ya eneo, na jingine lolote ambalo mahakama itapima na kuona linafaa kuisukuma itembelee.

Misingi hii pia imeelezwa katika kesi ya MARTIN MGANDO vs MICHAEL .F. MAYANGA , Rufaa Namba 93/2019, chini ya Jaji Bahati.

Nisisitize tu kwamba mahakama inaweza kuamua yenyewe(sua moto) kutembelea eneo la mgogoro bila kuombwa na mtu yeyote. Hata hivyo ni muhimu wewe uliye kwenye kesi mlalamikaji ama mlalamikiwa kuwa wa kwanza kulianzisha hili ikiwa unaona ni la muhimu. Hii ni kwasababu wewe ndiyo mwenyue kesi ambapo matokeo mabaya ama mazuri yanakuja kwako. Kwa leo yatutoshe haya.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.  0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com

 

0 comments:

Post a Comment