Thursday 10 May 2018

NINI UFANYE IKIWA MNUNUZI WA ARDHI YAKO AMESHINDWA KUMALIZIA MALIPO.





Image result for KIWANJA KINAUZWA

NA BASHIR  YAKUB -

Ume;muuzia mtu kiwanja au nyumba. Mmeandika mkataba na kuusaini tena mbele ya mwanasheria. Kwenye mkataba mmeweka vipengele vingi  lakini kimojawapo kinahusu umaliziaji wa pesa ya manunuzi.  Hii ni kwasababu mnunuzi amelipa kiasi kidogo na kiasi kingine ameahidi kwenye mkataba kukimalizia baada ya muda fulani.

Mkataba umesainiwa na umekamilika. Mda umeenda na kufika ule ambao mnunuzi alitakiwa kumalizia kiasi kilichobaki  lakini bado haoneshi dalili za kumalizia kiasi hicho.  Umejaribu kumkumbusha mara kadhaa lakini maneno yake ni yaleyale  na pesa halipi.  Muda mlioahidiana sasa umepita lakini bado  mnunuzi hajamalizia hela .  Na pengine sasa hapokei hata simu  au hujui aliko au anatoa majibu ya dharau au yasiyoridhisha au vinginevyo.

Nini ufanye katika mazingira kama haya, zipi haki zako, ipi hadhi ya mkataba wenu wa mauziano ambao uliusaini nk, nk. Tutaona hapa chini.

1.KUHUSU KUUZIANA NA KUBAKI NA DENI.

Sheria haikatazi kuuziana ardhi na likabaki deni. Suala hilo limeachwa katika hiari ya muuzaji na mnunuzi.Ni wao watakoamua kuhusu kulipa hela yote au kulipa kiasi na kubaki na deni.  Kifungu cha 10 cha Sheria ya Mikataba kimesema  mkataba ni halali ikiwa umefanywa na wahusika timamu/kamili,huku wakiuziana kitu halali, na kwa masharti  halali ya kisheria.

 Basi madhali haya yametimia  jambo la kubaki na deni halikatazwi kisheria.

2. KUSHINDWA KUMALIZIA DENI.

Kushindwa kumalizia deni ndani ya muda ambao umeainishwa  ndani ya mkataba kwa ufupi ni kuvunja mkataba. Unapovunja sharti katika  mkataba ni umevunja mkataba. Basi kwa mazingira ya namna hii mnunuzi anakuwa amevunja mkataba.  Kifungu cha  39  cha Sheria ya Mikataba kinasema kuwa  kushindwa kutekeleza yale yaliyokubaliwa katika mkataba  ndio kufa kwa mkataba .

Kwahiyo ni vema mnunuzi ambaye hajamaliza ahadi yake ya kimkataba kufahamu kuwa amevunja mkataba na hivyo ameua mkataba.

3. NINI UFANYE IKIWA PESA HAIJAMALIZIWA.  

Ikiwa muda umepita na mnunuzi hajamalizia hela  basi kifungu cha 73 cha  sura ya 113  sheria Namba 4 ya ardhi  kimekupatia majibu kuwa unaweza kufanya haya ;-

( a )Unaweza kurejea katika umiliki kwa amani bila kupitia/kutumia mamlaka/taasisi yoyote( resume into possession peaceably). Utakachotakiwa kufanya ni kumpa taarifa ya maandishi mnunuzi kuwa kwakuwa ameshindwa kutekeleza ahadi iliyo kwenye mkataba basi narejea tena katika umiliki wa shamba,kiwanja ,au nyumba yako.Na utarejea kweli.

( b ) Kurejea katika umiliki kwa kuitumia mahakama. Hapo juu unarejea katika umiliki bila kuihusisha mahakama wakati hapa unaitumia mahakama kurejea katika umiliki.  Njia hii ya pili unaweza kuitumia pengine kwakuwa mnunuzi ameshaanza kulitumia eneo na hivyo ukaona ni vigumu kurejea katika umiliki bila nguvu ya sheria, au namna nyingine ambayo unaona ni vigumu kuurejea umiliki kwa amani.

( c ) Unaweza kufungua shauri la madai ya hela ya kiasi kilichobaki.  Hapa unaamua kutorejea katika umiliki lakini unachotaka ni kiasi kilichobaki tu umaliziwe na mambo yaishe. Njia hii  haipo kwenye sheria ya ardhi bali sheria ya mikataba na katika madai ya kawaida.

( d ) Unaweza kumtafuta msuluhishi(mediator) kumaliza tofauti zenu. Msuluhishi anaweza kuwa yule aliyetajwa katika mkataba wenu au yeyote ambaye hakutajwa ambaye mtamridhia asuluhishe.Wakili, hakimu au jaji anaweza kuwa msuluhishi mzuri kwa kumtumia kama mtu tu wa kawaida bila kutumia utaratibu wa kawaida wa kufungua kesi.

( e ) Unaweza kusamehe deni kwa maandishi ikiwa utaona inafaa kufanya hivyo. Haikatazwi kusamehe deni.

4. FIDIA.

Ikiwa utaamua kutumia njia yoyote hapo juu unaweza pia  kudai  fidia kama nyongeza ya hicho unachodai.  Kifungu cha 73( 2) cha Sheria ya ardhi kimesema hivyo. Fidia ni kwasababu huyu amevunja mkataba. Fidia ni nyongeza  tu wala haipunguzi kile unachodai.


MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA  JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment