Monday 20 March 2017

WANANDOA KUACHANA KWA MKATABA MAALUM BILA KWENDA MAHAKAMANI.

Image result for WANANDOA

NA  BASHIR  YAKUB -

Zipo  namna  nyingi  za  kuachana  kisheria  kwa  wanandoa  ambao  wanadhani  sasa hawawezi  kuendelea. Wengi  wetu  tunajua  zile  za  kupitia mahakamani.  Zile  ni  sahihi  lakini  upo  uwezekano  pia wa  kuachana  kwa  mkataba  maalum  bila  kuhitaji  kwenda  mahakamani.

Aidha  yafaa  ifahamike  kuwa  Kuachana  katika  ndoa  na  kuamua  kuishi   nje  ya  ndoa  ni  jambo  la  kawaida.  Kisheria si  dhambi  mwanandoa  yeyote   kuona  kuwa  sasa  hawezi  kuendelea  kuwa  katika  ndoa.  Ni  kwasababu  hii  hata  sheria  ikatambua   uwezekano  wa  watu  kuachana  na  halikadhalika  ikaweka  utaratibu  maalum  kwa  walio  tayari  kwa  hilo.

Tofauti  na kuachana  kwa  mkataba  namna  nyingine  ni  kwa  njia  ya  talaka  mahakamani  na  kwa  njia  ya  kutengana  mahakamani  ambazo  nazo tutaziona  hapa  chini kabla  ya  kutizama  ile  ya  mkataba.

1.KUACHANA  KWA  TALAKA.                                              

Kifungu  cha  99  cha  Sheria  ya  ndoa  kinaongelea  talaka.  Maombi  ya  talaka  hupelekwa  na  yule  anayedhani  hawezi  kuendelea  na  ndoa  kutokana  na  sababu   anazoamini  kuwa ndoa  hiyo haiwezi  kuendelea.  Mahakama  huzisikiliza  pande  zote  mbili  na  kuja  na maamuzi.

Kifungu  cha  107( 2 )  cha  sheria  ya  ndoa  kinazitaja  sababu  ambazo  zote  au  mojawapo  ikithibitishwa  ni  ushahidi  kuwa  ndoa  hiyo  haiwezi  kuendelea.  Baadhi  ni  ukatili, zinaa, kutelekeza, kifungo  cha  maisha  au  kifungo  kisichopungua  miaka mitano,   na  nyingine  nyingi.
Talaka  huombwa  mahakamani  na  hivyo maombi  yake hupelekwa  mahakamani.

2.   KUTENGANA   MAHAKAMANI   BILA  TALAKA.    

Hatua  hii  ni  kwa  mujibu wa  kifungu  cha  99  cha  sheria  ya  ndoa.  Mnatengana  kwa  muda  fulani  lakini  bila  talaka. Talaka  ni  kutengana  milele  wakati  hii  ni  kutengana  kwa  muda.  Njia  hii  nayo   muombaji  hutakiwa  kwenda  mahakamani  na  kufungua  maombi.

Wahusika  wote  wataitwa  na  kila  mmoja  atajieleza na baadae mahakama  itatoa  maamuzi.  Njia  hizi  zote mbili mwombaji  hutakiwa  kupitia  mahakamani  isipokuwa  hii   ya  mkataba  ambayo   itaelezwa  hapa  chini.

3.  KUACHANA  KWA  MKATABA  MAALUM.  

Kifungu  cha  67  cha  sheria  ya  ndoa  kinasema  kuwa  wanandoa  wanaweza  kwa  njia  ya  maandishi  ambayo  yatakuwa  yamesainiwa  na  wote  wawili   kuamua  kuishi  tofauti/nje  ya  ndoa.  Kwahiyo  utaona  hapa  kuwa  unachotakiwa  kufanya  ni  kukubaliana  na  mwanandoa  mwenzako  kwamba  sasa  naona  mambo  hayaendi  na hivyo  ni  bora  kila  mtu  aishi  maisha  yake.

Akikubali  basi  mtakaa  chini  mtaandikishana  kisheria  kabisa  na  kila  mtu  ataendelea  na  maisha  yake.  Isipokuwa  ni  lazima  mnapoamua kutumia  njia  hii hakikisha  katika  maandiko  yenu viwemo  vipengele  vinavyohusu  matunzo  ya  watoto/mtoto  kwa  maslahi  mapana  kabisa,  muafaka  na  hatima  kuhusu  mali  mlizonazo,  pia  matunzo  au  vinginevyo  kwa  mmoja  kati  ya  wanandoa  kama hilo  litakuwa  ni  la  lazima.

Kwahiyo  haya  ni  maandiko  na  ni  mkataba  sawa  na  mikataba  mingine  ya  kisheria.  Faida  ya  njia  hii ni  kuwa  ni  nyepesi, haitumii  mda  mwingi, haina  gharama  kubwa  na  inatekelezeka  kwa  urahisi.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment