Wednesday 5 April 2017

JE UNAUJUA MKATABA WA PANGO AMBAO NI LAZIMA KUSAJILIWA KISHERIA?.


Image result for mkataba wa pango
NA  BASHIR  YAKUB - 

Kwa  mujibu  wa  sheria  ya usajili  wa  ardhi  sura ya  334   ipo  aina   ya  mikataba  ya  pango  ambayo  baada  ya  kuwa  imeingiwa  kati  ya  mpangaji  na  mwenye  nyumba/eneo  ni  lazima  isajiliwe.  Mikataba  ya  aina  hiyo  isiposajiliwa  inakuwa   haijakidhi  vigezo  vya  kisheria  na  hivyo  kubatilika.

Aidha  pango  huhusisha  shughuli  mbalimbali.  Yapo  mapango  kwa  ajili  ya  biashara  maduka,  bar, mahoteli n.k.  na  pia  yapo  mapango  kwa  ajili  ya  makazi. Iwe  umepanga  kwa  ajili  ya  biashara  au  makazi  madhali  aina  yako  ya  upangaji  inahitaji  kusajiliwa  kisheria  basi  huna budi  kufanya  hivyo  ili  uhalali  wa  pango lako  upatikane.

Kabla  ya  kuona  aina  ya  mikataba  ya  pango  ambayo ni  lazima  kusajiliwa  ni  vyema  kujikumbusha  kidogo  kuhusu  haki  za  mpangaji.

1.HAKI   ZA  MPANGAJI.

( a ) Haki  ya  kutoingiliwa  na  mwenye  nyumba  ili  kumpa  uhuru mpangaji   kufurahia  pango  lake.

( b ) Haki  ya  kumpa  taarifa(notice)  mapema  mpangaji  ikiwa mwenye nyumba  anataka  kukagua  nyumba/eneo  lake.

( c ) Haki  ya  kutoondolewa  au  kusitishiwa  mkataba  mpaka  baada ya  kupewa  taarifa  maalum( notice) .

( d ) Haki  ya  kuambiwa  ukweli  kuhusu  hali  ya  nyumba kabla  ya  kusaini  mkataba  wa  pango. Mfano  kuambiwa  ikiwa  eneo  linajaa  maji  kipindi  cha  mvua, kuambiwa  ikiwa  nyumba  inavuja n.k.

( e ) Haki  ya  kukataa  sharti  lolote  ambalo  linalenga kuminya  uhuru   wa  mpangaji  au  linalovunja  sheria  yoyote  ya  Tanzania.

( f ) Haki  ya  kupewa  taarifa  mapema(notice)  kabla  ya  kupandisha  kodi  ya  pango.

( g )  Haki  ya  kupewa  taarifa  mapema(notice)   kabla  ya  kubadilisha  sharti  lolote  katika  mkataba  wa  pango.

Haki  ni  nyingi  hizi  ni  baadhi  tu.

2.  MKATABA  WA  PANGO  AMBAO  NI  LAZIMA  KUSAJILIWA.

Kifungu  cha  54 ( 1 )  cha  Sheria  ya  Usajili  wa  Ardhi ,  Sura  ya  334  kinasema  kuwa   pango  ambalo  mkataba  wake  unazidi  miaka  mitano   linatakiwa  kusajiliwa.
Wapo  watu  wanapanga  mahoteli,  bar, maduka  nk.  ambao   miaka ya  pango  katika makubaliano  yao  ni  zaidi   ya  mitano.  Hawa  mikataba  yao  ni  lazima  isajiliwe.  

Mara  nyingi   mkataba  wa  pango  huweza  kuwa   wa  miaka  mingi  kutokana  na  aina  ya  biashara  anayotaka  kufanya   mpangaji    halikadhalika  uwekezaji  anaotarajia  kufanya  eneo  analotegemea  kupanga.  Wakati  mwingine  mpangaji  hukubaliana  na  mwenye  eneo  kufanya  marekebisho  makubwa ( renovation) ili  enepo  lifanane  na  aina  ya biashara  anayotaka  kufanya. 

Mbali  na  hayo ni  vema  kufahamu  pia  kuwa  mkataba  ambao  ni  chini  ya  miaka  mitano  lakini mkataba  huo  una  sharti  la  kuhuisha( renew)  kwa  miaka  mingine,  ambapo  ukijumlisha  miaka  ya  awali  na  hiyo  ya  kurenew  jumla  inazidi  mitano  basi  nayo  ni  lazima  kusajiliwa.

Tumeongelea  mikataba  inayozidi  mikaka  mitano  lakini  hatupaswi  kusahau  kuwa hata  mikataba  ya  pango  iliyo  chini  ya  miaka  mitano  inaweza  kusajiliwa japo  sio  lazima.  Mikataba  hii  una  chaguo  kusajili  au  kutosajili.  Kisheria kutosajiliwa  kwake kwa  namna  yoyote  hakuathiri  uhalali  wake.

4.  WAPI  UKASAJILI.

Msajili  wa  nyaraka  anayepatikana  ofisi  za  ardhi  ndiye  anayehusika  na  usajili   wa  mikataba  hii. Unapofika  ofisi  yoyote  ya  ardhi  utapewa  maelekezo  lipi   la  kufanya  ili  mkataba  wako  uweze  kusajiliwa.
Aidha  ipo  ada ya  kulipa  kabla  ya  usajili  ikiwemo  kodi  ya  faida.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

1 comments:

Post a Comment