Tuesday 4 December 2018

WAKRISTO MSIFUNGUE MIRATHI ZENU MAHAKAMA ZA MWANZO, HAIRUHUSIWI.


Image result for WAKRISTO

NA  BASHIR  YAKUB -

Nimeona mara nyingi ambapo marehemu alikuwa mkristo halafu warithi wake, au ndugu, jamaa wanaamua kufungua mirathi katika mahakama za mwanzo. Yatupasa kujua kuwa, pale ambapo marehemu alikuwa mkristo hairuhusiwi kisheria kufungua mirathi yake katika mahakama yoyote ya mwanzo. Iwe ya mjini au kijijini, madhali ni mahakama ya mwanzo basi inakosa mamlaka ya kimirathi kwa marehemu mkristo.
Na hili ni katika namna zote, yaani pale marehemu anapokuwa ameacha wosia au hajaacha. Madhali tu alikuwa ni mkristo basi usifungue mahakama ya mwanzo. 

Mahakama za mwanzo ni zile ambazo zipo kila kata vijijini au mijini, na ni rahisi tu kuzijua kwani hata ukiuliza utaambiwa, na nyingine zina mabango kabisa “MAHAKAMA YA MWANZO YA..........”

Kwenye masuala ya mirathi tunazo sheria za aina mbili, zile za kiutaratibu (procedures), na zile zinazoelekeza mgawanyo wa mali yaani nani apate nini(substantive laws). Hizi zinazoelekeza nani apate nini nazo ziko aina kuu tatu. Na kila sheria katika hizi tatu inasimamia kundi lake. Kundi linalosimamiwa na sheria moja haliwezi kutumia sheria ya kundi jingine. Na kila sheria ni tofauti na nyingine katika namna ya kugawa mali. 

Ya kwanza katika hizi tatu ni sheria iitwayo Sheria ya Urithi ya India ya Mwaka 1865(The Indian Succession Act), ya pili ni sheria iitwayo Sheria ya Amri za Mila ya Mwaka 1963(The Customary Law(Declaration)Order, na ya tatu ni Sheria ya Kiislam ambayo ni Qur-an na Hadith/Sunnah.

Sheria ya Urithi ya India ni maalum kwa ajili  ya Wakristo,wakati Sheria ya Amri za Kimila ni maalum kwa watu wa mila ambao sio waislam wala wakristo, na Sheria ya Kiislam ni maalum kwa ajli ya Waislam. Kwahiyo kisheria unatakiwa kuandaa mirathi yako kutokana na sheria yako. Na mirathi inaanza tangu unapoandaa wosia na kuishia pale usimamizi au mali za marehemu zinapogawanywa.  

Hivyo kama ni wosia uwe na sifa zinazokubalika katika sheria ya kundi lako, na usijiandikie tu kwani itakuwa kinyume na sheria na itabatilishwa. Kadhalika kwa wale wanaofungua mirathi wafungue mahakama ambayo imekubaliwa katika sheria ya kundi lao, na usifungue tu unavyojisikia.

Pia nilitaja Sheria za  kiutaratibu(procedures)  ambazo baadhi  ni Sheria ya Mahakama za Mahakimu(The Magistrate Court Act), na Sheria  ya Mirathi sura ya 352,(PAEA).
Kuhusu wakristo kutofungua mirathi yao mahakama za mwanzo ni kuwa, Jedwali la 15 kipengele cha 1(i) cha Sheria ya Mahakama za Mahakimu kinasema kuwa mahakama ya mwanzo itakuwa na mamlaka katika masuala ya mirathi iwapo sheria inayotumika katika mirathi hiyo ni sheria ya kiislamu au Sheria ya Mila. Kwa maana ya kifungu hiki ni kuwa mahakama ya mwanzo inatumika katika mirathi ambayo marehemu alikuwa muislam ama marehemu alikuwa mtu aliyeishi kimila. Marehemu aliyekuwa mkristo mahakama hii haiwezi kutumika.

Aidha, mahakama inayotumika kwa marehemu mkristo ni Mahakama  Kasimu ya Wilaya(district delegate) kwa mujibu wa kifungu cha  5 cha Sheria ya Mirathi sura ya 352. Mahakama  Kasimu ya Wilaya utaipata popote ilipo mahakama ya wilaya ya kawaida. Ni vyema ukafika hapo ukasema nataka kufungua mirathi utaelekezwa utaratibu au uwasiliane na mawakili.

Kadhalika makundi yote ya waislamu,wakristo na watu wa mila wanaruhusiwa kuitumia mahakama kuu kwa shughuli za mirathi kwa mujibu wa kifungu cha 3 cha Sheria ya Mirathi Sura ya 352 kwakuwa ina mamlaka ya jumla.

Basi ni muhimu kwetu kuyazingatia haya ili kuweza  kusimamia mirathi kwa uhalali. Msimamizi wa mirathi anakosa uhalali na anahesabika si msimamizi wa mirathi, na kama amegawa mali ugawaji unakuwa haramu iwapo  hakufuata utaratibu wa sheria.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment