Thursday 17 May 2018

NAMNA UNAVYOWEZA KUOMBA KUBADILISHIWA MASHARTI YA UMILIKI WA ARDHI.

Image result for HATI MILIKI YA NYUMBA


NA  BASHIR  YAKUB -

Umiliki wa ardhi hutolewa kwa masharti maalum. Kila aliyepewa hati miliki anajua kuwa amepata hati hiyo kwa masharti ambayo anapaswa kuyatekeleza. Wapo ambao hudhani kuwa ukishapewa hati na masharti basi ni hivyohivyo tu huna la kufanya hata kama hujaridhika au hunufahishwi na masharti hayo.

 Hii ni fikra isiyo sahihi na sasa wapaswa kujua kuwa masharti katika hatimiliki ya ardhi yanaweza kubadilishwa kwa maombi maalum. Masharti ni kwa ajili ya maendeleo na kwa ajili ya maendeleo waweza kuomba kubadilishiwa masharti/sharti la umiliki.

1.NI MASHARTI YAPI HUWEKWA KATIKA HATIMILIKI.

Yapo masharti mengi. Kifungu cha  34 cha Sheria Namba 4 ya ardhi  kimeeleza masharti ya hati miliki. Baadhi ya masharti hayo huwa ni pamoja na matumizi kwa mfano, utaambiwa unapewa hati ya eneo hili ni kwa ajili ya biashara tu, viwanda tu, hoteli tu,makazi tu, nk. 

Au utaambiwa unapewa umiliki wa ardhi kwa miaka 33, 66, au 99. Au utapewa sharti kuhusu ujenzi, kwa mfano utaambiwa eneo hili huruhusiwi kujenga jengo lisilo la ghorofa, au eneo linaruhusiwa kujengwa jengo la chini tu, au pajengwe jengo lisilo la kudumu nk, nk.
Haya ni baadhi ya masharti unayoweza kupewa wakati unapokuwa ukipewa hati miliki.

2. UTARATIBU WA KUOMBA KUBADILISHIWA MASHARTI.

Ndio, unaruhusiwa kuomba kubadlishiwa masharti au sharti kulingana na mahitaji yako.  Unaweza kuomba muda wowote baada ya kupewa umiliki au wakati mchakato wa kupatiwa umiliki ukiendelea. Utaratibu wake ni huu;-

 ( i )Utatakiwa kujaza fomu namba  27 ambayo inaeleza matumizi ya sasa na yale mapya unayoomba kubadilishiwa. Fomu hii inapatikana kwenye kanuni za Sheria namba 4 ya ardhi, za mwaka 2011, pia zinapatikana ofisi za ardhi, na kwa wanasheria.

( ii ) Fomu hiyo itaambatanishwa na nakala ya hati husika, picha za muombaji, na ada ya maombi ya kubadilisha.

( iii ) Itakuwa imesainiwa  na muombaji au wakili wake.

( iv ) Itaambatana na risiti za karibuni za malipo ya kodi za ardhi au jengo.

( v ) Pia utaambatanisha taarifa nyingine yoyote ambayo unaweza kuombwa kuwasilisha  na mamlaka za ardhi.

( vi ) Maombi hayo yatapelekwa kwa kamishna wa ardhi kwani ndiye mwenye mamlaka na mchakato huu.

3. KUKUBALIWA MABADILIKO YA MASHARTI.

Unaweza kukubaliwa maombi au kukataliwa au kubadilishwa  kwa kile ulichoomba. Endapo utakubaliwa  basi kamishna atakutaarifu kwa taarifa maalum kupitia anuani na mawasiliano uliyotumia kwenye maombi. Atakutakata kuwasilisha kwake hati miliki halisi ili  aingize mabadiliko mapya na kutia muhuri wake. Pia atakutaarifu mabadiliko mapya ya malipo ya kodi na tozo za ardhi kutokana na matumizi mapya.

4. ADHABU YA KUKIUKA MASHARTI.

Kifungu cha 45 cha Sheria namba 4 ya ardhi kimesema kuwa ukiukwaji wa masharti ya umiliki wa ardhi  utapelekea hati ya mmiliki kufutwa.  Kufutiwa umiliki ardhi maana yake ni kunyanganywa ardhi.  Kwahiyo ni muhimu kuendana na masharti haya na panapo tatizo au hitaji la kubadili sharti kwa ajili ya maendeleo basi omba ubadilishiwe kuliko kujibadilishia matumizi bila kufuata taratibu jambo ambalo linaweza kugharimu ardhi yako yote.


MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA  JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment