Wednesday 21 March 2018

USHAHIDI WA DAKTARI KUHUSU SABABU ZA KIFO .


Image result for USHAHIDI WA DAKTARI

NA  BASHIR  YAKUB- 

Unaweza kuwa wewe, ndugu yako,rafiki au  jamaa yako ameunganishwa katika kesi ya mauaji. Aghalabu, daktari anasubiriwa kutoa ushahidi mahakamani kuhusu sababu za kifo cha marehemu. Na ni ushahidi huo wa daktari utakaokuondoa katika kesi  hiyo ya mauaji au utakuingiza katika kesi hiyo na hivyo kutiwa hatiani na kuadhibiwa.

Lakini sio daktari tu bali wenye kesi wote ambao ushahidi wake unahitaji mtaalam(expert) kuthibitisha mfano mkemia, mtaalam wa muandiko na sahihi, mtaalam wa biashara , mtaalam wa DNA  nk.

1.USHAHIDI WA DAKTARI.

Kifungu chac 47 cha Sheria ya Ushahidi kinaruhusu kutumika na kukubalika kwa ushahidi wa mtaalam( expert). Mtaalam ni pamoja na daktari.

2. MAMBO  6  MUHIMU UNAYOTAKIWA KUJUA.

A ).  Kabla daktari au mtaalam mwingine yoyote hajaanza kutoa ushahidi wake ni ni muhimu sana athibitishe kwa ushahidi kuwa yeye ni mtaalam kweli (expert) kwa hicho anachotaka kutolea ushahidi. Usikubali akaanza  kueleza kabla ya kuthibitisha utaalam.Mtake athibitishe hilo kwanza.

Utaalam unathibitishwa kwa taaluma(professional). Kama ni daktari na mtaalam wa eneo fulani la tiba ,mfano mifupa, moyo, nk, aoneshe cheti cha taaluma katika eneo hilo. Halikadhalika kwa wataalam wengine nao wanatakiwa kufanya hivyo. Kama hawezi kuthibitisha hilo basi hiyo ni faida kwako kwakuwa ushahidi wake ni wa kutia shaka.

Na hapo haijalishi mtaalamu(expert) huyo ameletwa na nani. Awe ameletwa na polisi, PCCB, au idara nyingine yoyote. Msimamo huu ulitolewa na mahakama  katika kesi ya MUHAMMED AHMED V REPUBLIC(1957)E.A. C.A 523.
B ). Daktari au shahidi yoyote mtaalam, asiwe tu mtaalam wa vyeti, bali awe mwenye ujuzi wa uzoefu wa kazi husika. Kwa mfano, daktari au mtaalam ambaye amemaliza chuo, ana cheti lakini hajaajiriwa wala kuwahi kuifanyia kazi taaluma yake popote hawezi kuitwa mtaalam mwenye uwezo(competence) wa kutoa ushahidi wa kitaalam.

Hakikisha unahoji  uzoefu katika taalum husika(practice) . Kama hana sifa hiyo basi ni faida kwako kwani ushahidi wake ni wa mashaka. Lakini ni baada yako kulihoji  hili, ili liingie katika kumbukumbu za mahakama. Huu ni msimamo wa mahakama katikas  kesi ya GATHERU s/o NJAGWARA v R(1954)E.A.C.A 384.

C ). Hata kama kinachotolewa ushahidi kinajulikana kwa kila mtu, bado anayetakiwa kukitolea ushahidi ni mtaalam.
Kwa mfano katika kesi ya  SALUM HARUNA v R (1968)HCD 37, askari alitoa ushahidi kuwa alichomkamata nacho mtuhumiwa ni bangi. Mahakama ya wilaya ilikubali ushahidi huo na kumtia hatiani. Kwenye rufaa  mahakama ilibatilisha hatia hiyo na kusema kuwa , askari ambaye si mtaalam wa madawa ya kulevya  hawezi kuijua bangi.

Hivyo hakikisha si tu shahidi anakijua kitu hicho, bali pia ni mtaalam wake(expert). Kama si mtaalam hata kama anakijua kitu hicho bado hakijua mbele ya sheria. Ndio maana utaona polisi wanasema “kitu chenye ncha kali” “kitu kigumu” nk. Wanajua ni panga au jiwe lakini hawasemi kwakuwa si wataalam (expert) wa kusema hivyo.

D ).Mtaalam asiseme  kwa akili yake mwenyewe(personal knowledge)  bali aseme taaluma au sayansi inavyosema kuhusu jambo husika. Kwa mfano asitumie maneno kama “mimi ninavyojua”, “ nionavyo mimi”, “ushauri wangu”, “nafikiri”, bali aseme “ sayansi inasema hivi”, “ kitaalam jambo hili liko hivi” nk.Huu ni msimamo katika kesi ya LONGINUS KOMBA v R (1973) LRT 39.

E ).Pia aeleze amefikiaje jibu lake(conclusion). Ni kama ilivyo kwenye hesabu ambapo si tu unatakiwa kuonesha jibu, bali njia uliyotumia kufikia hilo jibu. Lengo ni hiyo njia ihojiwe kuona kama inaweza kuzaa jibu sahihi au laah.

F  ). Mahakama hailazimiki kukubaliana na ushahidi wa mtaalam hata kama jaji au hakimu sio mtaalam wa hicho kitu kilichotolewa  ushahidi.  Kwa hakimu au jaji ushahidi wa mtaalam(expert) ni maoni tu na sio hukumu.Ataamua kuyabeba au kuyatupa. Ni msimamo wa mahakama katika kesi ya  HASSAN SALUM v R (1964) E.A 126.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com




0 comments:

Post a Comment