Tuesday 21 March 2017

SHERIA IMERUHUSU KUDAI ZAWADI ULIZOTOA UCHUMBA UNAPOVUNJIKA.

Image result for ZAWADI YA UCHUMBA

NA  BASHIR  YAKUB -

Una  mahusiano  na  mwanaume au  mwanamke  ambaye  kimsingi  mpo  katika  uchumba.  Unampa  zawadi  nyingi  naye  anakupa  zawadi. Mnayo  ahadi  ya  kufunga  ndoa  na  kuishi  kama  mme  na  mke .  Na  kwasababu  hiyo    unajitoa  sana  kimatumizi   kwa  mtu  huyo.

Lakini  katika  mazingira  usiyoyaelewa   unaona  sasa  mambo  hayaendi  vizuri.  Hayaendi  vizuri  katika  kiwango  ambacho  sasa   mahusiano  yamevunjika  kabisa.  Hakuna  tena  mahusiano. Au  bado  yapo  lakini  kwa   mambo  unayofanyiwa  unaona  kabisa  hutakiwi  tena.

Kumbuka  huko  nyuma  umegharamia  sana.  Umegharamia  kwa  fedha   na  mali.  Swali  ni je  vitu  hivi   haviwezi  kurudishwa ?.  Vitu  hivi  haviwezi  kufidiwa ?.  Na  je sheria  imeongelea  kuhusu  jambo  hili ?. 

Majibu  ya  maswali  haya yote   ni  ndiyo.  Ni  ndiyo,  na  gharama pamoja  nazo  zawadi   zinaweza  kurejeshwa. Unaweza  kushangaa  kuona sheria   imeongelea  hata  mambo  ya  uchumba  lakini  ndio  ukweli.

Wengi  tunaijua  sheria  katika  kuongelea  wizi,  dhamana,  mikataba, mirathi,  ndoa,  na  mengine.  Lakini  ni  vyema  tukajua  kuwa  sheria  ni  pana  na  imeongelea  mambo mengi  mno.  Hili  la  uchumba  nalo  ni  sehemu  ya yaliyoongelewa.

1.KUVUNJA  UCHUMBA.

Kifungu  cha  69( 1 ) cha  Sheria  ya  Ndoa  iliyofanyiwa  marekebisho  2010 kinasema kuwa  mtu anaweza  kufungua  shauri   na  kudai  fidia  baada  ya uchumba  kuvunjwa. 

Kwa  haraka  utaona  kuwa  tafsiri  ya  kifungu  hiki  sio  kufungua shauri ili kumlazimisha  mtu  akurudie,  hapana.  Mahakama  haiwezi  kutoa  maamuzi  kuwa  fulani  lazima  amrudie  fulani.  Isipokuwa  lengo  lake  ni   kumtaka  yule  aliyeumizwa  katika  hili  kudai  fidia  kutokana  na  maumivu  aliyoyapata.  Hapa  hatujaongelea  kurudisha  zawadi. 

Kudai  fidia   na  kurudisha  zawadi  ni  vitu  viwili  tofauti. Fidia  inahusu  kulipwa  maumivu  uliyoyapata  kutokana na  tukio  hilo la  kuachwa  pamoja  na  muda  uliopoteza  na  huyo  mtu. Wakati  zawadi  ni  kurejesha  kile  ulichotoa. Kwahiyo  la  zawadi  tutaliona  baadae.

Aidha  masharti  ya kufungua  shauri  la  kudai  fidia  ni  kuwa ,  moja  anayefungua  shauri  awe  ni  yule  aliyeumizwa,  pili ahadi  ya  kuoana  lazima  iwe  ilikuwa  imefanyika  Tanzania, tatu  wakati mnaingia  kwenye  mahusiano  iwe  mlikuwa  nyote  mmetimiza  miaka 18 .

2.  KURUDISHA  ZAWADI.     

Kifungu  cha  71  cha  Sheria  ya  ndoa  kinasema  kuwa  mtu  anayo   haki  ya  kufungua  shauri  kudai kurejeshewa   zawadi   ambazo  alizitoa  kwa  mtu  ambaye  alikuwa ana  ahadi  ya  kufunga  naye  ndoa  lakini  ndoa  haikufungwa.
Zawadi  ni  pamoja  na  fedha,  nyumba,  magari, nguo  na  kila  kitu  chenye  thamani(valuable).  Haijalishi   mali  hiyo  ipo  kwenye  jina  la nani   suala  la  msingi  ni  kuthibitisha  kuwa  wewe  ndiye  uliyetoa hiyo  zawadi.

Shauri  la  namna  hiyo  unaweza  kulifungua  mahakama  yoyote  ya  mwanzo, ya  wilaya, ya  hakimu  mkazi  au  hata mahakama  kuu.  Itategemea  na  thamani  ya kiwango  cha  mali  unazodai.  

Kama  mali  hizo  zitakuwa  zimekwishatumika  au  hazipo  tena  pengine  zimeuzwa  au  kutolewa  zawadi  kwa  mtu  mwingine  basi  itatakiwa   kulipwa  fedha  zinazolingana  na  mali  hizo  au  mali  hizo zikanunuliwe  tena  kwingine   ili  kumrudishia  anayedai.

Ukishindwa  kabisa  kurudisha  basi  mali  zako  binafsi  ambazo  hazikuwa  sehemu ya  zawadi  zitauzwa  ili  kupata  kiwango  kinachodaiwa  na  kama  huna  mali yoyote  ya  kuuza  utatakiwa  kwenda  jela  kama  mfungwa  wa  madai.
Kwa  hiyo  watu  wanatakiwa  waelewe  kuwa  uchumba  na  ahadi za  kuoana  si  jambo  jepesi  kama  wanavyolitamka  na kuliahidi .
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com




0 comments:

Post a Comment