Monday 23 May 2016

KUPATA TALAKA FUATA HATUA HIZI.

Image result for talaka

NA  BASHIR  YAKUB - 

Talaka  ni  haki  aliyonayo  kila  mwanandoa. Kama  ilivyo  haki  ya  kufunga  ndoa ndivyo  ilivyo  haki  ya  talaka pia. Yeyote  kati  ya wenye ndoa  anaweza  kuomba  talaka.  Awe  mwanamke  au  mwanaume. Lakini  hii  ni  katika sura  ya  29 ya  Sheria  ya  ndoa na si  katika  imani  ya dini  yoyote.

1.TALAKA  NININI.

Talaka  ni  amri /tamko maalum  la  mahakama  linalotamka  kuhusu kuvunjika kwa ndoa. Hii  ndio  maana ya  talaka  lakini kwa  mujibu  wa  sheria.
Katika  maana hiyo   twapata  kujua  kuwa  talaka  ni  lazima  itolewe  na  mahakama. 

Mahakama  ndicho  chombo   chenye  dhamana  kuu  katika   kubatilisha  ndoa  kwa  namna  ya  talaka.

2.  JE UNAWEZA KUOMBA TALAKA MUDA GANI  BAADA  YA KUFUNGA  NDOA.

Ili  uweze  kuomba talaka  ni  lazima  ndoa  itimize  miaka iwili . Huwezi  kufunga  ndoa  mwezi  huu  halafu mwezi  ujao  ukakimbilia  mahakamani  ukitaka talaka.  Ndoa  ikifikisha  miaka  miwili  basi  haki  ya  talaka  inafunguka.

3.  TOFAUTI  YA  KUTENGANA NA TALAKA.

Sio  kila  kuachana  ni  talaka.  Aina  nyingine  za  kuachana zina  sifa  za  kutengana  na  sio  talaka.  Kutengana  ni hatua  ambapo  wanandoa  wanaacha  kuishi chini ya  paa au  dari  moja.  Wanaweza  kuishi  nyumba  moja  lakini  vyumba  tofauti.Halikadhalika  wanaweza  kuishi  nyumba  tofauti  na  hata  pakawa mbali ya nchi  kwa  nchi, mkoa kwa mkoa,  wilaya kwa wilaya,kijiji kwa kijiji  n.k.

Tofauti  kubwa kati  ya  talaka  na  kutengana  ni  kuwa  katika  talaka  kunakuwa  na  tamko  maalum  kutoka  mamlaka maalum  linalositisha  mahusiano  ya  ndoa,  wakati   katika  kutengana  hakuna  tamko  lolote  kutoka katika  mamlaka  linalotangaza kuisha au kusitishwa  kwa  mahusiano  ya ndoa.

Kutengana  kupo  kwa  aina  mbili.  Kwanza  ni  kutengana  kwa  hiari  ambapo  wanandoa  kwa  hiari  yao  wanatengana,  na  pili  ni kutengana  kwa  kuiomba  mahakama  kuwatenganisha.  Yapo  mazingira  ambapo  kumtenga  mwenza kunaweza  kuwa  kugumu kutokana na mazingira kadha wa kadha na  hapo  ndipo  unapoweza  kuiomba  mahakama  iwatenganishe.

4.  UNAPOHITAJI TALAKA  FUATA  HATUA  HIZI.

(  a ) Hatua  ya  kwanza  kabisa  kabla  ya  kwenda  mahakamani  lazima  upeleke ombi  lako  baraza  la  usuluhishi  wa  migogoro  ya  ndoa. Kwa  waislamu  baraza  hilo  ni  BAKWATA   na  wengine  baraza  hilo  ni  ustawi  wa jamii . Kila  makao  makuu ya wilaya   ustawi  huu  upo  ukiuliza  utaelekezwa. 

Baraza  hili  litajaribu  kusuluhisha  na  likishindwa  litakuandalia  fomu maalum  kuhusu  kushindwa kwake  kusuluhisha. Fomu  hiyo  inaitwa  fomu  namba  3.

( b ) Hatua  ya  pili  utakapokuwa  umepewa  fomu  hiyo  utatakiwa   kuandaa  maombi  ya  kisheria  ya kutaka  kuvunja  ndoa  huku  ukiambatanisha  hati  hiyo.

Katika  maombi  hayo  utatakiwa kuthibitisha uwepo wa ndoa halali, sababu  inayokupelekea  kuomba  talaka, watoto  mlionao  kama  wapo,  na  mali  mlizonazo  kama  zipo.  Mahakama  itasikiliza  na itatoa  uamuzi.

5. JE  NIENDE MAHAKAMA  IPI  KUDAI  TALAKA.

Shauri  la  talaka  ni  shauri  la  ndoa. Na  mahakama  zenye  mamlaka  ya  kusikiliza  mashauri  ya  ndoa  ni  Mahakama  ya  mwanzo, ya  wilaya,  ya  hakimu  mkazi  na  mahakama  kuu.  Unaweza  kufungua  shauri  lako  katika  mahakama  yoyote  kati  ya  hizi. Isipokuwa  ni  lazima  iwe mahakama  ile  iliyo  katika  wilaya  yako na  mahakama  kuu iwe  katika  kanda  yako.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com




3 comments:

  • Unknown says:
    15 January 2022 at 12:28

    Je? Balaza la kata linaweza kutoa talaka kwa wanandoa?

  • Unknown says:
    5 February 2022 at 05:25

    Je,ni lazima uende na cheti Cha ndoa unapenda kufungua maombi ya talaka..?

  • .. says:
    9 August 2023 at 01:31

    Baada ya kuona chapisho kwenye mtandao la Jenna kutoka USA akisema jinsi alivyosaidiwa na Dk. DAWN, niliamua pia kuwasiliana naye kwa msaada kwa sababu sikuwa na chaguo nilichotaka ni kumrudisha mpenzi wangu na furaha. Kwa mshangao mkubwa mpenzi wangu alifika nyumbani akiwa amepiga magoti kwamba nitafute nafasi moyoni mwangu kumsamehe, hakika nilistaajabu na kushtuka mpenzi wangu alipopiga magoti akiomba msamaha na mimi nimkubalie tena. Kweli nimepungukiwa na maneno, na sijui ni kiasi gani cha kukushukuru wewe Dr. DAWN. Wewe ni Mungu aliyetumwa kurejesha uhusiano uliovunjika, Na sasa mimi ni mwanamke mwenye furaha. mawasiliano yake ni Whatsapp +2349046229159
    dawnacuna314@gmail.com

Post a Comment