Thursday 21 June 2018

MSAADA WA KISHERIA BURE BILA MALIPO YOYOTE.


Image result for MSAADA WA SHERIA


NA  BASHIR  YAKUB -

Wapo watu wana matatizo na wanahangaika kupata msaada wa bure wa kisheria lakini hawajui waanzie wapi,wafanye nini ili kupata huduma hii. Taratibu zipo, na unaweza kupata wakili wa kusimamia kesi yako bure bila malipo kupitia utaratibu wa msaada wa kisheria. Unaweza kupata uwakilishi huu  katika kesi zote yaani zile za jinai pamoja na zile za madai. 

Tunapoongelea za jinai tunamaanisha zile kesi za kuua,kubaka, kupiga,kutukana nk, na tunapoongelea kesi za madai  tunamaanisha zile za ardhi kugombea mali, mirathi, ndoa, mikopo,watoto malezi, talaka, nk.

Kwahiyo pote kwenye jinai na madai unaweza kupata uwakilishi wa bure wa Wakili. Utasimamiwa kesi yako mwanzo hadi mwisho bila kuhitaji kulipa gharama yoyote. Na msaada wa kisheria unaweza kuwa wa uwakilishi kwa maana kuwa wakili utakusimamia mahakamani au unaweza kuwa wa ushauri tu bila kuhusisha mahakama au vyote kwa pamoja. 

Lakini yafaa tufahamu kuwa sio watu wote wanaweza kupata msaada huu. Makala yataeleza utaratibu wa kupata msaada wa kisheria bure halikadhalika ni watu wa aina gani wanaweza kupata msaada huu.

1.WANAOSTAHILI KUPATA MSAADA WA KISHERIA BURE.

i)Watu wasiojiweza kabisa kifedha.
ii) Wanawake.
iii)Wazee.
iv)Walemavu.
v) Watoto.
vi)Wagonjwa wasiojiweza.

Hata hivyo kwa wanawake, walemavu,wagonjwa wasiojiweza, na wazee bado nao sifa ya kutokuwa na uwezo wa kifedha inatizamwa. Haimaanishi kila mwanamke,mzee,mgonjwa au mlemavu anastahili msaada wa kisheria wa bure. Sifa ya kutokuwa na uwezo kifedha ni sifa kuu inayoangaliwa. Isipokuwa kwa watoto hata kama mzazi au mlezi ana uwezo, bado mtoto anaweza kupatiwa msaada huu kwakuwa kinachoangaliwa ni maslahi ya mtoto mwenyewe wala sio ya mzazi ama mlezi.

2.  UTARATIBU WA KUOMBA MSAADA WA KISHERIA.

Utaratibu utategemea kama tatizo lako ni madai au jinai.

i)Madai.

Ikiwa ni madai kwa mfano masuala ya ardhi, mirathi,ndoa, watoto, nk utatakiwa kutafuta vituo vya misaada ya kisheria. Vituo hivi ni zile asasi(NGO) zisizo za serikali ambazo  hutoa misaada ya kisheria. Kila mkoa zipo na hutofautiana mkoa hadi mkoa.

Kama hujui zilipo basi waweza kwenda eneo la mahakama na hapo utauliza wapi nitapata shirika  la msaada wa kisheria  na hapo utaelekezwa. Pia unaweza kuuliza makao makuu ya wilaya  kwani orodha ya mashirika huwa ipo hapo pia . Zaidi, unaweza kuuliza kwenye ofisi za mawakili wa kujitegemea ili uelekezwe mashirika ya msaada yalipo. Na kwa wanaojua kutumia mtandao, humo pia unaweza kutafuta ukapata. Maeneo haya utapata majibu sahihi ya wapi yalipo mashirika ili usaidiwe.

Ukilipata shirika husika basi watakupa utaratibu wao  lakini zaidi huwa ni kujaza fomu maalum na kuleta barua ya utambulisho kutoka serikali za mitaa inayokutambulisha na kuelezea hali yako  ya kiuchumi.  Taratibu nyingine ni za kawaida na hapo utapata ushauri wa kisheria bure au wakili wa kukuwakilisha bure bila malipo yoyote.

ii)  Jinai

Sura ya 21 ya Sheria ya Msaada wa Kisheria katika Jinai ndiyo hueleza utaratibu wa msaada wa sheria katika jinai. Kifungu cha 3( 1 ) kinaeleza makosa ya jinai ambayo unaweza kuombea msaada wa kisheria kuwa ni yale  ambayo adhabu zake haziko chini ya kifungo cha miaka 15, adhabu za kifo, maisha, adhabu ya kuondolewa ndani ya nchi, na sifa nyingine zilizotajwa hapo juu mwanzoni  awali.

Utaratibu wa kupata msaada hapa kama huna uwezo ni kuomba kwa hakimu husika au jaji kuwa unaomba kupata msaada wa uwakilishi kwasababu huna uwezo. Muombe huyuhuyo hakimu au jaji anayesikiliza kesi yako. Na unaweza kumuomba mda wowote hata mara ya kwanza tu unapofikishwa mbele yake. Yeye anajua ni utaratibu gani afuate ili upate wakili wa kukuwakilisha bure bila malipo yoyote.

Na usiogope kumuomba hakimu/jaji kwani kufanya hivyo ni haki yako, na takwa la kisheria na wala sio kosa au ujuaji(much know).
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment