Tuesday 9 October 2018

UNAHITAJI KUPIMIWA ARDHI ?, UTARATIBU NI HUU

Image result for KUPIMA ARDHI



NA  BASHIR YAKUB -

Ardhi iwe kiwanja au nyumba thamani yake hupanda pale inapokuwa imepimwa. Kupima ardhi ni kurasimisha ardhi. Faida nyingi hupatikana baada ya ardhi kuwa imerasimishwa. Baadhi ya faida ni kuwa ardhi hupanda thamani yake, kuweza kupata mkopo kwa urahisi, ardhi kutumika kama dhamana mahakamani, lakini kubwa ni kuwa na amani na uhakika wa ardhi yako kuwa eneo ulilopo linaruhusiwa  kisheria, sio eneo hatarishi, sio eneo la miradi ya serikali, sio hifadhi ya barabara au barabara nk. 

Unakuwa  na amani kuwa uko sehemu sahihi na salama.
Kupima ardhi ni hatua inayopitiwa pale unapoelekea kupata hati. Kila ardhi yenye hati imepimwa lakini  si kila ardhi iliyopimwa ina hati.

UTRATIBU WA KUPIMIWA ARDHI.

1.Kuandika barua ya maombi ni hatua ya kwanza ambapo utatakiwa kumwandikia mkurugenzi wa halmashauri ukiomba kupimiwa eneo lako. Hii ni barua ya kawaida ya kiofisi isipokuwa ieleze majina yako kwa ukamilifu na ichambue anuani ya eneo ambalo linalotakiwa kupimwa kwa ukamilifu.Mkurugenzi unayetakiwa kumwandikia ni yule wa halmashauri ambamo ardhi inayotakiwa kupimwa imo. Kwa mfano kama ardhi  iko wilaya ya kinondoni basi mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya atakayeandikiwa barua.

Barua hiyo itaambatanishwa na nyaraka za umiliki wa  eneo husika. Mara nyingi nyaraka hapa huwa ni ile mikataba ya mauziano.  Kadhalika, barua yako inatakiwa kupitishwa  serikali za mitaa na kwa mtendaji kata.

2. Barua itakapokuwa imekidhi vigeo basi itapokelewa kwa mkurugenzi na hapo mkurugenzi  ataiwasilisha idara ya ardhi. Baruayako ya maombi itakabidhiwa kwa afisa ardhi ambaye kazi yake kubwa itakuwa ni kuthibitisha na kujiridhisha na umiliki wa ardhi ya mwombaji.

3. Baada ya kujiridhisha, afisa ardhi ataandaa  na kujaza fomu namba SF 47 na kuiwasilisha kwa afisa mipango miji.

4. Fomu na nyaraka vikishafika kwa afisa mipango miji kazi yake kubwa ni kutizama iwapo eneo linaloombwa kupimwa lina mchoro wa mipangomiji. Kama mchoro upo basi kazi nyingine ya afisa mipango miji ni kusoma mchoro ule kuangalia kama eneo limepangiwa sawa na kile unachoomba. Unaweza kuwa unaomba kwa ajili ya makazi kumbe eneo lilishapangiwa viwanda tangu miaka ya huko nyuma pengine hata kabla hujazaliwa. 

 Maeneo yote yenye michoro huwa yamepangwa  kwa ajili ya shughuli fulani mf, maeneo ya makaburi, makazi, viwanda, maeneo hatarishi, dampo, miradi mbalimbali ya serikali, viwanja vya wazi au vya michezo nk.

5. Afisa mipango miji akithibitisha kuwa maombi yako yanaendana na mchoro husika  basi atairudisha ile fomu na SF 47 kwa afisa ardhi ikiwa na mapendekezo ya maombi yako. Hapo afisa ardhi atajaza fomu SF 37  ambayo ndiyo maombi rasmi ya kuomba  kupimiwa  akiambatanisha na ushahidi wa mchoro wa mipango miji unaoonesha eneo husika na vitawasilshwa  kitengo cha upimaji.

6. Hapo upimaji atateuliwa afisa upimaji ambaye utaambatana naye mpaka eneo husika kwa ajili ya upimaji . Baada ya hayo, ardhi yako itapimwa na hapo utaratibu wa kupimiwa utakuwa umekamilika na hivyo kufungua mlango kwa hatua nyingine kufuata.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment