Friday 29 November 2019

KUZUIA MALI ZA NDOA KUUZWA WAKATI KESI IKIENDELEA.


Tokeo la picha la MALI ZAGOMBEWA


NA BASHIR  YAKUB -

Unakuta umefungua shauri la ndoa, inaweza kuwa maombi ya talaka,mgawanyo wa mali ,malezi ya watoto au vyote. Wakati huo ambapo kesi haijaanza, au imeanza lakini haijaisha, unahisi au umeona mali za ndoa ambazo pengine zinatakiwa kugawanywa  zikiwa katika hatari ya kuuzwa, kugawiwa,kuharibiwa,au kubadilishwa umiliki. Unaona kabisa shauri likija kuisha patakuwa hamna kitu au kitakuwepo kidogo. Nini ufanye kisheria katika mazingira kama haya ili kuokoa mali hizi, ili usije kukosa haki yako kesi ikiisha. Hiki ndicho kitakachozungumzwa hapa.

Kitu unachotakiwa kufanya  kimeelezwa katika kifungu cha 138( 1 ) cha Sheria ya Ndoa. Kifungu kinasema pale ambapo mtu ataona kuna hatari ya mali kuuzwa,kuharibiwa  au kupotezwa kwa namna yoyote ile basi atakuwa na haki ya kuomba mahakama itoe zuio la muda kumzuia mtu yeyote kuuza,kubadili umiliki,kuharibu,kutoa zawadi au kufanya kitu kingine chochote chenye lengo la kuathiri mali hizo.

Kitu hiki pia kimeelezwa mara nyingi na mahakama kuu pamoja na mahakama ya rufaa katika kesi mbalimbali mojawapo ikiwa ni hii ya ELIZABETH GIKENE vs JOHN ZAKHARIA GIKENE shauri la ndoa namba 5/2004.

Kwahiyo utakachofanya,kwanza kama shauri liko mahakama ya wilaya, ya hakimu mkazi, au mahakama kuu na unaye Wakili anayekuwakilisha basi mwambie kuhusu huo wasiwasi wako wa dalili za kupotezwa kwa mali lakini pia muombe mfanye utaratibu wa zuio hili. Bila shaka mtakubaliana kuhusu hilo.

Pili,kama shauri liko katika mahakama nilizotaja hapo juu lakini hauna Wakili anayekuwakilisha basi ni muhimu kumtafuta wakili yeyote umweleze wasiwasi wako na umuombe akuandalie maombi ya zuio hili ili uzuie mali wakati shauri la msingi likisubiriwa kuisha. Mtaelewana kuhusu hili na mtafanya kama mlivyoelewana. Maombi haya ni lazima umtafute Wakili hata wa kukuandikia tu halafu wewe ukaenda mwenyewe mahakamani, kwasababu mtu ambaye sio Wakili sio rahisi kuandaa maombi haya.

Zaidi, kama kesi iko mahakama ya mwanzo hapa huna haja ya wakili wala kuandaliwa maombi rasmi bali utamueleza hakimu anayesikiliza shauri lako kwa mdomo kuhusu  wasiwasi wako wa mali kuharibiwa na utamuomba atoe zuio la muda mali zisiguswe mpaka shauri la msingi liishe. Kama utaweza unaweza kumtajia hata kifungu cha sheria  nilichotaja hapa juu pamoja na hiyo kesi niliyoweka ambavyo kwa pamoja vinaruhusu maombi haya ya zuio. Kama utashindwa basi mwambie tu bila kumtajia kifungu, atatoa msaada.

Mara nyingi tatizo hili la kuharibiwa mali wakati shauri likiendelea limekuwa likiwakumba zaidi wakina mama. Anapofungua shauri kuomba talaka au mgawanyo wa mali  basi mwanaume huanza kuuza baadhi ya mali au kuzibadilisha umiliki ili wakati shauri linaisha mali ziwe zimeisha ili mwanamke asiambulie kitu, au kwa lengo kuwa ikifikia ushahidi kila mali itakayotajwa na mwanamke kuwa ni ya ndoa akatae kuwa sio yake au ilishauzwa.

Hata wanaume nao hukumbwa na tatizo hili lakini zaidi ni wanawake. Basi hili lisikupe tabu tena kwakuwa dawa yake ndiyo hii. Na kwa taarifa mali ikizuiwa na mahakama isiuzwe na mtu akaendelea na uuzaji au kuiharibu basi adhabu yake ni kifungo miezi sita jela kwa kuidharau mahakama, lakini pia yule aliyenunua anakuwa amepoteza hela yake kwakuwa amenunua mali ambayo imezuiwa na mahakama na hivyo batili.  Basi tuchukue hatua.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA YA SHERIA KUPITIA GAZETI  LA JAMHURI KILA JUMANNE.   0784482959, 0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment