Tuesday 10 October 2017

MAMBO SITA MUHIMU UNAPOPEKULIWA NA ASKARI.


Image result for POLISI  WAKIPEKUA

NA  BASHIR   YAKUB - 

Unapopekuliwa  yapo  mambo  ambayo  usipoyazingatia  wewe  unayepekuliwa  basi  yatakuingiza  matatani  mbeleni  au   hata  kama  umebambikiziwa  kosa  itaonekana ni  kweli    na  waweza  kwenda  jela  bila  kuwa  umetenda  kosa lolote.

Kawaida  wanaopekua  ni  askari.  Usitarajie  huyu  anayekuja  kukupekua  awe  ndiye  wa  kukwambia  haki  zako . Badala  yake wewe  unayepekuliwa  ndiye  uwe  wa  kumwambia  askari  kuwa  hiki  ndicho  hiki  hapana.  Askari  anapokuja  kukupekua  tayari  wewe  unashukiwa na  hivyo ni  rahisi   kwake  kuacha kufuata  au  kuongeza jambo lisilokubalika  ilimradi  atimize  lengo  lililomleta. Wewe  ndiye  wa  kusema  hili  ndio  na  hili  hapana.

Hivyo  basi  ni muhimu  sana kwako  kujua  kuhusu  kupekua  na  mambo  gani  ya  msingi  ufanyiwe  au  usifanyiwe  ili  kuepuka uwezekano  wa kwenda  jela  bila  kosa.
Usiseme  mimi  sina haja  ya  kujua  kuhusu  kupekua  kwasababu  ni  mwema  sana  na  hivyo si  rahisi  kutakiwa  kupekuliwa. Laa  hasha, kupekuliwa  na  kukamatwa  na  polisi  humkumba  yeyote  awe mwema  ama  vinginevyo. Kujua  ni  silaha  na  hivyo  ni  muhimu  kukaa  na silaha  hii.  

Makala  yatapitia  sura  ya  20, vifungu  vya 38 hadi 45 vya  Sheria  ya Mwenendo  wa  Kesi  za  Jinai .  

1.NANI  ANARUHUSIWA  KUKUPEKUA.

Askari  ndiye  anayeruhusiwa kukupekua. Hata  raia  wanaweza  kumzuia  raia  mwenzao  wakampekua  ikiwa  wana  taarifa  kuhusu kuficha  au  kumiliki kitu  ambacho  ni  kosa  kwa  mujibu  wa  sheria.  Isipokuwa  ni  haramu  kabisa  kwa  raia  kumpekua  raia  mwenzake  bila   kuwa  na  kibali  maalum.

2.   VITU  GANI  VINAWEZA  KUPEKULIWA.

Mtu  kama  mtu  anaweza  kupekuliwa,  kwa  maana  nguoni  mwake  kama  mifukoni  nk. Pia  vifaa  kama  gari,  ,meli, nk  navyo  vyaweza  kupekuliwa.  Halikadhalika  nyumba  kama  nyumba nayo  yaweza  kupekuliwa  pamoja  navyo  vifaa  vingine.

3.  JE  WAWEZA  KUPEKULIWA  MDA  WOWOTE.

Hapana,  si  kweli  kuwa  waweza  kupekuliwa  mda  wowote  anaotaka  askari.  Sheria  niliyotaja  hapo  juu  inasema  mda  wa  kupekua  ni  kuanzia   jua  linapochomoza  na  mwisho  ni  linapozama.  Yametumika  maneno  jua  kuchomoza  na  kuzama   badala  ya  kutaja  mda labda  saa  11  za  asubuhi  mpaka  saa  12  za  jioni  kwasababu  ya utofauti wa  jiografia  ya  sehemu  na  sehemu.

Muonekano  wa  saa  12  za  jioni  wa  kanda  ya  ziwa  ni  tofauti  na  ule  wa  pwani  nk.  Kwahiyo  kutaja  saa  kwa  lengo  la  kumaanisha  usiku  unapoingia  na  unapotoka ingekuwa  kama  inapotosha.

Hata  hivyo  inawezekana  tu  kupekuliwa nje  ya  muda  huo  kwa  kibali maalum  cha  mahakama.

4.  MPEKUAJI  KUAMBATANA  NA  SHAHIDI  MWENYEJI.       

Askari  anayepekua  aje  na  shahidi mwenyeji.  Mjumbe au  kiongozi  kutoka  serikali  za  mitaa ni  mtu  muhimu  kuwa  mwenyeji. Jirani  pia   anaweza kuwapo.  Hii  ni  kuhakikisha  wanakuwa  mashahidi  kuwa  hakuna  kilichoingizwa  ndani  wakati  kuingia  kupekua  na  pia  kushuhudia  vinavyochukuliwa.

5.  ORODHA  YA  VITU  VINAVYOCHUKULIWA.

Ni  lazima  kila  kinachochukuliwa  kuandikwa  kwenye  orodha  maalum .  Orodha  hiyo utaisaini  wewe  uliyepekuliwa,  askari  aliyekupekua, pamoja  na  mashahidi  ambao  ni  mjumbe au  serikali  za mitaa  au  jirani  mwema.

Hii  huepusha  badae  kuambiwa  kuwa  hata  kitu fulani  ambacho  kinajenga  kosa  kuwa kilikutwa  kwako. Lakini  pia  ni  muhimu  kwa  ajili  ya  kurejesha  mali  zako  baadae  zikiwa  zimetimia.

6.   KIBALI  CHA  KUPEKUA.

Askari  mwenye  cheo  chini  ya  Sub Inspector  haruhusiwi  kupekua  nyumba  au  eneo  la  mtu  bila  kibali  maalum aidha  kutoka  mahakamani  au  kutoka  kwa  mkubwa  wake  mwenye  cheo  cha  Sub  Inspector  kwenda  juu.   Hii  ni  kwa  kesi  ya  kupekua  nyumba.

Kwa  kesi  ya  kupekua   mtu  binafsi  pale  anaposimamishwa  au  upekuzi  wa  gari  na  vifaa  vingine  askari  yeyote    anaweza  kupekua  bila  kibali.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

2 comments:

  • chizcom says:
    11 October 2017 at 06:15

    tatizo la polisi ukijua sheria ya haki zako,ndivo unavo jitengenezea mazingira magumu kuwa adui yake

  • Mwagalilu says:
    5 September 2021 at 05:37

    Good

Post a Comment