Monday 12 June 2017

UFAFANUZI MUHIMU KUHUSU USAJILI WA ACCACIA.

Image result for ACACIA TANZANIA

NA   BASHIR  YAKUB - 

Kwa kutumia kigezo cha usajili, Tanzania tunazo aina kuu mbili za  kampuni. Kampuni za ndani(Local companies) na kampuni za kigeni ( foreign companies).

Kampuni za ndani ni zile  zote zilizoanzishwa  hapa nchini na kusajiliwa hapa nchini. Hata kama wanahisa wake wote ni raia wa kigeni kwasababu tu ya kuanzishwa hapa na kusajiliwa hapa zinakuwa ni kampuni  za ndani.

Kampuni ya kigeni ni ile iliyoanzishwa na kusajiliwa nje ya Tanzania lakini ikaanzisha ofisi/biashara/tawi hapa Tanzania. Sheria Na. 12 Sheria ya Makampuni kifungu cha 433 kinasema hivyo. Kampuni kama imeanzishwa nje hata kama wanahisa wake wote ni Watanzania, hapa kwetu hiyo bado ni kampuni ya kigeni.

Kampuni ya ndani inaposajiliwa hupatiwa cheti cha usajili kiitwacho "Certificate of Incorporation" kwa mujibu wa kifungu cha 15(2) Sheria ya Makampuni. Kampuni ya ndani inapopata cheti hiki basi usajili wake huwa umekamilika na inatambulika rasmi kama kampuni ya ndani.

Kampuni ya kigeni inaposajiliwa hapa Tanzania hupatiwa cheti kiitwacho "Certificate of  Compliance" kwa mujibu wa kifungu cha 435(1) Sheria ya Makampuni. Kampuni ya kigeni inapopata cheti hiki basi  usajili wake huwa umekamilika na hutambulika rasmi kama kampuni ya kigeni.

Acacia ni kampuni ya kigeni. Kwa maana kuwa ilianzishwa nje ya Tanzania na kufungua shughuli zake hapa nchini. Kwa hiyo ili ihesabike imesajiliwa Tanzania ilitakiwa kuwa na cheti kiitwacho"Certificate of Compliance". Kutokuwa na cheti hiki maana yake ni kuwa haijasajiliwa Tanzania na haitambuliki.

Nimesikia mjadala BBC SWAHILI leo wanaojadili wakijiuliza inawezekanaje kampuni kubwa kama hii ikafanya biashara bila usajili. Watanzania wengi pia wanajiuliza swali hili.

Jibu lake ni hili. Acacia ni kampuni tanzu(Subsidiary  Company) ya Barrick. Kampuni inakuwa tanzu pale ambapo zaidi ya nusu ya hisa zake zinamilikiwa na kampuni nyingine. Ile inayomiliki huitwa "holding company" na inayomilikiwa huitwa "subsidiary company". Kwahiyo  Barick ni " holding" wakati Acacia ni "subsidiary".

Barrick inamiliki hisa za Acacia 63.9%. Kwa kusema hivi maana yake Barrick ndiye mwenye Acacia. Hata hivyo kwa mujibu wa sheria hizi zinahesabika kampuni mbili tofauti na kila moja inabeba wajibu na hatia zake yenyewe(its own responsibility& liability).

Basi kumbe kilichotokea ni kuwa Acacia walikuwa wakifanya biashara kwa jina la Acacia lakini wakibebwa na mgongo wa  Barrick. Walijificha hapa na wakaweza kuishi bila usajili wa kwao kama wao. Walijibeba kwenye usajili wa Barrick.

Barrick wao wanao usajili na wanayo " Certificate of Compliance" ya kwao ambayo tayari wameitoa hadharani. Kwakuwa haya ni makampuni mawili tofauti kila moja inatakiwa kuwa na cheti chake  kwa mujibu wa kifungu cha 487 Sheria ya Makampuni na kutokufanya hivyo ni kosa kabisa. Kwa hiyo hivi ndivyo ilivyowezekana kampuni hii kufanya biashara bila usajili miaka hii yote.

Adhabu ya kosa kama hilo ni kifungo jela. Sheria Na. 12 Sheria ya Makampuni iliyofanyiwa Marekebisho mwaka 2002, kifungu cha 472 kinasema hivyo.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment