Monday 5 June 2017

JE ULIPEWA NOTISI YA SIKU 60 KABLA BENKI HAIJAUZA NYUMBA/KIWANJA CHAKO ?.


Image result for MKOPO
NA  BASHIR   YAKUB - 

Wanaokopa  hela  kwenye  taasisi  za  fedha  wanatakiwa  kujua  haki  walizonazo. Haki  kabla  ya  kuchukua mkopo,  haki  wakati  wa  kuchukua  mkopo,  haki  wakati  wa  kurejesha,  na  haki  baada  ya  kurejesha au  kushindwa  kurejesha. Hautakiwi  kusubiri  taasisi  iliyokukopa  iwe ndiyo ya  kukueleze  haki  ulizonazo  bali  watakiwa ujue   haki    hizo  kwa  jitihada  zako.

Taasisi  ya  fedha  inaweza  kukueleza  baadhi  ya  haki  lakini  ni  muhali  kukueleza  haki  ambazo  wao  zinawabana. Watakueleza haki  ambazo  hazina  madhara  kwao. 
Basi  yakupasa  ulijue  hili.

Masuala  ya  kuweka  rehani  ili  upate  mkopo  yanaongozwa  na  sheria  mbili.  Sheria  namba  4  ya  mwaka  1999    Sheria  ya  ardhi,  pamoja  nayo  Sheria  namba  17  Sheria  ya  rehani  ya  mwaka  2008. Humo  zimo haki  nyingi  za  mtoa  mkopo   wakadhalika  mchukua  mkopo.  Hata  hivyo  tutatizama  haki  moja  tu ya   notisi  kabla  ya  kuuzwa kwa   nyumba/kiwanja  cha  mkopaji.       

1.KUSHINDWA  KUREJESHA  MKOPO.

Kifungu  cha  127 ( 1 ) cha  sheria  ya  ardhi  kinaeleza   habari  ya  kushindwa  kurejesha  mkopo. Kifungu  kimeieleza  habari  hii  ikiwa  miongoni  mwa  mambo  ambayo  yanachukuliwa  kama ukiukwaji wa  masharti  ya  mkataba  wa  mkopo. 

Mengine  ambayo  yanachukuliwa  kama  ukiukwaji  wa  masharti   ya  mkopo  ni  kuweka  rehani  mara  zaidi  ya  mmoja  kwa  taasisi  tofauti, kuuza, kupangisha  wakati  kuna  rehani  bila  taarifa   au  ridhaa kutoka  kwa  mtoa  mkopo n.k.  Hata  hivyo   haya  na  mengine  yatachukuliwa  kama  kukiuka  masharti  ya  mkopo  ikiwa  yamekatazwa  katika  mkataba  wako  na  taasisi  ya  fedha.

Pia  kwa  mujibu  wa  kifungu  hicho  kushindwa  kurejesha  mkopo  kunajumuisha  pesa  kamili  uliyoikopa,  riba, pamoja  na  makato  mengine  ambayo  yanajenga  sehemu  ya  mkopo.

2.  NOTISI  YA  SIKU  60.

Hii  ni  notisi   ya  lazima  kabla  nyumba/kiwanja  chako  hakijauzwa.  Si  tu  lazima upewe  bali  pia ni  lazima   iwe  ya  siku  60. Kamtindo  ka  kuwapa  watu  siku  14  au  chini  yake  au  zaidi  kidogo  kanakiuka  sheria. Na  hapo  baadae   tutaona   ufanye  nini  ikiwa  hilo  limekiukwa.

Kifungu  cha  127( 1 ) ( a ) kimeeleza  kuwa   pale  mkopaji  anapokuwa  ameshindwa  kurejesha  kwa mujibu  wa  makubaliano  ya  mkopo   basi  taasisi  ya  fedha  itampa  mkopaji  taarifa( notice)  ya  siku  60  ambapo  siku  hizo  zikiisha   kabla  mkopaji  hajalipa   basi  taasisi hiyo  inaweza  kuendelea  na  hatua  za  kuuza  ikiwa  itaamua  kufanya  hivyo.

Kwahiyo  ni  lazima  kuwepo  na  taarifa  ya  siku  60. Na  siku  hizo  zinaanza  kuhesabiwa  tokea  siku  ulipopokea  notisi  ya  kwamba  umeshindwa  kulipa. Hivyo  basi  ukipokea  notisi  leo  anza  kuhesabu  mpaka  siku  60.  Humo  katikati  hawataruhusiwa  kuuza  mali  yako. Na  wakiuza  ndani  ya  muda  huo  basi  itakuwa  ni  makosa.

Juu    ya  hilo  ni  vema  pia  ukajua  kuwa notisi  hiyo  ya  siku  60  haihusishi  tu  uwezo  wa  kushindwa  kulipwa.  Bali  pia  lolote  lile  ambalo  ni  sharti  katika  mkataba  wa  mkopo  na  ambalo  taasisi  ya  fedha  inadai   umelikiuka. Hapo  pia  haitachukua  hatua  ya  kuuza  mali  yako  hadi  upate  notisi  hiyo  ya  siku  60.

3.  NINI  UFANYE   IKIWA  NOTISI  HIYO  ITAKIUKWA.

Kwanza   kama  nyumba/kiwanja  hakijauzwa  kimbilia  mahakamani  na   weka  zuio,  na  pili  kama  tayari   mali  imeuzwa   tena kwa  kukiuka  notisi  na muda  wake  basi  unaweza  kufungua  shauri  la  kubatilisha  mauzo  hayo   kwa  msingi  wa  kukiukwa  kwa taratibu  za  mauzo  na  waweza  kurejeshewa  mali  yako.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment