Wednesday 1 August 2018

FOMU YA KUOMBA HATI MPYA PALE YA ZAMANI INAPOPOTEA.



Image result for FOMU KUBATILI HATI
NA  BASHIR  YAKUB -

Ni fomu namba 3 katika kanuni za Sheria ya usajili wa ardhi .Inatokana na kifungu cha 38 cha Sheria ya Usajili wa Ardhi Sura ya 334. Fomu hii  kazi yake ni kuombea hati mpya ya ardhi  baada ya ile uliyokuwa nayo mwanzoni kupotea. Hati, sawa ilivyo kwa vitu vingine vyote inaweza kupotea, kuibiwa au kuharibiwa. Mazingira ya matukio haya yote yameandaliwa majibu na sheria za ardhi.  Fomu hii namba 3 ni rasmi kwa waliopoteza hati  na hivyo kutaka kupata hati mpya.

Fomu hii hutakiwa kujazwa na mhusika yaani yule ambaye jina lilikuwa linasomeka kwenye hati iliyopotea. Kama lilikuwa likisomeka jina la kampuni basi wale waliokuwa wamesaini ile hati iliyopotea awali ndio wasaini na kujaza fomu hii. Anaweza kuwa mkurugenzi wa kampuni ama katibu wa kampuni.

Msimamizi wa mirathi pia anaweza kujaza na kusaini fomu hii ikiwa jina lililo kwenye hati iliyopotea ni la mtu ambaye sasa ni marehemu. Isipokuwa sasa kwa msimamizi wa mirathi ni lazima awe na fomu za kuthibitisha kuteuliwa na kuthibitishwa na mahakama kuwa msimamizi wa mirathi. Ikiwa msimamizi wa mirathi ni zaidi ya mmoja basi  wote watajaza fomu hii ya kuomba hati mpya na watasaini .

Yafaa tujue kuwa kabla hujajaza fomu hii ni muhimu ukawa tayari umetafuta na kupata  taarifa ya kupotelewa(lost report) kutoka kituo cha polisi. Taarifa ya Kupolewa si tu  ni muhimu, bali pia ya lazima kwani ndio itakayoambatanishwa kwenye hii fomu ya kuomba hati mpya. Msajili wa hati hawezi kujua kama kweli umepotelewa na hati kama hakuna taarifa hii.  Na ni ushauri kuwa kitu cha kwanza unachotakiwa kufanya unapopotelewa na hati ni kutoa taarifa polisi na kupata taarifa rasmi ya kupotelewa.

Basi unapokuwa umejaza fomu ya kuomba hati mpya, na umeambatanisha taarifa ya kupotelewa, peleka nyaraka hizo kwa msajili wa hati. Mamlaka za ardhi zina vitengo vingi, ila kitengo rasmi kinachohusika na maombi haya ni ofisi ya msajili wa hati. Kwahiyo peleka hapo nyaraka zako. Msajili wa hati anaweza kuomba taarifa nyingine zaidi za uthibitisho kuhusu kupotelewa kwako. Anaweza kuomba kiapo au vinginevyo ili kujiridhisha. Hicho atakachoomba utatakiwa kukiwasilisha  ili maombi yako ya hati mpya yaweze kukubaliwa.

Fomu husika ya kuombea hati mpya ina maeneo makuu mengi. Kwanza, ni kichwa  ambacho huandikwa “maombi ya  kuomba hati mpya”. Pili, kuna sehemu ya picha. Picha kwa maana ya paspoti size moja ambayo itakaa upande wa kulia wa fomu husika. Kimsingi picha zinatakiwa kuwa tatu kwakuwa  fomu zitatakiwa kuandaliwa tatu pia ili kila fomu ipate picha moja.   Hata kujaza na kusaini kama ilivyoelekezwa hapa juu itakuwa ni hivyohivyo  fomu tatu zote.

Fomu ina sehemu ya mtu kueleza jina lake lile lililokuwa likitumika kwenye hati ya awali  pamoja na anuani yake. Kuna sehemu ya kueleza kuwa hati imepotea hali kadhalika maelezo ya namna ambavyo imepotea. Pia yapo maelezo ya kiapo kwenye hiyo fomu kuwa ni kweli hati imepotea na haijawekwa sehemu nyingine yoyote kwa makusudi mengine.  Mwisho tarehe  ya kujaza fomu na sahihi ya muombaji/waombaji. Kisha itashuhudiwa na Wakili.  Wakili atasaini na kugonga mhuri.               

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment