Monday 25 September 2017

KUPATA ZUIO LA MAHAKAMA.


Image result for ZUIO LA MAHAKAMA
NA   BASHIR   YAKUB - 

1.ZUIO  LA  MAHAKAMA  NININI.

Ni  amri  inayotolewa  na  mahakama  kumzuia  mtu  kutofanya  jambo  fulani  kwa  muda. Kampuni  nayo  ni  mtu  ambapo  yaweza  kuomba  zuio  au  kuzuiwa. Aidha yeyote  ana  haki ya  kuomba  amri  hii  ikiwa  anaona  kuna  jambo  fulani  linafanyika  na  ikiwa  litaendelea  kufanyika  basi  litaharibu  au  kupoteza  kabisa  kitu  fulani.

Kwahiyo  zuio   ni  amri inayobeba  maagizo  maalum  kwa  mtu  au  watu  maalum kuwaamrisha  kutoendelea  na  kitu  fulani  kama  tulivyoona  hapo  juu.Sheria  ya  Mwenendo  wa Madai,  Sura  ya  33 na  Sheria  nyingine  mtambuka zimeongelea  kuhusu  zuio.

2.   KATIKA   MATUKIO   GANI  UNAWEZA  KUOMBA  ZUIO.

( a ) Kwa  mfano, umeshindwa  kulipa  mkopo  na  tayari  una  taarifa  kuwa  benki au  taasisi  yoyote  ya  fedha  inataka kwenda  kuuza  na  unahisi  kuna  pahala   hapaendi  sawa katika  mikataba yenu.
 Basi  unaomba  zuio  ili  hiyo  mali  yako  uliyoweka  rehani  isiuzwe  mpaka  hapo  hilo eneo  ambalo  mmeshindwa  kuelewana  litakapopatiwa  majibu.

( b ) Kwa mfano, umemuuzia  mtu  gari, pikipiki,  au  mashine  yoyote.  Mtu  huyo  hajalipa  kiasi  cha  pesa  iliyobaki kama  mlivyokubaliana. Lakini  anaendelea  kutumia  kifaa  hicho. Unaweza  kuomba   kumzuia  kuendelea  kutumia  mpaka  atakapolipa  kiasi  kilichobaki  ili  asiendelee  kuharibu  au  kuzeesha  kifaa  hicho.

( c ) Kwa  mfano, we  ni  mpangaji  katika nyumba ya kuishi  au  biashara.  Mwenye  nyumba,eneo anataka  kukutoa  kwenye  pango  hilo  bila  kufuata  utaratibu  au  kwa  kukiuka baadhi  ya  makubaliano  kwenye  mkataba  wenu. Unaweza  kuomba  zuio asiendelee  kukutoa.

Pia  mazingira  mengine  yoyote  ambayo  unahisi  kuna  kitu, jambo  linataka  kuharibiwa  au  kuingiliwa, kuuzwa, kupotezwa,kufichwa  kinyume  na  utaratibu  unaweza  kuomba  zuio  hilo.

3.   SHARTI  KUU  .

Ili  uweze  kuomba  zuio  ni  lazima  pia  kuwepo  na  shauri  la  msingi.  Kwa  maana  utafungua  shauri  la  msingi  kulalamikia  jambo  fulani  halafu utaomba  zuio  ndani  ya  shauri hilo.  Kwa  mfano  unafungua  shauri  kulalamikia  mwenye nyumba  kusitisha  mkataba  wa  pango  bila  kufuata  utaratibu.

Hilo  ni  shauri  kuu.  Halafu  ndani  mwake  unafungua  shauri  dogo  la  kuomba  zuio ili  asikuondoe  katika  nyumba  mpaka  kwanza  shauri  kuu  la  kukiuka  utaratibu  litatuliwe.        

Kwahiyo  ni  sharti  kuwapo  shauri  kuu  ukilalamikia jambo  fulani  halafu ndani  mwake  ndio  uombe  zuio.

4.  UMUHIMU  WA  ZUIO.

( a ) Linasaidia  mali yako  kutouzwa  au  kutoondolewa  kwenye  nyumba  kama  mgogoro  unahusu  nyumba.

( b ) Linalinda  mali  yako  isiharibiwe ,isifichwe, isihamishwe,isiingiliwe  kwa  namna  yoyote  ile  kama  ipo  katika  mazingira  hayo.

( c ) Linakupa  nafasi  ya  kutafakari  na  kujipanga  ikiwa  upo  katika  presha  ya  kukimbizana  na  jambo ama  mgogoro.

( d ) Linatoa  mwanya  wa  mazungumzo  kati  ya  mlalamkaji  na  mlalamikiwa.

5.  WAPI   UKAOMBE  ZUIO.

Zuio  linaombwa  mahakamani.  Na  linaweza  kuombwa  mahakama yoyote   katika  shauri  lolote. Linaweza  kuombwa  kwenye  mashauri  ya  ndoa, mirathi,  ardhi,  biashara,  mikataba, madai   ya  kawaida ya  pesa au  mali, makampuni n.k.

Na  linaombwa  katika  mahakama  zote  yaani  ya  mwanzo,  ya  wilaya,  ya  hakimu  mkazi  mahakama  kuu  na  ya  rufaa  pia.  Lakini  pia  linaombwa  kwenye  mabaraza    ya  ardhi  ya  kata  na  wilaya.

6.  KUKIUKA  AMRI  YA  ZUIO.

Ikiwa  utaomba  zuio  na  kupata  halafu  aliyezuiwa  akakiuka  na  kuendelea  na  kile  alichozuiwa  basi   kosa linabadilika  na  kuwa  la   jinai. Inakuwa jinai  ya   kuingilia  amri   na   shughuli  za  mahakama.  Ni  kosa  ambalo   aliyekiuka  amri  hiyo akithibitika   ni  kweli  kakiuka  basi  atatakiwa  kwenda  jela  miezi  sita  ama  vinginevyo.

Kinachotakiwa kwako  ni  kuripoti  tu  kuwa  amri  iliyotolewa  sasa  haitekelezwi   na  yule  aliyeamrishwa  kutekeleza.  Utaripoti  mahakama  hiyo  hiyo  iliyotoa  zuio  hilo.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment