Tuesday 13 March 2018

KUPOTELEWA NA NYARAKA INAYOHITAJIKA MAHAKAMANI KAMA USHAHIDI.

Image result for NYARAKA


NA BASHIR YAKUB -

Inaweza kuwa nyaraka  muhimu kama hati ya nyumba, mkataba wa mauziano au mkataba mwingine wowote, wosia, kadi ya gari au ya mashine yoyote,hati ya kusimamia mirathi, cheti cha ndoa au vyeti vinginevyo, na nyaraka nyingine mbalimbali.

Nyaraka hii  inaweza kuwa inatakiwa  sehemu muhimu kama mahakamani  ili kuthibitisha shauri au kesi yako. Na inaweza ikawa ni nyaraka ambayo kuwepo kwake ndio kushinda kwako na kutokuwepo kwake  ndio kushindwa kwako.

Pamoja na umuhimu wa nyaraka hii bado umeitafuta kote pa kutafuta na hukuweza kuipata. Au hukuitafuta madhali tu unajua ilishapotea au iko mikononi mwa mtu ambaye hujui alipo na hawezi kupatikana. Katika mazingira ya namna hiyo makala yataeleza vitu vichache vinavyoweza kusaidia kutoka Sura ya sita,Sheria ya Ushahidi.

1.   USHAHIDI WAKO.

Kitu kikubwa  kinachomsaidia mtu kushinda kesi mahakamani ni ushahidi. Kadhalika kushindwa kwako pia ni ushahidi. Ukisema hiki kiwanja au  nyumba ni yangu unatakiwa kuonesha hati au mkataba wa mauziano au vyote viwili. Ukisema hili gari ni langu kadhalika uoneshe kadi yenye jina lako ama vinginevyo. Ukisema nilikuwa na ndoa halali uoneshe cheti cha ndoa ama vinginevyo. Ukisema nilimuuzia au kununua kitu fulani uoneshe mkataba ama risiti,vivyo hivyo nk, nk.

Hakimu au Jaji si mtu ambaye anakuwa eneo la tukio na hivyo kuwa katika nafasi ya kujua nini kilitokea huko. Yeye hajui chochote kilichotokea na hivyo taarifa zote anazipata kwenu mnaoshitakiana. Kwa msingi huu yupo katika wakati mgumu kuamua nani yuko sahihi na nani hayuko sahihi kwa kitu ambacho hakushuhudia na hakijui.

Kama hivi ndivyo kitu pekee cha kumuongoza hakimu/jaji huyu ambaye hakuwepo wakati mnadhulumiana, ni ushahidi wa kila mmoja atakaowasilisha. Hataangalia suraya mtu, kulia machozi kwa mtu, kuongea kwa kujiamini au kwa unyonge kwa mtu, umri wa mtu, rangi ya mtu,wala jinsia, bali ushahidi ulio uliowasilishwa na mtu.

2. MAMBO MAWILI YANAYOWEZA KUKUSAIDIA IKIWA UMEPOTEZA NYARAKA.

Jambo la kwanza,  lipo kifungu cha65 ( a ) ,( b ) na ( c ) cha Sheria ya Ushahidi. Ni uwepo wa nakala(kopi) ya nyaraka halisi(orijino). Kama umepoteza orijino lakini ipo kopi au unajua sehemu ambayo unaweza kupata kopi basi inaweza kukusaidia.

Ndio maana ni muhimu kuwa na kopi ya kila nyaraka ambayo una orijino yake. Kifungu cha 63 cha Sheria ya Ushahidi kinasema kuwa nakala isiyo halisi/kopi inaweza kutumika kuthibitisha jambo.  Lakini pia vitu vingine vinaweza kuhitajika kuthibitisha kupotelewa na nakala halisi kwa mfano taarifa ya polisi ya kupotelewa nk.

Jambo la pili, linaloweza kukusaidia lipo kifungu cha 65( e ) cha Sheria hiyohiyo ya Ushahidi. Ni kumleta shahidi ambaye anakumbuka na kujua kile kilichokuwa kimo/kimeandikwa katika nyaraka hiyo ambayo haionekani.

Anaweza kuwa mtu aliyeiandaa, aliyeishuhudia,aliyeisoma, au yeyote ambaye kwa uhakika alijua nini kilichokuwa kimeandikwa ndani mwake. Kazi yake itakuwa ni kueleza nini kilikuwa kimo/kimeandikwa humo na atahojiwa na kuulizwa kuhusu hicho alichosema. Hili nalo laweza kusaidia.  

Na kama hivi vyote havipo, basi  kuthibitisha kwaweza kukuwa vigumu kidogo na hivyo kujikuta unapoteza hata kama haki ni yako.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com




                   

0 comments:

Post a Comment