Thursday 23 August 2018

UTARATIBU MPYA WA KUSAJILI KAMPUNI.



Image result for kusajili kampuni online
NA  BASHIR  YAKUB -

Tokea April mwaka huu 2018 utaratibu wa kusajili kampuni umebadilika. Ni tofauti kabisa na ambavyo tulizoea.Hata hivyo, yapo mambo ambayo yamebaki vile vile kama awali, kadhalika yapo mengi pia yaliyobadilika.Tutapitia utaratibu wa awali kidogo na huu mpya.

UTARATIBU WA AWALI.

a  Ulikuwa unatakiwa kuandika barua kuuliza jina unalotaka kutumia kama jina la kampuni  iwapo lipo au hapana. Kama lipo ungetakiwa kuleta jingine, na kama halipo ulikuwa unapewa ruhusa ya kulitumia katika usajili.

b ) Ulikuwa unatakiwa kuandaa waraka na katiba ya kampuni(article and memorandum of association). Zilikuwa zinatakiwa kwa uchache  angalau nakala nne.

c  ) Ulikuwa unatakiwa kupakua fomu namba 14(a) na 14( b ) kutoka kwenye mtandao wa BRELA, au kuzifuata fomu hizo hapohapo BRELA ambapo ungetakiwa kuzijaza kisha kuzisaini.

d  ) Kisha ulikuwa unatakiwa kubeba hizo nakala za waraka na katiba ya kampuni, pamoja na hizo fomu zilizojazwa na kuzipeleka BRELA  mnazi mmoja jengo la ushirika kwa ajili ya usajili.

e ) Huko BRELA, baada ya kuzipitia na kuona hazihitaji masahihisho sasa ungepewa ruhusa ya kulipia ambapo malipo yalikuwa yakifanyika kupitia benki ya CRDB.

f  ) Baada ya hapo ungetakiwa kusubiri kipindi cha wiki moja au wiki na sikukadhaa, au wiki mbili  ili uweze kupatiwa cheti rasmi cha usajili  wa kampuni(certificate of incorporation).

UTARATIBU MPYA.

a  ) Hitaji la kwanza kabisa katika utaratibu mpya ni lazima uwe na kitambulisho cha taifa. Sio kile cha mpiga kura bali kile cha NIDA. Hiki ni lazima. Na si lazima tu kwa yule anayetaka kufungua kampuni, bali lazima kwa yeyote ambaye atakuwa mwanahisa katika kampuni(shareholder), au ataandikwa(subscribe) kama mkurugenzi katika kampuni.

Kwa ufupi yeyote anayeingia kwenye nyaraka za kampuni ambazo zinatakiwa kuwasilishwa BRELA kwa ajili ya usajili wa kampuni ni lazima awe na kitambulisho hiki.

Lakini pia tokea mabadiliko haya yafanyike, muamala wowote unaotakiwa kuufanya kuhusiana na kampuni  mathalan kubadili jina(name change), kubadili aina ya kampuni, kubadili wakurugenzi, kuongeza au kupunguza wanahisa au hisa, mrejesho wa mwaka(annual return), kuuliza  hadhi ya kampuni(official search) nk, lazima uwe na kitambulisho hiki.

b ) Lazima ufungue akaunti au mtu mwingine mwenye akaunti akusaidie kukusajilia. Usajili wa sasa unafanyika kwenye mtandao kupitia akaunti iliyofunguliwa na mhusika anayehitaji kufungua kampuni. 

Kufungua akaunti unaingia kwenye WEBSITE ya BRELA humo utaona  maelekezo ya kufungua akaunti ambayo kimsingi sio yenye utata(complicated). Kufungua akaunti ni rahisi sana sharti kubwa ni  uwe tu na kitambulisho nilichoeleza hapo juu kwenye “a”.

c ) Ukishakuwa na akaunti basi utaSCAN waraka na katiba ya kampuni(memorandum & article of association) , kadhalika uta SCAN fomu zote zilizojazwa taarifa husika, utajaza taarifa za ziada kwenye mtandao kwenye akaunti yako kisha utatuma BRELA.

d  ) Ada za usajili sasa unalipia kwa njia ya mtandao wa simu  tigopesa, Mpesa Airtel Money nk, au benki ukitaka iwe hivyo.

e  ) Muda wa kusubiri usajili nao umepungua ambapo kama kila kitu kimefanyka vizuri unaweza kusubiri chini ya wiki moja ili upate cheti cha usajili wa kampuni(certificate of Incorporation).

f  ) Cheti cha usajili nacho kikiwa tayari kinatumwa moja kwa moja kwenye akaunti yako, na wewe hukohuko uliko utakichapa(print) na kuanza kukitumia bila kuhitaji kwenda BRELA kukifuata kama ilivyokuwa awali.

Ada, masuala ya uandaaji wa nyaraka na kuzijaza taarifa, kuzisaini ikiwa ni pamoja na kuzigonga mihuri ya wakili yamebaki vilevile. Kubwa lililobadilika ni hitaji jipya na kitambulisho cha taifa, na usajili kupitia mtandao kutoka mfumo wa usajili wa ana kwa na(physical/manual).

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment