Thursday 31 May 2018

NINI UFANYE KAMA KESI YAKO MAHAKAMANI INACHELEWESHWA BILA SABABU ZA MSINGI.


Image result for mahakamani


NA  BASHIR  YAKUB -

Ni miaka mingi tangu kesi yako imefunguliwa mahakamani lakini  haiishi.  Huelewi ni kwanini na kila siku ukienda ni tarehe juu ya nyingine. Mwingine atakwambia kesi yangu ina miaka  zaidi ya kumi  na bado haijaisha nk.  Tatizo hujui nini  zaidi ya kupata kalenda kila siku. Basi makala yataeleza hatua ambazo unaweza kuchukua kumaliza tatizo hili.

Aidha, Ibara ya 29(2 ) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka bayana kuwa kila raia wa Tanzania ana haki ya kupata ulinzi wa sheria. Basi sio sawa ukimbilie mahakamani kupata ulinzi wa sheria halafu usipate ulinzi huo hata baada ya miaka mingi.

CHUKUA HATUA HIZI  KAMA KESI YAKO IMECHELEWESHWA  BILA SABABU ZA MSINGI.

( 1 ).Tafuta ushauri wa kisheria kutoka kwa mwanasheria,hata wale wa msaada wa sheria. Utamwelezea ishu yako nzima na wapi umekwama. Huyu atakusaidia kutambua kama imechelewa kwa makusudi, kwa uzembe, au ni sababu tu za kisheria zimesababisha ichelewe. 

Wakati mwingine kesi inaweza kuchelewa kwasababu za kisheria ambazo ziko juu ya uwezo wa mahakama kuiharakisha kesi yako, kwa mfano mapingamizi ya mara kwa mara, maombi ya mara kwa mara, upelelezi kuchelewa nk, nk. Hii ndiyo sababu utamtafuta mwanasheria ili abainishe(identify) nini hasa chanzo cha kukwama kwa kesi yako. Atakwambia kama umeonewa au sheria ndivyo ilivyo.

( 2 ). Toa malalamiko yako kwa jaji au hakimu anayesikiliza kesi yako. Usiogope kumwambia Jaji au hakimu kuhusu kuchelewa kwa kesi yako.Kumwambia ni haki yako na hutaambiwa kuwa umekosea au umeidharau mahakama.  
Na unaweza kumwambia kwa njia mbili, moja  kwa mdomo, na pili kwa kumwandikia barua.

Kwa mdomo utamwambia wakati wowote kesi itakapokuwa ikiendelea mahakamani, baada ya kunyoosha mkono na kumuomba kuwa kuna jambo unataka kumwambia, na kwa maandishi utaandika barua na kuipeleka masijala,au kwa karani wake, au namna nyingine utakavyoelekezwa na wahusika pale mahakamani. Usitukane wala kusema/kuandika maneno ya hovyo, eleza tu lalamiko la kesi yako kuchelewa na utasaidiwa.

( 3 ). Kama hukupata msaada hapo juu, basi peleka malalamiko yako kwa hakimu mfawidhi, jaji mfawidhi, au hata kwa msajili. Hakimu mfawidhi ni hakimu kiongozi wa eneo la mahakama husika. Kwahiyo kama kuna mahakimu wengi eneo lile la mahakama yeye ndiye kiongozi wao. 

Na utampataje/utamjuaje, ni kwa kuuliza tu. Uliza hakimu mfawidhi ni nani na mpe malalamiko yako. Unaweza kufanya hivyo kwa mdomo/mazungumzo au kwa barua kama tulivyoona hapo juu.

Wakati mwingine hakimu mfawidhi anaweza asiwe anakaa eneo la mahakama bali yuko huko wilayani au pengine. Bado si tatizo, uliza  na peleleza ujue alipo mfuate na mpe malalamiko yako au mwandikie. Hii ni kwa wale ambao kesi zao zipo mahakama za mwanzo, za wilaya na zile za hakimu mkazi.

Kwa wale ambao kesi zao zipo mahakama kuu, Jaji mfawidhi ndiye kiongozi wa eneo husika na majaji wote wa eneo hilo anawaongoza yeye. Unaweza kumpatia huyu malalamiko yako kwa njia ya mdomo/mazungumzo, au kwa njia ya maandishi.  Unampataje/unamjuaje, ni kwa kuuliza tu.Uliza jaji mfawidhi ni nani ,na omba kuonana naye kwa mujibu wa utaratibu wa pale ulivyo au mwandikie.

( 4 ). Kama hukupata msaada katika 3 juu, basi peleka malalamiko yako kwa Jaji mkuu. Jaji mkuu ni mtumishi mkuu wa mahakama, na yupo kuhudumia, na kutatua kero za watu ikiwemo ya kwako. Huyu sio mfalme ambaye hawezi kufikika, laa hasha. Ni mtumishi na anawatumikia watu kama wewe. Isipokuwa sikushauri uende kwake kabla hujapitia ngazi hizi zilizoelezwa hapa juu.  Yeye apelekewe tatizo sugu ambalo limeshindikana huku kote.

Jaji mkuu ni mmoja Tanzania nzima na ofisi yake kuu ipo mahakama ya rufaa kivukoni, Dar es salaam.  Naye unaweza kumwandikia barua au ukaomba miadi ya ana kwa ana.
Wakati mwingine unaweza kuwa unacheleweshwa na watu wa chini na hawa viongozi waliotajwa humu hawajui. Wafuate watakusaidia.

Yumkini, usiende kwa rais,waziri mkuu,waziri yeyote ,mkuu wa mkoa, wa wilaya ama mkurugenzi nk. Hawa katu hawawezi kukusaidia kwakuwa hawawezi kuingilia kazi inayoendelea mahakamani. Usipoteze mda chukua hatua sahihi.  Hakuna nje ya hawa anayeweza kukusaidia.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com




0 comments:

Post a Comment