Thursday 2 March 2017

NAMNA YA KUOMBA KUKAA NA MTOTO PANAPO MGOGORO NA MZAZI MWENZAKO .

Image result for WAKIGOMBANIA MTOTO


NA BASHIR  YAKUB -

Tumesikia  mara  kadhaa  wazazi  wakigombania  kukaa  na mtoto/watoto. Haya  hujitokeza  baada  ya  kuvunjika  kwa  ndoa  kwa  talaka,  baada  ya  kutengana  bila  talaka   au  pasi  na  ndoa  wazazi  tu  wamezaa  na  sasa  hawaelewani  na  mgogoro wa  nani  akae  na  mtoto  umeibuka.

Tunahitaji  kujua ikiwa kuna  haja  ya  kugombania  mtoto kwa matusi  na  ugomvi wakati  zipo  taratibu  za  kisheria. Tujue  kama yafaa  kutumiana  jumbe  chafu  za  kudhalilishana pale   unapotaka  ukae  na  mtoto. Jibu  ni  hapana  ila  ni  watu  tu  wajue  taratibu.

Ifahamike  kuwa  iwe  kwa  ndoa  au  bila  ndoa   haki  ya  mtoto  kukaa  na  wazazi  au  mzazi   iko  kwa  yeyote. Ni  aidha  atakaa  na wote  wawili  au  mmoja  wao. Sheria  namba  21 ya  2009, Sheria  ya  Mtoto  ndiyo  sheria  ambayo  kwasasa  inasimamia  ustawi  na  haki  za  mtoto.  Hivyo  makala  yataeleza  yaliyo  katika  sheria  hii.

1.MTOTO  NI  NANI.

Kifungu  cha 4( a ) cha  sheria  ya  mtoto  kinatafsiri  neno  mtoto  kumaanisha  mtu  ambaye  yuko  chini  ya umri  wa  miaka  18. Kwa  maana  hii  miaka  18  kamili  sio  mtoto  isipokuwa sasa  chini  yake  ndiye  mtoto  kwa  tafsiri  ya  kifungu  hiki.

Sambamba na  hilo  kifungu  cha  7( 1 ) kinaeleza  haki  ya  mtoto  kukaa  na  wazazi  wake  wote  wawili. Basi  yaje  hayo   ya  kutengana   na  mtoto  kuishi  maisha ya  mzazi  mmoja , bado  uhalisia  ni  haki  ya  msingi   ya  mtoto  kukaa  na  wazazi  wake  wawili  kama  ilivyoainishwa  hapa.

2.  NAMNA  YA  KUOMBA  KUKAA  NA  MTOTO.

( a ) UTAOMBA  WAPI.

Utaomba  mahakamani.   Swali  la  ni   mahakama  ipi  ina  mamlaka  hayo  au  ni  mahakama  ipi  utakwenda  kuomba linajibiwa  na  Kifungu  cha  3 ( a ) cha   sheria  hiyo  kinachozitaja  mahakama  za  mwanzo,  za  wilaya,  za  hakimu  mkazi  na  mahakama  kuu  kushughulika  na  masuala  hayo.  

Lakini  ni vema  zaidi  ikiwa  utaitumia  mahakama  ya  mwanzo   au  ya  wilaya kwa  hatua  za  awali.
Hivyo  basi  hapo  ndipo  utakapopeleka  maombi  yako.

( b ) NANI  ANARUHUSIWA  KUOMBA.

Kifungu  cha  37 ( 1 ) cha  sheria  hiyo kinasema  yeyote  kati  ya  wazazi  wawili  ambao  wanagombania  mtoto  anaweza  kuomba.  Kila  mmoja  ana  haki  na  haki  ya  mmoja  haiondoi  haki  ya  mwingine.

Wapo  wanaodhani  haki  ya  mwanaume  ipo  chini  na  ya  mwanamke  ipo  juu  katika  hili,  si  kweli. Haki  ni  haki  na  kila  mmoja  ana  haki.  Kwahiyo  huna  haja  ya  kujihofia  kuwa pengine  itakuwa  hivi  au  vile.

( c )  NI  KITU  GANI  UTAPELEKA  MAHAKAMANI.

Utapeleka   maombi  rasmi  ambayo  yatakuwa  yameandaliwa  kwa  hoja  za  kisheria  huku  yakiwa  yamesainiwa   na  muombaji .  Kawaida  maombi   hulipiwa  ada  mahakamani   japo   haiwezi  kuzidi  elfu  50.

Baada  ya  maombi  kuwa  yamesajiliwa  utatolewa  wito  kwa  ajili  ya  yule  unayegombea  naye mtoto  na  kesi  itahesabika  kuanza  rasmi.

( d ) ILI  MAHAKAMA  IKUPE  MTOTO  UNATAKIWA   KUTHIBITISHA  NINI  NA  NINI ?.

Kifungu  cha  37( 4) na  kifungu cha 4 ( 2 )  kwa  pamoja vimeongelea  suala  la  maslahi  mapana  ya  mtoto( best  interest  of  the  child).  Kwahiyo  ili  mahakama  iweze  kukupatia  mtoto  unatakiwa  kuonesha  kuwa  yule  aliye  na  mtoto  hawezi  kumpatia  mtoto  huyo  maslahi  mapana  kama  sheria  inavyotaka  na  badala  yake  wewe  unaweza.

Kutompatia  maslahi  mapana  ni  pamoja  na  mazingira  mabovu  anayoishi  mtoto  huko  aliko, uwezo  mdogo  wa  huduma  muhimu, tabia  chafu  za  aliye  na  mtoto, uchizi, ugonjwa  wa  kuambukiza  au  ugonjwa  uliompotezea  fahamu  aliye  na  mtoto, mazingira  hatarishi  kama  baa,  dangulo, kumbi  za  starehe, na  mengine  yote  ambayo  kwa  sura  yake  hayajengi  ustawi  bora  wa  mtoto.

Hivyo  kuthibitisha  baadhi, yote  au  hata  moja  kati  ya  haya  litaipelekea mahakama   kuamua  ukae  na  mtoto.
Yako  mengi kuhusu  mada  hii  lakini  angalau  kwa  ufahamu  wa  jumla  ni  hayo.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA  JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment