Monday 15 May 2017

KWA SHERIA ZETU ZILIVYO HAITAWEZEKANA TUNDU LISSU KUMSHITAKI MAKONDA.

Image result for TUNDU  LISSU  MAKONDA


NA  BASHIR  YAKUB - 

SHERIA  ZILIZOPITIWA :
1. Sheria ya Mwenendo wa Kesi za Jinai, Sura ya 20.
2. Sheria  ya Huduma za Mashtaka  kwa Taifa, Na. 27/2008.
3. Kanuni  za  Adhabu, Sura  ya  16.
_______________

Tundu Lissu anasema  anaamua kumshitaki Makonda kwa kosa la kughushi nk. kwa kuwa Serikali imekataa na haioneshi nia ya  kumfikisha mahakamani Makonda.

Kama sababu ni kuwa serikali imekataa kumpeleka Makonda mahakamani  ndio maana  Tundu Lissu na wenzake wanaamua sasa kuchukua hatua basi nao hawatafanikiwa.

Kwa sheria ilivyo hawatafanikiwa mpaka serikali  wanayosema haitaki itake.  Kwa mujibu wa kifungu cha  97 cha Sheria ya Mwenendo wa Kesi  za Jinai kazi ya kufungua na kuendesha mashtaka  yote ya jinai ni kazi ya serikali kupitia  ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Jinai (DPP).

Hata hivyo  kwa mujibu wa kifungu cha 99(1)  cha sheria hiyohiyo ni kweli bila
ubishi kuwa mtu binafsi  au Wakili yeyote binafsi kama alivyo Tundu Lissu naye  anaweza  kufungua na kuendesha mashtaka ya jinai dhidi ya mtu yeyote mkosaji kama ilivyo kwa DPP wa serikali.

Pamoja na hayo kifungu cha  97 cha sheria hiyo ya Mwenendo wa Kesi za Jinai kinasema kuwa ikiwa mashtaka yamefunguliwa na mtu binafsi au Wakili binafsi kama alivyo Tundu Lissu basi  mwendesha mashtaka wa serikali  akiamua anaweza kuchukua kesi hiyo.

Pia kifungu kinasema zaidi kuwa Wakili huyo binafsi katika kesi hiyo aliyofungua atalazimika  kufuata maelekezo   ya  mwendesha mashtaka  huyo wa serikali wakati wote  wa kesi.

Maana yake ni kuwa ikiwa mwendesha mashtaka wa serikali atamwamuru Tundu Lissu kubadili jambo lolote katika kesi aliyofungua basi atalazimika kulibadilisha. Lakini kubwa kuliko yote ikiwa mwendesha mashtaka wa serikali atamwamuru Tundu Lissu kufuta kabisa kesi ya Makonda  basi atalazimika kuifuta. Hii ndio maana ya kifungu hicho.

Lakini pia kifungu cha 91(1) cha hiyo kinasema kuwa DPP anaweza kuifuta kesi YOYOTE  ya  jinai wakati wowote kabla ya hukumu. Neno kesi YOYOTE  maana  yake ni iwe imefunguliwa na mtu au Wakili binafsi, au taasisi yoyote ya serikali au binafsi mathalan Chama cha Wanasheria,  DPP  wa serikali akiamua kuifuta  anaifuta mara moja.

Kwa msingi huu wa sheria ndio maana nikasema kuwa Kama Tundu Lissu anasema anamshitaki Makonda kwasababu serikali imekataa kumshitaki  basi  utaona  wazi kuwa bado hataweza kumshitaki mpaka serikali iamue na itake.

Awali kifungu cha 90 cha sheria ya Mwenendo wa Kesi za Jinai kilikuwa kikilieleza  hili kwa undani kabla ya kufutwa na Sheria  Namba 27/2008 ya Huduma za Mashtaka kwa Taifa kifungu cha 31.

Mwisho  yatupasa kujua kuwa Tundu Lissu  hawezi kumshitaki Makonda mpaka apate idhini ya hakimu. Kifungu cha 99(1) Sheria ya Mwenendo wa Kesi za Jinai kinasema hivyo. Nimemsikia Lissu akisema  kuwa ati wanachotakiwa kufanya ni kutoa taarifa kwa hakim basi. Hapana sio kweli , kifungu kinasema ni idhini na ndio maana hakimu anaweza kukataa au kukubali. Limetumika neno "MAY" kuashiria uhiari wa hakimu.

Kwa ufupi Tundu Lissu na wenzake  katu hawataweza  kumshitaki Makonda na kufanikiwa mpaka serikali iamue na itake. Hakuna namna  ambavyo unaweza kuikwepa serikali katika hili.
Tanbihi  ni  kuwa  makala  hayasemi  kuwa  Tundu  Lissu  hatafungua  kesi,  bali  ni  kuwa  kama   atafungua   kesi  na  ikaendelea  hadi  mwisho    basi   bila  shaka  serikali  itakuwa  imeamua  iwe  hivyo  kwa  kuacha  kutumia  mamlaka  iliyopewa  na  sheria  na  si  kwa  ujanja  wa  yeyote.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment