Saturday 29 September 2018

HUKUMU KESI YA MV. BUKOBA NA MAFUNZO KWETU LEO TUNAPOOMBOLEZA.



Image result for mv bukoba
NA  BASHIR  YAKUB -

( A ).NAMBA YA KESI.

Kesi ya Jinai Na. 22/1998, Mahakama kuu Mwanza , Mbele ya Jaji  Mlay.

( B ) WASHITAKIWA.

1.     Kapteni Jumanne Rume Mweiru. Huyu ndiye alikuwa Kapteni siku ya tukio, akiendesha toka Bukoba VIA  kemondo Bay  hadi  Mwanza.

2.     Gilbert Mokiwa. Huyu alikuwa mkaguzi wa meli, na ndiye alikuwa na wajibu wa kuikagua MV Bukoba.

3.     Alphonce Sambo. Huyu alikuwa afisa bandari Bukoba, na wakati meli inaanza safari yeye na wenzake waliratibu safari.

4.     Prosper Rugumila.Huyu alikuwa afisa bandari kemondo ambapo MV Bukoba ilipitia ikitokea bandari ya Bukoba na kuongeza abiria na mizigo.

( C ) KOSA WALILOSHITAKIWA NALO.

Kuua  bila kukusudia kinyume na kifungu cha 195 cha Kanuni za Adhabu, Sura ya 16 ya Sheria za Tanzania.

( D ) MAELEZO YA KOSA.

Kuwa, tarehe 21 / 5 / 1996 majira ya saa 7 :30 asubuhi, eneo la ziwa Victoria Mwanza washitakiwa kwa uzembe walisababisha meli ya MV BUKOBA  iliyokuwa ikitokea Bukoba kuelekea Mwanza kupinduka na kuzama ,na hivyo kusababisha vifo vya watu 159.

( E ) MASHAHIDI UPANDE WA MASHTAKA.           

Upande wa mashitaka ulileta mashahidi 32  wakiwemo ;

1.     Kapteni Cleophas Magoge . Huyu saa 8 : 15 asubuhi,aliitoa MV VICTORIA bandarini Mwanza ilipokuwa inaendelea na matengenezo na kulazimika kuiendesha  kuelekea kwenye eneo la ajali baada ya kuambiwa kuwa MV BUKOBA imezama.

Anasema alipofika eneo la tukio aliiona MV Bukoba ikiwa kichwa chini miguu juu, huku mizigo hasa ndizi,watu, na miili mingi ikielea majini. Na aliposogea karibu alimuona Kapteni wa MV Bukoba  mshitakiwa wa kwanza akiwa ananing’inia juu ya meli iliyozama.

2.     Shahidi mwingine ni Kapteni Mannase Ephraim Kombo. Huyu anasema siku ya tukio alikuwa akiendesha MV BUTIAMA kutoka Port Bell Uganda kuelekea Mwanza. Anasema saa 6 :00 za asubuhi aliingia kwenye radio na kuwasiliana na bandari ya Mwanza kuwa atafika saa 9 : 00 asubuhi.

Anasema wakati akiwasiliana alisikia Kapteni wa MV Bukoba naye akiwasiliana kuwa atafika mwanza saa 8 :00 asubuhi. Anasema alifika bandari ya Mwanza saa 9:00am akashusha mizigo lakini MV Bukoba iliyosema kufika saa 8:00am haikuwa imefika.

Anasema, baadae alimsikia MPANGALA aliyekuwa muongoza meli siku hiyo akiiita MV Bukoba  kwenye radio bila majibu. Anasema MPANGALA aliita sana mpaka akaamua kutoka nje kutizama, na kwa mbali saana aliona kitu ambacho hakukielewa. Alirudi ndani na kuchukua hadubini(binocular) kutizama tena, na hapohapo alimsikia akiongea kwa mshtuko kuwa MV Bukoba inazama.

Anasema maramoja aliamua kuiendesha MV BUTIAMA kuelekea eneo la tukio ambapo alikuta mitumbwi kadhaa ya wavuvi ikiokoa watu, na aliona maiti nyingi, watu hai, na mizigo vikielea.

3.     Shahidi mwingine ni meneja wa yard ya meli Mwanza. Anasema siku 29 kabla ya kuzama yaani april MV Bukoba ilikuwa  na matatizo ya kuyumba ambayo pia yalithibitishwa na mashahidi wengine. Anasema, mtaalam kutoka Ubelgiji ambao ndio waliotengeneza meli hiyo aliletwa  kuchunguza tatizo hilo na aliifanyia majaribio katika eneo liitwalo Karumo.
Mtaalam aligundua matatizo ya kuyumba na akasema watatoa ripoti mwezi wa 7 /1996, lakini meli ikazama mwezi 5/ 1996 miezi miwili kabla ripoti kutolewa.Anasema lakini baada ya majaribio hayo kuanzia tarehe 12 / 5 / 1996 meli ilifanya safari tatu, mbili Mwanza – Port bell Uganda , na moja Mwanza – Kisumu Kenya, na ya nne ndio ilikuwa ya mwisho ya Mwanza- Bukoba.

Anasema siku hiyo MV BUKOBA ilienda Bukoba lakini haikuwa imepangiwa kwenda huko, na badala yake MV VICTORIA ndiyo iliyokuwa imepangiwa kwenda Bukoba. Anasema MV Victoria ina uwezo wa kubeba abiria 1200, na tani za mizigo  250 wakati  MV BUKOBA  ina uwezo wa kubeba abiria 400, tani za mizigo 85.

Anasema kwahiyo tiketi za abiria na mizigo zilizoandaliwa huko Bukoba zilikuwa ni za MV Victoria  kwasababu ndiyo ilitakiwa kwenda. Kutokana na hitilafu za injini ikashindwa kwenda na ikabidi ibadilishwe na MV BUKOBA na hivyo MV Bukoba ikafanya kazi ya MV Victoria.

4.     Munaf Hussein Ibrahim Punja ni abiria aliyenusurika katika hiyo ajali. Anatoa ushahidi kuwa alipanda meli saa 9:00 pm bandari ya Bukoba na watu walikuwa wengi pamoja na mizigo. Anasema meli ilikuwa inakwenda upande. Anasema walipofika Kemondo saa 10 ;00 usiku alishangaa kuwaona David pamoja na Mutayoba ambao aliwaacha bandari ya Bukoba na hawakuwa wamepanda meli.

Anasema aliwauliza kulikoni, wakamwambia kuwa kule Bukoba bandarini walizuiwa kuingia kwenye meli kwasababu ilijaa kwahiyo wakaamua kuchukua Taxi kuja kuisubiria Kemondo Bay. Anasema hapo Kemondo walipanda na wakasafiri wote.

5.     Zabron Kasindirano naye ni abiria aliyenuurika. Anasema meli ilipofika Kemondo Bay alimuona shemeji yake  Francis Justusi Kaganji na kushangaa kwasababu walimuacha Bukoba.  Anasema alimuuliza amefikaje Kemondo akamwambiwa alipanda taxi baada ya kuzuiwa kupanda bandari ya Bukoba.

Anasema  saa 7 :00 asubuhi wakati wamekaribia kufika meli ilianza kuyumba sana. Anasema  alikuwa amekaa na wanawake akawaambia wapande juu kuchukua “life Jacket” lakini wakamcheka kuwa ni mwanaume muoga  na hivyo kwa hofu ya kutoonekana muoga naye hakuchukua tena Jacket.

Anasema haikupita dakika 10 tokea aambiwe muoga meli ikapinduka, akatupwa kwenye maji karibia na mkungu wa ndizi ambao aliushikilia mpaka akaokolewa, na kuwa wale wanawake hakuwaona tena.
Mashahidi walikuwa wengi ila  kwa kutaja ni wachache.

( F ) ILI  WATUHUMIWA WAPATIKANE NA HATIA YALITAKIWA KUTHIBITISHWA MAMBO YAFUATAYO.

1.     Kwamba meli ilikuwa na matatizo ya kiufundi(ya kuyumba) na wao hawakuyashughulikia/kuyajali  au kuzingatia matatizo hayo.

2.     Pili, waliijaza meli  watu kuzidi uwezo wake.

3.     Tatu, waliijaza meli mizigo kuzidi uwezo wake.

MATATIZO YA KIUFUNDI.

-         Hii ilishindwa kuthibitika kwasababu  kwanza hakukuwa na rekodi yoyote ya mafundi na wataalum akiwemo yule Mbelgiji,  iliyozuia meli kuendelea kufanya kazi. Hakukuwa na shaka kuwa meli ilikuwa na matatizo ya kuyumba ila haikuzuiwa kufanya kazi.

-          Pili, hakukuwa na ushahidi wa kisayansi ulioonesha kuwa  matatizo ya kuyumba ndiyo yaliyopelekea meli kuzama.

KUJAZA WATU KULIKO UWEZO.      

-         Hii nayo ilishindwa kuthibitika kwasababu hakukuwa na rekodi sahihi ya watu waliongia kwenye meli. Baadhi ya vitabu vinaonesha 400, vingine 700, vingine 759 nk.

-         Pia  idadi ya watu ilioneshwa kwa kuangalia tiketi zilizouzwa. Hakukuwa na ushahidi wa kuonesha waliongia ndani ya meli yaani waliosafiri walikuwa wangapi. Mashahidi nao wanathibitisha kuwa kununua tiketi sio kusafiri, unaweza kununua tiketi halafu usisafiri. Kwahiyo ni vigumu kupata idadi ya waliosafiri kwa kuhesabu tiketi zilizouzwa. 

-         Kitabu cha uhakiki wa wasafiri ambacho hutumiwa na wakaguzi ndani meli inapokuwa safarini  ndicho kinaweza kuthibitisha waliosafiri yaani waliokuwa ndani ya meli, na hivyo kujua kama ilizidisha au hapana. Hata hivyo kitabu hicho nacho kilizama, na hivyo kukosa ushahidi wa kujua mpaka meli inazama ilibeba  abiria wangapi, na hivyo kuweza kutambua kama walikuwa wamezidi ama hapana.Hii nayo ikafia hapo.

KUJAZA MIZIGO KUPITA UWEZO.

-         Hii nayo haikuweza kuthibitishwa. Hakuna rekodi Bukoba bandari kuwa zilipakiwa tani ngapi ,na hakuna rekodi Kemondo Bay ziliongezwa tani ngapi. Unawezaje kusema ilizidisha mizigo kwa ushahidi wa macho tu bila rekodi sahihi ya mizigo.Hii nayo ikafa.

( G ) HUKUMU.

-         Kama hakuna ushahidi kuwa ubovu wa meli ndio uliosababisha izame, kama hakuna ushahidi kuwa meli ilipakia abiria wengi kuliko uwezo wake, kama hakuna ushahidi kuwa meli ilipakia mizigo kuliko uwezo wake, nini kilichobakia zaidi ya kuwaachilia huru washitakiwa wote wanne.

-         Mahakama ikaona washitakiwa wote wanne hawana hatia ,  ikaamuru waachiliwe huru mara moja.

( H ) TUNAJIFUNZA NINI.

Ajali zote za majini, kuanzia hii ya MV Bukoba, Spice Islanders Zanzibar, mpaka sasa Mv nyerere, nk, hadithi ni moja tu, kuzidisha abiria na mizigo. Pamoja na hayo katika ajali zote hizi, hakuna mtu unayeweza kumsimamisha akwambie idadi halisi kabisa,ile yenyewe ya watu waliokuwemo na akakwambia. Huu ni ukweli. Hayupo, na narudia hayupo. Si mkata tiketi, si mkaguzi anayesafiri na meli, si kapteni, si ofisa  wa bandari, hakuna. Ndio maana utaona inatajwa idadi ya waliokufa leo, kesho wanasema mwili mwingine umegunduliwa na hivyo waliokufa idadi imeongezeka na kufikia kadhaa.

Hakuna mtu wa kukwambia waliosafiri ni 100, walionusurika ni 50, tuna maiti 30, na hivyo sasa hivi tunafuta maiti 20 TU tufunge zoezi. Hakuna wa kutoa takwimu kama hii. Ajali zikitokea tunakaa mwaroni tunasuburi chochote  ambacho kitatemwa na ziwa ndicho tunachobeba na kuongeza kwenye idadi. Ziwa lisipotema tunasema basi wameisha. Hatuwezi kusema kwenye idadi yetu anakosa maiti mmoja na ndiye tunamtafuta kwasasa, katu hatuwezi. Kweli dunia hii ya karne ya 21 hatuwezi hata kujihesabu hata kwa kutumia vidole na vijiti ?, Kweli. ?.

Mbona huku kwenye usafiri wa anga idadi iko wazi na inajulikana. Utaambiwa abiria waliosafiri,na sio waliokata tiketi, bali waliosafiri ni 257, watumishi wa ndege(crew) ni 10, na hivyo waliokuwemo jumla ni 267. Na inakuwa hivyohivyo  kweli hakuna kubabaisha.  Kwanini haiwi hivyo kwenye meli/vivuko. Leo  ni miaka 22 tangu MV Bukoba izame, nakuhakikishia hakuna wa kukwambia idadi halisi ya waliofariki katika ajali hiyo, hayupo. 

Leo ni miaka 7 tangu MV Spice Islanders izame, nakuhakikishia hakuna wa kukwambia idadi halisi ya waliofariki katika ajali hiyo, hayupo. Na leo nasema hakuna wa kukwambia idadi halisi kabisa ya waliofariki kwenye kivuko cha MV Nerere, hayupo. Na huu ndio ukweli.  Kadhalika katika meli zote hizo hakuna wa kukupa idadi ya tani halisi ya mizigo iliyokuwemo bila kubabaisha, hakuna.

Sasa unaweza kujiuliza tunakabiliwa na tatizo gani hasa, hatujui hesabu hizihizi  za kuhesabu 1-10 na.....,ni wazembe, ni wasiojali,ni wapuuzi, ni watu ambao bado tunaishi maisha ya ujima,ni watu wa aina gani hasa. Watu ambao ulaya, America na uchina wameanza kugawana maeneo mwezini ili wachimbe madini ya  PLAGIOCLASE  sisi hatuwezi hata kuhesabiana  kwa hesabu ya darasa la kwanza.Tuseme nini hiki kama sio janga. Na hakuna shaka kushindwa kuhesabiana ndiyo sababu ya ajali za majini . Hatuna ajali ya majini ambayo  idadi ya watu ilikuwa sawa(capacity). Zote idadi ilizidi.

Tizama pale feli kigamboni. Vinafanya kazi vivuko vitatu kwa kupishana  na wote tiketi mnachukua sehemu moja. Kama kinazama kivuko kimoja pale(mungu aepushie mbali)  nani anaweza kusema idadi ya waliokuwemo. Kwasababu hata tukisema tuhesabu tiketi bado hutopata jibu kwakuwa   tiketi za kupanda kivuko chochote kati ya vitatu zinakatwa sehemu mmoja, hivyo huwezi kujua aliyekata tiketi amepanda kivuko kipi kati ya vitatu.

Lakini tizama watu wanavyoingia kwenye kivuko. Geti likifunguliwa  mpaka mtu mwenyewe aseme kimejaa sana siingii, vinginevyo watu wote mlioko kwenye banda la kusubiria mtaingia. Kivuko hiki kinabeba watu wangapi kwani. Kikija kidogo wanaingia haohao, kikija kikubwa wanaingia haohao, Looh.Mwanzoni nilifikiri kwakuwa safari ya feli - kigamboni ni ya karibu sana basi sio rahisi kutokea janga, lakini MV Nyerere imenifunza mengi. 

Hoja ni kwamba, kama huwezi  kujua na ukawa na idadi halisi ya waliosafiri maana yake huwezi kudhibiti  upakiaji  unaozidi  uwezo wa chombo.  Kwanini, kwasababu unajua chombo kinahitaji kupakia wangapi, lakini hujui wanaoingia huwa ni wangapi.Na hapa ndipo yalipo majanga.

Sasa tubadilike, yatoshe tuliyofunzwa na ulimwengu. Tunahitaji mifumo mizuri ya kuratibu upakiaji wa abiria na mizigo katika vyombo vya majini. Uratibu unaanza na nani anawajibika na nini, vifaa vya kutambua watu wanaoingia kusafiri, na sio mashine za kukatia tiketi tu,  usimamizi wa kiwango cha juu kwenye vituo vya meli na vivuko, kuondoa rushwa meneo hayo,mfumo wa uongozi katika bandari na meli unaoanisha kwa uwazi wajibu wa kila mfanyakazi. 

Isiwe kama ya MV Bukoba kapteni anasema, ni chief officer, chief officer anasema ni 1st officer, 1st officer anasema ni marine surveyor, marine surveyor anasema  port officer,  yaani unakosa hata awajibike nani katika nini mpaka mwisho watu wote wanaachiwa huru. Mfumo mzuri wa nani anawajibikia nini.

Watu wa marine wachukue semina  ya usimamizi wa abiria na mizigo kwenye viwanja vya ndege. Hakuna dhambi umakini uleule unaotumika kwa abiria na mizigo kwenye viwanja vya ndege ukatumika maeneo ya bandarini kwasababu pote zinabebwa roho za watu. Kwanini huku ionekana   tahadhari kubwa ya abiria na mizigo  wakati huku hakuna, na wanaobebwa wote ni watu. Tusipofanya hivyo tukaendelea na uenyeji enyeji wetu huu, tujiwekee guarantee ya kupokea misiba ya majini kila baada ya kipindi fulani.

Narudia tena tatizo lipo kwenye upakiaji, soma ripoti zote za ajali za meli ni abiria na mizigo kuzidi. Hapa ndipo tunatakiwa kushughulika napo. Yanitoshe haya kwa leo.
MWANDISHI  WA MAKALA HII NI WAKILI WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA NA MAHAKAMA ZA CHINI YAKE ISIPOKUWA MAHAKAMA YA MWANZO, NA MCHAMBUZI WA MASUALA YA SHERIA NA SIASA. +255 784 482 959.




2 comments:

  • Unknown says:
    29 September 2018 at 22:36

    Hongera xana msomi, kwa uchambuzi wa kitaalamu na wenye kuelewekaa, makala hii inaonyesha uzalendo wako hakika huu ndio uzalendo,ujumbe huu ukiwafikia wa lengwa twaweza kuondoa tatizo. Hongera xana bro

  • gosbert Jr.blog.com says:
    5 February 2022 at 11:40

    Wapumzike kwa amani waliopoteza maisha yao katika ajali ya mv bukoba

Post a Comment