Tuesday 27 March 2018

BUBU ANAPOKUWA SHAHIDI MAHAKAMANI.



Image result for SHAHIDI KIZIMBANI
NA  BASHIR  YAKUB -

Bubu yaani mtu asiyeweza kuongea  anaweza kuwa shahidi mahakamani iwapo ameshuhudia tukio. Kutokuwa na uwezo wa kuongea hakumwondolei sifa ya kushuhudisha kile ambacho amekishuhudia. Ikumbukwe ushuhuda unatokana na  na hatua ya mtu kuona, kusikia, kuhisi, kugusa, au  utambuzi wa tukio kwa namna yoyote  ambao umetokana na kiungo cha mshuhudiaji.

Yumkini, bubu wengi hawasikii. Na tumeona hapo juu kuwa ushuhuda ni pamoja na kusikia. Hata hivyo pamoja na kutosikia kwao bado wanavyo viungo vingine vya mwili ambavyo wanaweza kuvitumia kushuhudia tukio. Viungo hivyo ni pamoja na macho, mikono kugusa, ulimi kuhisi,akili katika utambuzi nk.

1.  SHERIA KUHUSU BUBU SHAHIDI.

Kifungu cha 128( 1 )  cha Sheria ya Ushahidi, Sura ya 6 kinasema kuwa  mtu ambaye  hawezi kuongea(bubu) anaweza kutoa  ushahidi wake  katika namna nyingine ambayo itaweza kuwa fanisi na ya kueleweka.  Njia fanisi na ya kueleweka ni kama kupitia maandishi/kuandika ikiwa anao uwezo wa kuandika, na kwa ishara ikiwa anao uwezo wa kutumia ishara.

Wengi tunajua ishara kama njia kuu ya mawasiliano kwa bubu. Basi hiyohiyo inaweza kutumika kwa bubu kutoa ushahidi.

2.  HALI IKOJE KAMA HAKIMU/JAJI HAELEWI  ISHARA YA BUBU.

Bubu anapotoa ushahidi wake kwa ishara panatakiwa pawepo mtu ambaye atatafsiri ishara zile kwa maneno. Hata kamaHakimu/Jaji angekuwa na uwezo wa kujua ishara za bubu bado mtu anayetafsiri anatakiwa kuwepo. Hii ni kwasababu mahakamani hayupo hakimu tu. Bali wapo wapo wengine kama upande wa mashtaka , upande wa utetezi ambao wangependa kujua nini bubu anaongea katika ishara zake ili wapate kumuhoji na kumuuliza maswali kuhusu kile alichoongea.

Hata hivyo mahakama ina hiari ya kupima kile ambacho anafasiri  mfasiri ili naye asije akapotosha au kuingiza yake . Na kwa msingi huu ndio maana mahakama hailazimiki kukubaliana au kubanwa na kile alichoongea/alichofasiri mfasiri.

Katika kesi ya HAMIS v REPUBLIC . 18 EACA. 217,  dada wa bubu aliiambia mahakama kuwa yeye anaelewa vizuri ishara za mdogo wake ambaye ni bubu na hivyo  akasema atasaidia kutafsiri wakati mdogo wake akitoa ushahidi.
Mahakama ilimruhusu atafsiri ushahidi wa mdogo wake. Lakini katika hukumu mahakama ilisema kuwa imeukataa ushahidi wa bubu kwakuwa tafsiri iliyotolewa dada yake  ilikuwa haieleweki.

3.  JARIBIO KABLA BUBU HAJATOA USHAHIDI.

Bubu hustahili kujaribiwa kabla ya kupokelewa ushahidi wake. Jaribio hulenga kujua kama anajua alichokuja kufanya mahakamani  na kama anao uwezo wa kujibu kile anachoulizwa kwa usahihi. Jaribio hufanyika kwa kumuuliza maswali na kuona kama anaweza kutoa majibu yanayoendana na maswali hayo(capability of giving rational answers).  Ikiwa ana uwezo huo basi huchukuliwa kama shahidi kamili( competent witness).

Na kama hawezi kujibu sawa na kile anachoulizwa basi hawezi kuchukuliwa kama shahidi kamili. Basi, hayo ni machache kuhusu bubu kuwa shahidi.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com





2 comments:

  • LEGAL AID CLINIC says:
    14 May 2018 at 06:08

    Umetoa elimu nzuri lakini pia ni kusahihishe Kidogo mwanasheria msomi katika sheria za watu wenye ulemavu ziwe za kimataifa na kitaifa ni kosa kumuita mtu mwenye ulemavu jina la hilo tatizo lake hayo majina yamekuwa yenye kunyanyapaa mfano mtu asieweza kuongea kumuita bubu kama ulivyo ita juu ya title yako

  • LEGAL AID CLINIC says:
    14 May 2018 at 06:11

    Umetoa elimu nzuri lakini pia ni kusahihishe Kidogo mwanasheria msomi katika sheria za watu wenye ulemavu ziwe za kimataifa na kitaifa ni kosa kumuita mtu mwenye ulemavu jina la hilo tatizo lake hayo majina yamekuwa yenye kunyanyapaa mfano mtu asieweza kuongea kumuita bubu kama ulivyo ita juu ya title yako

Post a Comment