Wednesday 25 July 2018

MAHAKAMA KUU KITENGO CHA MAWAKILI WANASTAHILI PONGEZI.



Image result for mahakama kuu
NA BASHIR  YAKUB -

Kawaida  safu hii huandika na kufafanua masuala mbalimbali ya kisheria  na mahakama.  Mara nyingi huandika kuhusu ndoa, mirathi, makampuni, jinai, ardhi, na madai mengine kwa ujumla. Leo itakuwa tofauti kidogo japo ni ndani ya tasnia ya sheria humohumo.

Nianze tu kwa kusema kuwa wakati taifa zima likifanya kazi kufikia uchumi wa kati ambao ndio dira ya mihimili yote mahakama,bunge na serikali, kuna jambo moja ambalo hatuwezi kulisahau. Jambo hili ni utumishi uliotukuka. Hakuna ubishi, injini ya uchumi wa kati ni watumishi. Lakini ni aina gani ya watumishi ambao ni injini ndilo litakuwa swali. Aina ya watumishi ambao wanaweza kutufikisha huko ni wale  wenye moyo wa kazi, ari, uvumilivu, waelewa,na wale ambao utumishi kwao sio kazi tu ya kusubiri mshahara mwisho  wa mwezi, bali pia huduma nzuri kwa watu.

Kote duniani ambako si tu wamefikia uchumi wa kati tunaoulilia, bali pia wana uchumi wa juu kama china, amerika, na nchi za ulaya wamefikishwa hapo na watumishi bora . Waliowahi kufika huko wanajua ni namna gani watumishi wa huko wanavyotoa huduma. Unaweza kudhani unahudunmiwa na ndugu yako wa tumbo moja. 

Niseme tu kuwa watumishi wa mahakama kuu ya Dar es salaam kitengo cha mawakili wameonesha mfano wa aina hii. Ni aina ya watumishi ambao ukibahatika kuhudumiwa nao unahisi kweli umepewa huduma. Hawatachoka kukupatia maelezo, hawatachoka kukuelekeza, na hata ukitaka namba zao binafsi hukupatia, na endapo utapiga muda wowote kutaka ufafanuzi utapewa bila kukaripiwa kama ambavyo imekuwa pahala pengine pa utumishi.

Ni muhimu sana, tena sana kumpatia sifa anazostahili  yule ambaye amefanya vizuri. Kadhalika kumuonya yule ambaye hajafanya vizuri. Tumekuwa tukipenda sana  kukosoa na kulalamika huku tukiacha kusifia na kusemea yaliyo mazuri. Hii ni desturi mbaya kabisa na inavunja moyo. Hata awe Rais , Jaji mkuu au Spika na ukubwa wao wote, pale ambapo wanafanya mambo mazuri badala ya kusifia tukakosoa tu, nao huwa tunawavunja moyo.

Nimefanya kazi za mahakama kwa muda mrefu kabla sijawa wakili na baada. Nawajua watumishi mbalimbali wa ngazi za mahakama kama makarani, watunza kumbukumbu, wapeleka nyaraka(process server), wahasibu, nk. Sio siri wengi wamekuwa wakilalamikiwa sana na wananchi. Masuala ya mafaili kupotea ilishaacha  siku nyingi mno kuwa  habari ya kushangaza . Namkumbuka mhasibu mmoja wa kike mahakama ya wilaya kinondoni . Alikataa kutukatia risiti za malipo watu kama sita hivi akasema ana kazi nyingine na hivyo turudi kesho, na badala yake akahamia chumba kingine akawa anapiga gumzo na wenzake.  Na anafanya hivyo  akijua kabisa kuwa unapokata risiti ndipo unapohesabika kuwa umeingiza nyaraka mahakamani ndani ya muda. 

Kwahiyo usipopata risiti leo maana yake kwa mujibu wa sheria  umeingiza nyaraka mahakamani kwa kuchelewa na hivyo inaweza ikawa mwisho wa kesi yako, yaani umepoteza. Hawa ndio wengi wa watumishi wetu.

Niwataje na kuwapongeza wawili tu kwa niaba ya wengine kitengo cha mawakili mahakama kuu Dar es salaam. Rajab Kagame na Mwenzake ndugu Bedson Mariba hongereni sana. Mnafanya kazi nzuri na nyie ni mfano wa kuigwa. Mawakili na wananchi wengine ambao hupata  huduma yenu hapo ni mashahidi wa hili. Anayefanya vizuri sharti aambiwe ili aongeze na aamshe ari kwa wengine.
Nimalize kwa kusema kuwa utumishi sio tu ni kazi bali pia ni  huduma, basi yafaa tufanye kazi  kwa kutoa huduma.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment