Tuesday 30 May 2017

UNAYO HAKI YA KUMUONA MTOTO HATA KAMA UMEACHANA NA MZAZI MWENZAKO.


Image result for MTOTO
NA  BASHIR  YAKUB -

Wapo  wazazi  wanaowakatalia  wazazi  wenzao  kuwaona  watoto/mtoto   baada  ya  kuwa  wameachana.  Wengine  hawakuachana  bali  hawakuwahi  hata kuishi pamoja  isipokuwa  walizaa  tu  lakini  yule  mzazi  anayeishi  na  mtoto  anamzuia  mzazi mwenzake  kumuona  mtoto  husika. 

Basi  makala  haya  yatatizama  jambo  hili  kwa  sura  ya  sheria  zetu.  Uhalali  wake  na  uharamu  wake, hatua  unazoweza  kuchukua  na  mtazamo  wa  jumla  ikiwa jambo  hili  ni  haki  kisheria  ama  laah.

Sheria  namba  21  ya  mwaka  2009  Sheria  ya  Mtoto  ndiyo  itakayotupatia  majibu  ya  suala  hili  kwa  ujumla  wake.

1.KUMUONA  MTOTO  HUMAANISHA  NINI.

Unapotizama  kwa ujumla  sheria  ya  mtoto  hasa  vile  vifungu  vinavyozungumzia   habari  ya  kumuona  mtoto   utaona   kuwa   vinazungumzia  kumuona  mtoto  kwa  maana  ya  hatua  ya  baba  mzazi,  mama  mzazi,  au  mlezi  mwenye   mamlaka  kutembelea  eneo  alilohifadhiwa  mtoto  kwa  ajili  ya  kuonana  na  mtoto  huyo.

Haijalishi  anaumwa  au  yu  mzima,  yuko  kituo  cha kulelea  watoto  au  nyumbani  kwa  mtu, na  hali  nyingine  au  mazingira  yoyote  atayokuwemo. Pia kumuona  mtoto  si  tu  kumuonesha  mtu  kuwa  mtoto  ni  yule  halafu  basi.  Bali  kumuona mtoto  kunajumuisha   kumuona  na  kumgusa  kimwili.

2.  JE  NI  MTOTO   WA  UMRI  GANI  ANAYEONGELEWA  HAPA.

Kifungu  cha  4 cha Sheria ya mtoto  kinajibu  swali  hili.  Kifungu  kinasema  kuwa  mtu  mwenye  umri   wa  chini  ya  miaka  18  ataitwa  mtoto .  Kwa  hiyo  tunapoongelea   kumuona  mtoto    tunamaanisha  mtu  ambaye  umri  wake  uko  chini  ya  miaka  18  yaani  kuanzia  miaka  17   kushuka  chini.  Mwenye  miaka  18  kamili  si  mtoto  kwa  maana  ya  kifungu  hiki.

3.  HAKI  YA  KUMUONA  MTOTO  HII  HAPA.

Kifungu  cha 38  cha  sheria  ya  mtoto  kinatoa  haki  kwa  mzazi  au  mlezi  ambaye  hakai  na  mtoto    kuwa  na  uwezo  wa  kumuona  mtoto. Haki  hii  ipo  kisheria  na  mzazi  au  mlezi  anayekaa  na  mtoto  hapaswi  kumnyima  mzazi  mwenzake  au  mlezi  mwingine   haki  ya  kumuona  mtoto  huyo.

Suala  la  msingi  ni  kuwa  kumuona  kwako  mtoto  kusiwe  na  lengo  lolote  la  kumdhuru  au    kumfanyia  jambo lolote  lililo  kinyume  na  haki  za  mtoto  pamoja  na  haki  za  binadamu  kwa  ujumla  wake.  Nje  ya  haya  haki  yako  ya  kumuona  mtoto  iko  palepale.

Usinyimwe  haki  hii  kama  wewe  ni  baba  na  mama  ndiye  anayekaa  na  mtoto    na  usinyimwe  haki  hii  kama  wewe  ni  mama  na  baba  ndiye  anayekaa  na  mtoto  halikadhalika  mlezi.

4.  NINI  UFANYE   UKINYIMWA   HAKI   YA  KUMUONA   MTOTO.

Kifungu  cha  38  cha  Sheria  ya  mtoto  kinasema  kwamba   unatakiwa  kwenda  mahakamani   kufungua  malalamiko  kwa  ajili  ya  kupewa  haki  hiyo.  Wewe  utakua  mlalamikaji  na  na  mzazi au  mlezi  aliyekunyima  haki  hiyo  atakuwa  mlalamikiwa.

Sehemu  nzuri  ya  kufungua  malalamiko  ya  aina  hii ni  mahakama  ya  mwanzo  iliyo  ndani  ya  eneo  alilomo  mtoto.  Sio  eneo  unaloishi  wewe bali  eneo  ambako  mtoto  analelewa na  kuishi. Pia waweza  kufungua  lakamiko  hili hata  mahakama  ya  wilaya iliyo  katika  wilaya  anakolelewa  na  kuishi  mtoto.

Mwisho  sababu  zinazotolewa  na  wale  wanaonyima  haki  hii  kwa mfano  ati  hujawahi  kuleta  matumizi,  ati ulimtelekeza  mtoto  miaka  mingi, nk hazina  mashiko  kumnyima  mzazi  haki  hii.

Ikiwa  kuna  mtu  analalamikia sababu  hizo  basi  naye  anayo  haki  ya  kuyalalamikia   hayo mahakamani   lakini  sio  kumnyima  mzazi  mwenzake  au  mlezi  haki  ya  kumuona  mtoto.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


2 comments:

  • Unknown says:
    10 September 2019 at 23:37

    Je ni kila baada ya MDA gani mzazi asiekaa na mtoto ataruhusiwa kumuona mtoto???

  • double N says:
    2 March 2022 at 22:27

    Naomba hiki swali lijibiwe

Post a Comment