Monday 28 May 2018

NINI UFANYE UNAPOCHELEWESHWA NA MAAFISA WA MAHAKAMA KUPATA NAKALA YA HUKUMU.

Image result for NAKALA HUKUMU


NA  BASHIR  YAKUB -

Nakala ya hukumu ya mahakama huhitajika pale kesi au shauri linapokuwa limefika mwisho. Kwa lugha nyingine maamuzi ya mahakama ndiyo hukumu ya mahakama. Hapa ndipo tunapojua nani ameshinda na nani ameshindwa. Nani anastahili kulipwa au kukabidhiwa mali fulani na nani hastahili. Kadhalika nani anastahili kufungwa na nani anastahili kuachiwa huru. Yote haya na mengine mengi  ndiyo yanayojenga kitu kinachoitwa hukumu.

1.UMUHIMU WA NAKALA YA HUKUMU.

Mara nyingi wale ambao hawakuridhishwa na maamuzi ya mahakama kwenye hukumu hutaka kukata rufaa. Rufaa ni malalamiko yanayopelekwa mahakama ya juu zaidi  yakilalamikia  hukumu au maamuzi  yaliyotolewa  na mahakama ya chini. Rufaa hufunguliwa na mtu ambaye hakuridhika na kile kilichoamuliwa. Kwahiyo hata wewe kama unayo kesi ambayo tayari imetolewa hukumu na  hukuridhishwa na kile kilichoamuliwa basi unayo haki ya msingi ya kukata rufaa.

Na huna haja ya kuhofu kama unazo sababu za msingi na za kisheria. Waweza kuwa umeshindwa mahakama ya chini lakini ukaibuka mshindi mahakama ya juu ambako umekata rufaa.

Hata hivyo, huwezi kukata rufaa bila kuwa na nakala ya hukumu. Na hapa ndipo linapojitokeza suala la kupata nakala ya hukumu kwa wakati na bila kucheleweshwa. Narudia huwezi kukata rufaa ikiwa hujapata nakala ya hukumu kutoka  mahakama  iliyotoa uamuzi.

2. HASARA ZA KUCHELEWA KUPATA NAKALA YA HUKUMU.

Ikiwa lengo lako ni kukata rufaa basi yafaa ujue kuwa rufaa zote huwa zina muda wake. Zipo za siku 45,za siku 30 nk. Muda huo unahesabika tokea siku hukumu iliposomwa. Ni ndani ya muda huo ambapo unatakiwa kukata rufaa. Nje ya muda huo huruhusiwi na unakuwa umepoteza haki hiyo.

Sasa wakati mwingine muda huo waweza kuisha ukiwa bado unashughulikia kupata nakala  ya hukumu. Ni hapa tunapotakiwa kujua la kufanya ili kuepuka kadhia na mazingira hatari kama haya.

3.  KUCHELEWA  KUPATA NAKALA YA HUKUMU.

Unaweza kuchelewa kupatiwa nakala ya hukumu kwasababu mbalimbali. Moja ni kutokuomba kwako kupatiwa nakala ya hukumu. Kesi au shauri linapoisha yafaa mara moja uombe kupatiwa nakala ya hukumu. Katika mada nyingine nitaeleza utaratibu wa kuomba nakala ya hukumu. Kwahiyo kumbe waweza kuchelewa kuipata kwasababu hukuiomba.

Pili, waweza kuchelewa kuipata kwasababu ya uwezo na ufanisi wa mahakama husika. Nakala  ni lazima iwe imechapwa na imesahihishwa vizuri. Ukosefu wa vitendea kazi kama kompyuta laweza kuwa tatizo la kuchelewa kupata hata kama uliiomba kwa wakati.

Tatu, uchache wa watumishi/makarani wachapaji ambapo huwa na mizigo mingi na hivyo huchapa kazi moja moja kwa awamu jambo ambalo laweza kukuchelewesha ukisubiri kazi yako ifikiwe.

Nne,uzembe wa wachapaji  na wakati mwingine huwa ni makusudi ili kujenga mazingira ya  kupozwa(rushwa).

4.  NINI UFANYE IWAPO NAKALA YA HUKUMU IMECHELEWESHWA.

Jambo la kwanza, kesi au shauri linapoisha hakikisha siku hiyohiyo au inayofuata umeandika barua ya kuomba nakala ya hukumu. Hii itakusaidia  kwani hata ukichelewa kukata rufaa ukapitwa na mda utasema mimi niliomba nakala mapema kwahiyo kuchelewa sio makosa yangu.

Pili, ikiwa unaona makarani au wachapaji wanakuchelewesha bila sababu au huelewi ni namna gani wanavyoshugulikia suala lako  tafuta muda muone hakimu aliyetoa hukumu na mpe maelezo  yako na namna ambavyo hujapatiwa nakala hiyo. Au waweza kumuona hakimu mfawidhi. Hakimu mfawidhi ndiye kiongozi wa mahakama husika. Ukiuliza hakimu mfawidhi ni nani utaoneshwa na hapo utampatia malalamiko yako. Hivi ndivyo unavyoweza kuepuka kupoteza haki hii.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA  JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment