Tuesday 29 May 2018

MFANO WA BARUA YA KUOMBA NAKALA YA HUKUMU HUU HAPA.



Image result for BARUA YA NAKALA YA HUKUM
NA  BASHIR  YAKUB -

Nakala ya hukumu ni haki yako ikiwa ulikuwa mhusika katika kesi au shauri. Unakuwa mhusika katika kesi au shauri pale unapokuwa mshitaki au mshitakiwa,  mlalamikaji au mlalamikiwa, au mhusika mwingine mwenye maslahi.  Hapa ndipo unapohesabika kuwa mhusika katika kesi au shauri na hapa ndipo unapokuwa na haki ya kuomba kupatiwa nakala ya hukumu.

Makala yaliyopita yalieleza kuwa nakala ya hukumu ni muhimu hasa ukitaka kukata rufaa au kuchukua hatua zaidi , lakini pia ni muhimu kama nyaraka ya kumbukumbu kwa ajili ya kesho, pia ni muhimu kwa ajili ya utekelezaji wa kile kilichoamuliwa.  Leo tuone mfano halisi wa barua ya  maombi ya  nakala ya hukumu kama ulivyo hapa chini ;-

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,                                                        24 / 5 / 2018
S.L.P..............................
Dar es salaam.
YAH ; MAOMBI YA KUPATIWA NAKALA YA HUKUMU.

Nilikuwa mlalamikiwa katika shauri namba  13 la mwaka 2018,  ambalo limetolewa hukumu tarehe 22 / 3 / 2018, mbele ya Mhe. Kijana Mponela. Ninaomba kupatiwa nakala ya hukumu  kwa kumbukumbu au hatua zaidi.

Wako
Mti Mkavu
( aliyekuwa mlalamikiwa ).
0717600900
Sahihi...............................

Barua itakuwa nyepesi na fupi hivyo. Na inaweza kuwa imeandikwa kwa mkono au imechapwa. Lakini ni nzuri zaidi ikiwa imechapwa kama uwezo upo.
 Pia unaweza kutumia hii hii ila ukabadilisha tu taarifa(copy&paste).Kwenye anuani imeandikwa kisutu lakini wewe utaweka anuani ya mahakama iliyotoa hukumu yako na mkoa/wilaya ilipo, tarehe utaweka ya kwako, kichwa kinaweza kubaki  hivyohivyo, na kwenye maelezo utabadilisha kutokana na taarifa za kesi/shauri lako. Mwisho utaweka jina lako,namba ya simu pamoja na sahihi yako.

Kumbuka utakapoandika barua hii hakikisha unatoa kopi na unakuwa na nakala mbili. Moja itabaki mahakamani na moja utakwenda nayo ili wakugongee muhuri wenye tarehe wa kuthibitisha kwamba wamepokea. Hiyo iliyogongwa muhuri urudi nayo kwa ajili ya kumbukumbu na hatua za baadae.

Hiyo iliyogongwa muhuri ambayo umerudi nayo ndiyo itakayokusaidia pale utakapokuwa umechelewa kukata rufaa na kupitwa na muda. Na muda umekupita kwasababu  ulikuwa ukiisubiria mahakama kukamilisha kuchapa/kuandaa nakala yako ya hukumu. Basi hiyo nakala iliyogongwa muhuri ni kwa ajili hii na ni  muhimu sana tena sana kubaki nayo.

Barua ya kuomba nakala ya hukumu utaiwasilisha katika mahakama ileile ambayo iliamua kesi au shauri lako.Gharama zake ni bure  kwasasa kwa maelekezo ya jaji mkuu. Hakuna malipo.

Maelezo mengine kuhusu nakala ya hukumu kwa ujumla,umuhimu wa kuiomba na hasara za kutoiomba yalielezwa katika makala yaliyopita.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment