Wednesday 6 September 2017

MSIMAMIZI WA MIRATHI ANATAKIWA KUGAWA MALI BAADA YA MUDA GANI ?.


Image result for MSIBANI
NA  BASHIR  YAKUB - 

1.UKOROFI  WA  WASIMAMIZI  WA  MIRATHI.

Baadhi  ya wasimamizi  wa  mirathi  ni  wakorofi.  Baada   ya  kuteuliwa  kwa  jukumu  hilo   hawapendi  kugawa  mali  ili  kila  mtu  achukue  chake. Inapaswa  kufahamika  kuwa  mali  si  za  msimamizi  wa  mirathi .  Mali  ni  za  warithi  halali  isipokuwa  msimamizi  ni  kiongozi  tu.  Kwa  maana  hii  anawajibika  kusikiliza  warithi  wanasema  nini  ili  mradi  kile  wanachosema  kisipingane na  sheria.

Wakati  mwingine  warithi  wanataka  wagawiwe  mali  zao   ili  kila  mtu  endelee  na  maisha  yake lakini  msimamizi  hataki  tena  bila  sababu  za  msingi. Hili  linakuwa  si  sawa  isipokuwa  kama  kuna sababu  za  msingi  za kufanya  hivyo.

Sababu zaweza kuwa labda   anayetaka kugawiwa mali  ni  mtoto  mdogo asiyeweza  kumiliki  mali kwa wakati  huo, ni  mtu  asiye na  akili  timamu kwa  muda  huo,  kuna  shauri  mahakamani kuhusu  hiyo  mirathi  linaendelea, mali hazijakusanywa  zote, kuna  ugomvi  kwa  warithi  kuhusu  mali  ambao  utaathiri  mgao  nk.                      

2. WAJIBU  MKUU  WA  MSIMAMIZI   WA  MIRATHI.     

Kifungu  cha 108(1)  cha  Sheria  ya  Usimamizi  na  Uendeshaji  wa  Mirathi,  Sura  ya  352  kinaeleza  wajibu  wa  jumla  wa msimamia  mirathi. Kifungu  kinasema  kuwa  kazi  kubwa  ya  msimamizi  wa  mirathi  ni  kukusanya, mali  na  madeni  ya marehemu,kutunza  mali  hizo, kusimamia  gharama  za  mazishi  na  msiba, na  kugawa  mali kwa  wanaostahili. Na  kazi  hii yote  ifanyike  kwa  uadilifu  mkubwa.

Kwahiyo  kumbe  moja  ya  kazi  ya lazima  na ya  kisheria  ya  msimamizi wa  mirathi  ni  kugawa mali  kwa  warithi.  Huu  ni  wajibu  ambao  msimamizi  anawajibika  kuutekeleza. Na  atagawa  kwa  mujibu  wa  wosia  au sheria  husika kama  hakuna  wosia. Hagawi  anavyotaka  yeye. Nani  apate  nini  halipo  katika  hiari  yake.

3.  MUDA  WA  KUGAWA  MALI  KWA  WARITHI.

Kifungu  cha  107 cha  Sheria ya  Usimamizi  na  Uendeshaji  wa  Mirathi kinasema  kuwa   ndani  ya  miezi  sita  tokea  kuteuliwa  kwa  msimamizi  wa  mirathi,  msimamizi  huyo  anatakiwa  kupeleka  taarifa(inventory&account)  mahakamani  akionesha  ni  namna  gani  amekusanya  mali  za marehemu,  madeni,  amelipa  gharama  kama  zipo  na  kwa  namna  gani  amegawa kwa  wahusika.

Kwahiyo  kazi  ya  kugawa  yafaa  ifanyike  ndani  ya  miezi  sita.  Hii  ina  maanisha  inaweza  kufanyika hata  ndani  ya  mwezi  mmoja  tokea  kuteuliwa  ikiwa  atakuwa  amekamilisha  taratibu  zote.

Kifungu  kinasema  ikiwa  ndani  ya  miezi  sita  hajapeleka  taarifa (inventory&account) mahakamani na kuna sababu za  msingi  na  za  kisheria  za  kutofanya  hivyo  basi  iwe  ndani  ya  mwaka mmoja. Ikiwa  ndani  ya  mwaka  mmoja  itashindikana kwasababu  za  msingi  na  za  kisheria   basi  anaweza  kuongezewa muda  na  mahakama  hadi miezi  mingine  sita.

Pamoja na  hayo  sheria  hiyo  imetoa  uhuru  kwa mahakama  kutoa  amri  au  agizo  la  kugawa  mirathi  kwa  warithi  halali  katika  muda  ambao  itaona  unafaa  na  kupendeza.  Kuna  muda  mahakama  inaweza kuamrisha  hata  ndani  ya  wiki  tatu  mali  iwe  imegawiwa  na  taarifa  imerejeshwa  mahakamani.
Mara  nyingi  amri  za  namna hii  hutolewa  kutegemea  na  udharula  wa  mazingira  husika  na  kinachohitajika.

4.  NINI  UFANYE  IKIWA  MSIMAMIZI  HATAKI  KUGAWA  MALI.

Ikiwa  msimamizi  hataki  kugawa  mali  na hakuna  sababu  za  kisheria  zinazomzuia kugawa basi  lipo  jambo  moja  unaweza  kufanya.

Ni kutoa  taarifa  katika mahakama ambayo imemteua/kumthibitisha.Utapeleka  malalamiko  yako  hapo  halafu  ataitwa  kwa  wito(summons) na  atatakiwa  aoneshe  sababu(show  cause)  kwanini  hagawi  mali  kama  sheria  inavyotaka. Haufungui  kesi  ila  unapeleka  tu taarifa.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment