Thursday 8 November 2018

NAMNA YA KUZUIA UKAZAJI/UTEKELEZAJI WA HUKUMU.



Image result for KUKAZA HUKUMU

NA  BASHIR  YAKUB -

1.UKAZAJI WA HUKUMU NI NINI.

Ukazaji wa hukumu ni hatua inayochukuliwa na mtu aliyeshinda kesi/shauri kwa kuiomba mahakama kumlazimisha mtu aliyeshindwa katika kesi/shauri kufanya au kutekeleza kile ilichoamua dhidi yake/mshindwa. Kawaida mtu akishindwa kesi/shauri mahakama huwa inatoa maagizo mbalimbali. Mathalan, agizo la kulipa hela, agizo la kurudisha nyumba au mali fulani, agizo la kubomoa, agizo la kuondoka katika pango au katika nyumba,kiwanja fulani, agizo la kujenga, agizo la kulipa fidia, faini, gharama n.k. Maagizo  yako ya aina nyingi inategemea na shauri na shauri.

Hivyo basi, ukazaji hukumu/utekelezaji huwa ni kulazimisha agizo aumaagizo  ya aina tuliyoona hapo juu yaweze kutekelezwa kama ilivyoamriwa.

2.  NI WAKATI GANI HUKUMU HUTAKIWA KUKAZWA.

Kwa ujumla mahakama inapotoa hukumu basi yule aliyeshindwa mara moja au ndani ya muda aliopewa kama amepewa,hutakiwa kutekeleza kile kilichoamuliwa kwa hiari yake. Aliyeshindwa akikataa kutekeleza kile kilichoamuliwa kwa hiari yake basi ni wakati huu ambapo  suala la kukaza/kutekeleza hukumu kwa njia mahakama huja. 

Kwa maana nyingine mtu aliyeshndwa akiamua kwa hiari yake kufanya yale aliyoagizwa na mahakama basi suala ukazaji wa hukumu haliwezi kuwepo.

3. UMUHIMU WA  KUZUIA HUKUMU KUKAZWA.

Sababu za msingi zinazoweza kupelekea kuzuia hukumu kukazwa ni pamoja na sababu kuwa umekata rufaa na hivyo ukazaji wa hukumu usimame ili rufaa yako isikilizwe kwanza, sababu nyingine ni iwapo kesi imeendeshwa bila wewe kujua au kuwepo isipokuwa umeshtukia tu watu wanakuja kukaza hukumu, sababu nyingine ni iwapo una maslahi  katika mali inayokaziwa hukumu kwa mfano ni mali ya ndoa na hukuwa na taarifa na kilichoendelea,  ni mali yako lakini inataka kuuzwa au kutumika kutekeleza hukumu kwa kesi ambayo sio yako na pengine hukuwahi kujua uwepo wake, nk.

4. KUZUIA  UKAZAJI  WA  HUKUMU.

Ukazaji wa hukumu unazuiwa kwa njia ya mhusika kupeleka maombi ya faragha(chamber application) mahakamani. Mleta maombi/mlalamikaji  atakuwa yule anayezuia ukazaji wa hukumu na mjibu maombi/mlalamikiwa  atakuwa yule anayekaza hukumu. Kadhalika ataunganishwa dalali wa mahakama(court brocker) aliyeteuliwa kukaza hukumu kama yupo, na wengine ambao watakuwa ni muhimu kuunganishwa ili kutekeleza azma.

Maombi ya kuzuia ukazaji wa hukumu yatafunguliwa katika mahakama ambayo imetoa hukumu husika. Pia maombi haya yanaweza kupelekwa chini ya hati ya dharula ikiwa utekelezaji wa hukumu umeshaanza au ikiwa unaona kuwa uchelewaji wowote unaweza kupelekea utekelezaji kufanyika kabla hata maombi yako ya kuzuia hayajasikilizwa na hivyo kukusababishia hasara na usumbufu. Hati ya dharula husaidia maombi kusikilizwa haraka kuliko ilivyo kawaida.

Maombi ya kuzuia ukazaji au utekelezaji wa hukumu yataambatana na kiapo cha muombaji yakieleza sababu za msingi na za kisheria za kwanini hukumu isitekelezwe. Na watu wa aina mbili wanaweza kufungua maombi haya. Kwanza mhusika kwenye hukumu hasa yule aliyeshindwa, na pili mtu yeyote mwenye maslahi katika mali inayotaka kutumika  kutekeleza hukumu ambaye  alikuwa mhusika katika shauri lililoisha au hakuwa mhusika, na pia kuwepo sababu za msingi kuwa si halali mali hiyo kutumika kutekeleza hukumu.

Maombi haya yakishapokelewa mahakamani yatapangiwa hakimu au jaji wa kuyasikiliza. Na baada ya kusikilizwa inaweza kuamuliwa kuwa utekelezaji/ukazaji wa hukumu usitishwe kwa muda kupisha rufaa au vinginevyo, au kuwa sio halali kutumia mali hii kukazia hukumu na hivyo kuiondoa mali iliyokuwa inatakiwa kutumika kukaza hukumu katika mchakato huo.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment