Monday 30 October 2017

KUOMBA NA KUPATA LESENI YA MAKAZI .


Image result for leseni ya makazi
Na  Bashir  Yakub -

1.LESENI  YA MAKAZI  NININI.

Leseni  ya  makazi  ni  leseni/kibali  maalum kinachotolewa  kwa  mmiliki  wa  makazi  ili  kutambua  na  kurasimisha  makazi  hayo.
 Leseni  ya  makazi  ni  nyaraka  ya  umiliki  wa  makazi   kama  ilivyo  nyaraka  nyingine za  umiliki  wa  ardhi.  Leseni  ya  makazi  ni  kwa  ajili  ya  ardhi  makazi  tu  na  si  ardhi  nyingineyo.

2.  JE  LESENI  ZA  MAKAZI  ZINATAMBULIWA  NA  SHERIA.

Ndio, leseni  za  makazi  ni  kwa  mujibu  wa  sheria  namba  4/1999 Sheria  ya  Ardhi.  Leseni  za  makazi  zinatambuliwa  na  kifungu  cha  23  cha  sheria  hiyo. 

Kwahiyo  wanaodhani  kuwa  leseni  za  makazi  ni  mpango  tu  wa  serikali  za  mitaa  na  watendaji  wa  kata  wajue  sio  kweli.  Leseni  za  makazi  ni  nyaraka   iliyo  kisheria  kwa  mujibu  wa  kifungu  hicho  japo  juu.

3.  TOFAUTI  YA  LESENI  YA  MAKAZI  NA  HATI .

Hati ni “Right  Of  Occupancy”  kwa  jina  la  kitaalam,  wakati  leseni  ya makazi ni  “Derivative Right” .  Tofauti  za  viwili  hivi  ni  nyingi  ila kubwa  ya  kukufanya  uelewe  ni  kuwa,  leseni  ya makazi  hutolewa kwa  makazi  ya mjini  ambayo  hayajapimwa  na  hayakuwa   rasmi  lakini  yasiyo  hatarishi.

Wakati hati  hutolewa  katika  makazi  rasmi  na  ambayo  yamepimwa.  Isipokuwa  la  kuzingatia  ni  kuwa   iwe  leseni  ya makazi  ama  hati  vyote  vinatambuliwa  na serikali  kama  nyaraka  rasmi  za  umiliki  na  kila  moja  ina  haki  sawa na  nyingine  katika  umiliki.

4.  NANI  HUTOA  LESENI  ZA  MAKAZI.

Leseni  za  makazi  hutolewa  na manispaa  husika. Iwe  kubadili  jina  au  kupata  mpya  ni  kazi  inayofanywa  na  manispaa  ya  yalipo  makazi  husika.  Hii  ni  kwa  mujibu  wa  kifungu  cha  23( 3) Sheria  ya  Ardhi.

5.  MASHARTI  YA KUPATA  LESENI  YA  MAKAZI.

Kwanza,  muombaji  awe Mtanzania  aliyefikisha  umri  wa  miaka  18  au  zaidi. Pili,  awe  ndiye  mmiliki  wa  makazi  husika. Tatu, eneo  lisiwe  katika  maeneo  hatarishi au  maeneo ya hifadhi. Nne, eneo  liwe  maeneo  ya  mjini. Tano,  yawe ni  makazi  kwa  kipindi  kisichopungua  miaka  mitatu. Sita, lisiwe  eneo  ambalo lina  hati ya  kawaida  au  hati  ya  kimila.   Saba, malipo  ya ada  na  tozo  nyingine zitalipwa  kwa  mujibu  wa  kifungu  cha 23 (3)( c ).

6.  FOMU  INAYOJAZWA  NA  MUOMBAJI.

Muomba  leseni  ya  makazi  anatakiwa  kujaza  fomu  namba  73 kwa  mujibu wa  kifungu  cha  170 Sheria  namba  4  ya  ardhi. Kwenye  fomu hiyo  jina  la  mwombaji  litahitajika, anuani  yake na  ya  makazi, aina  ya  umiliki  anaoomba  kama  ni  binafsi, kundi, familia, kampuni, taasisi nk, taarifa  za  mtaa, kata, wilaya,  taarifa  za  matumizi  ya  ardhi  kwa  sasa, matumizi  mapya  yanayoombewa  leseni, ukubwa wa eneo husika, kutakuwa  na  sehemu ya  maoni  na  mapendekezo ya  mwenyekiti  serikali ya mtaa, sahihi  yako, dole  gumba  na  picha zako.

Fomu  hii  inapatikana kwa  wanasheria, au  manispaa,  au hata  ofisi  nyingine  za kata  wanazo.

7.  MUDA WA LESENI   YA  MAKAZI.

Kifungu  cha  23 (3) ( b ) kinasema  kuwa  leseni  ya  makazi  itatolewa kwa  muda ambao  sio  chini  ya  miezi  sita  lakini  sio  zaidi  ya miaka 5. Kwahiyo  muda  wowote  utakaopewa  kati  ya  muda  huo  utatakiwa   uhuishe ( renew) baada  ya  kuisha  kwake.  
Maana  yake, ukipewa  miaka 2 basi  ikiisha  huisha(renew). Halikadhalika miaka 3, 4 5, 1,miezi 6 ,8, 10 nk.
Kwa  ufupi  haya  yatakufaa.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


2 comments:

  • kulwa ngatigwa says:
    16 March 2019 at 06:55

    Saaafi, kuna mtu alikua anasema hakuna shwria inayosimamia leseni ya makazi

  • Unknown says:
    9 December 2021 at 10:43

    Asante kwa taarifa nzuri kuhusu leseni ya makazi. Nina swali. Mdogo wangu amemilikishwa eneo langu kwa makosa. Nifanyeje kubadili jina lake kuja kwangu?

Post a Comment