Tuesday 26 June 2018

NAMNA YA KUKATA RUFAA KWA WALIOFUKUZWA KAZI KWENYE UTUMISHI WA UMMA.



Image result for UTUMISHI WA UMMA
NA  BASHIR  YAKUB -

Wapo watumishi wa umma ambao wameachishwa kazi kwasababu mbalimbali na wanahisi kuwa pengine haki haikutendeka lakini hawajui la kufanya. Basi waelewe la kufanya lipo na ni rufaa. Na wengine wanajua kuwa ni rufaa yumkini wasijue rufaa yenyewe inakatwa kwa utaratibu upi. Nitaeleza hapa, lakini kwanza tujue nani mtumishi wa umma anayeongelewa hapa.

1.NANI MTUMISHI WA UMMA.

Sheria namba 8 ya 2002, Sheria ya Utumishi wa Umma , iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Namba 18 ya 2007 imemueleza mtumishi wa umma. Kifungu cha  3  kinasema kuwa mtumishi wa umma ni yule anayefanya kazi katika ofisi yoyote ya umma. Ili uelewe vizuri mtumishi wa umma anayeongelewa katika sheria hii na katika makala  haya ni yule mfanyakazi/mwajiriwa wa serikali.  Kwahiyo watumishi wa bunge, maafisa wa mahakama, na wafanyakazi wa taasisi/kampuni binafsi  taratibu hizi za rufaa zinazoelezwa humu haziwahusu.

Tunaongelea watumishi wa serikali kuu, za mitaa, mashirika ya umma, idara na taasisi zote zilizopo chini ya serikali tukiondoa wale wa uteuzi japo nao wanaongozwa na sheria hii.

2.  HAKI YA RUFAA.

Unapokuwa umesimamishwa kazi rufaa ni haki yako ewe mtumishi. Rufaa sio kuonesha ukorofi, sio kuwa mjuaji, sio kupingana na serikali, na sio kukosa utiifu. Rufaa ni haki kama zilivyo haki nyingine za mshahara, likizo, nk. Usiogope kukata rufaa kwani hata huyo aliyekusimamisha kazi naye akisimamishwa anakata rufaa.
Kifungu cha 25( 1 ) (b) cha Sheria ya utumishi wa umma ndicho kinachoeleza haki hii. 
Kadhalika kwenye barua yako ya kuachishwa kazi  au siku ya kusimamishwa, yafaa na ni haki uelezwe haki hii ya rufaa.

3. KUSHUSHWA CHEO NAKO KUNAKATIWA  RUFAA.

Rufaa sio kwa ajili ya kusimamishwa kazi tu. Kifungu hichohicho cha 25 cha Sheria ya Utumishi wa Umma kinasema rufaa pia inaweza kukatwa iwapo umeshushwa cheo , au  mshahara wako umepunguzwa. Kwahiyo haki ya rufaa kwa mtumishi ni pana na haikomei kwenye kusimamishwa kazi pekee.

4.  RUFAA  INAKATWAJE?.

Rufaa ni maelezo mazuri yenye hoja za kimazingira, yaani kile kilichotokea(facts), yakisaidiwa na hoja za kisheria(point/s of law). Na itakuwa katika mfumo wa maandishi. Itakuwa na sehemu kuu tatu,yaani  kichwa, hoja na hitimisho.

Kichwa chaweza kuwa “RUFAA YA KUPINGA KUSIMAMISHWA KAZI”.

Hoja, Utaeleza kile kilichotokea/ unacholalamikia  kwa maana ya yale maeneo(areas/aspects) unayohisi kuonewa, na kisha utaeleza sheria zinasemaje, au sheria zipi zilikiukwa wakati ukiwajibishwa.

Ni kitu ambacho unaweza kuandika na wala huna haja ya kuhofu. Ni maelezo ya namna ulivyoonewa + Sheria zinasemaje au sheria zipi zimevunjwa. Pia  taratibu za kukuwajibisha, mfano kutosikilizwa kabla  ya kuadhibiwa, kupewa mda kidogo wa kujitetea, kutoitwa kwenye kikao cha nidhamu nk, nayo ni maelezo ambayo unaweza kuingiza eneo hili la hoja.

Hitimisho. Hapa  utaomba maamuzi ya awali ya kufutwa kazi yabatilishwe na rufaa yako ikubaliwe/ishinde, utaomba urejeshwe kazini, kisha  utaandika jina lako, nafasi yako (uliyofutwa/cheo), na utaweka namba yako ya simu.

5. RUFAA IPELEKWE WAPI.

Ukishaandaa rufaa sheria inakutaka kuipeleka tume ya utumishi wa umma. Ofisi zao kwasaasa zipo pale Ubungo Plaza kwa Dar es salaam. Hiyo ni kwa mujibu wa kifungu cha 25 (1)(b) cha Sheria ya Utumishi wa Umma.

Pia unapokuwa umeandaa yale maelezo yako ya rufaa yafaa nakala uipeleke kwenye mamlaka/ofisi iliyokuwajibisha/iliyokufuta kazi. Hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 61( 1 )  Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003.

6. MUDA WA KUKATA RUFAA.

Kanuni  ya 61( 1 ) Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003  inasema kuwa  rufaa inatakiwa kukatwa ndani ya siku 45  tokea siku  yalipotolewa maamuzi ya kufutwa kwako kazi.  Utehesabu  siku 45 na ndani mwake uwe umekata rufaa.

7. KUCHELEWA KUKATA RUFAA.                             

Kanuni  ya 61( 4 ) Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003 inasema kuwa mtumishi aliyechelewa kukata rufaa ndani ya muda wa siku 45 rufaa yake inaweza kupokelewa ikiwa tu anazo sababu za msingi za kuchelewa.

Hivyo basi, unapokuwa  umechelewa na kupitwa na muda unachotakiwa kufanya ni kuandaa maelezo ya kuchelewa kwanza kabla ya maelezo ya rufaa. Utaeleza kwanini umechelewa na kama una ushahidi wa sababu za kuchelewa utaambatanisha kwenye maelezo yako. Kisha utaeleza rufaa yako kama ilivyoelekezwa hapo juu.

Maelezo yakuchelewa na maelezo ya rufaa yanakuwa ni maelezo kwenye nyaraka moja isipokuwa unaanza kueleza kuchelewa kwako na kuomba rufaa yako ipokelewe nje ya mda, kisha kwenye nyaraka hiyohiyo unatoa hoja zako za rufaa kama ilivyoelekezwa hapa juu.  Halafu unasaini na kupeleka kwa ajili ya mawasilisho.

8. VIAMBATANISHO VYA RUFAA.  

Rufaa yako inatakiwa iambatanishwe(annexeture/s)  na nakala ya maamuzi ya kufutwa kwako kazi. Barua ya kufutwa kazi ndiyo maamuzi ya kufutwa kazi ambayo nakala yake(kopi) unatakiwa kuambatanisha nyuma ya maelezo yako ya rufaa. Pia kama unavyo vielelezo vingine(exhibit/s) vinavyosimamia  hoja zako navyo waweza kuviambatanisha. Kwahiyo ni muhimu kupewa barua ya kufutwa kazi mara tu unaposimamishwa.

9. USUBIRI  MAJIBU YA RUFAA  BAADA YA MUDA GANI ?.     

Kanuni  ya 62( 2 ) Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003, inasema kuwa ndani ya siku 90 tokea siku ilipopokelewa rufaa unapaswa kupokea majibu ya rufaa hiyo. Hivyo ikifika muda huo na ukaona kimya yafaa ufuatilie hukohuko ulipopeleka  ili kujua  kulikoni.

10. HAKI ZAKO NI ZIPI IKIWA RUFAA YAKO IMESHINDA ?.

Kifungu cha 25( 1 ) ( e ) cha Sheria ya Utumishi wa Umma pamoja na Kanuni  ya 60( 6 ) Kanuni za Utumishi wa Umma vinasema iwapo rufaa itashinda basi mtumishi aliyekuwa amefukuzwa atahesabika kama ambaye hakuwahi kufukuzwa. Maana yake haki zote za mishahara muda uliosimama, haki za likizo, na mengine utastahili kupata ikiwemo kurejea kazini mara moja.

11. NINI UFANYE RUFAA YAKO IKISHINDWA.       

Bado unakuwa na nafasi ya rufaa  ikiwa tume itaamua kuwa rufaa yako imeshindwa. Kifungu cha 25( 1 ) ( d ) cha Sheria ya Utumishi wa Umma pamoja na Kanuni  ya 60( 5 ) Kanuni za Utumishi wa Umma vinasema kuwa , mtumishi ambaye hakuridhishwa na maamuzi ya tume ya rufaa anaweza kukata rufaa tena kwenda kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano.

Rais  ndiye mkuu wa watumishi wote na maamuzi yake yatakuwa ni ya mwisho na hakutakuwa na rufaa nyingine tena isipokuwa sasa ukiamua kubadilisha mwelekeo/upepo  na kwenda mahakamani.
Haya ndiyo ya msingi kuhusu rufaa ya mtumishi wa umma.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com








0 comments:

Post a Comment