Wednesday 22 February 2017

UTARATIBU WA KUPATA HATI UNAPONUNUA ARDHI YA KIJIJI KWA UWEKEZAJI.

Image result for ARDHI YA KIJIJI

NA  BASHIR  YAKUB -

Kawaida  hatimiliki( granted  right  of  occupancy)  hazitolewi  kwa  ardhi  za  vijijini. Ardhi  za  mijini  tu  ndizo  huwa  na hadhi  ya kupata  hatimiliki. Lakini  wapo  watu  ambao  wamechukua maeneo  ya  vijijni  kwa  ajili  ya  uwekezaji. 

Wapo  waliochukua ardhi  kama  wachimbaji  wadogo,  kilimo, madini, n.k. Hawa  pengine wangependa  wapate  hatimiliki  ili  kukuza  biashara  zao  sambamba  na  kupata  faida zinazotokana  na  kuwa  na  hati miliki. Moja  ya  faida  ya  kuwa  na  hatimiliki  ni  pamoja  na  kupata  mkopo.

Swali  ni  je  inawezekana  kuipatia  ardhi  yako  ya  kijijni  hatimiliki  yenye hadhi  sawa na  ile  inayotolewa  kwa  ardhi  za  mijini?.

1.ARDHI  YA  KIJIJI  NI  IPI.

Sheria  za ardhi  namba 4 na 5 kwa pamoja  zimeainisha  aina tatu  za  ardhi  kwa  hapa  Tanzania.  Kwanza  ardhi  ya  jumla,  ardhi  ya  hifadhi, na  ardhi  ya  kijiji. Ardhi  ya  jumla( general  land)  ni  hii  ardhi  ya  mijini  ambayo  huwa  na  hati  miliki( right  of  occupancy).  Hii  ni  asilimia  2  ya  ardhi  yote  ya  Tanzania.

Ardhi  ya  hifadhi( reserved  land)  ni  kama  mbuga,  kingo  za  mito na bahari, makaburi,  viwanja vya  wazi n.k. Hii  ni  asilimia 28 ya  ardhi  yote. Ardhi  hii  huwa  haimilikishwa  labda  isemwe  vinginevyo.

Ardhi  ya  vijiji( village  land). Hii ni  ardhi  ya  vijiji  kama  jina  lake  lilivyo. Sote  tunajua  vijijini  ni  wapi.  Inachukua  jumla  ya  asilimia 70 ya  ardhi  yote.

2.  UMILIKI  WA   WA  AINA  TATU  WA  ARDHI  YA  KIJIJI.

Ardhi  ya  kijiji  iwe kwa uwekezaji, makazi  au  vinginevyo  inaweza  kumilikiwa  kwa  namna  tatu  tofauti. Kama  ifuatavyo.

( a ) Kumiliki  kwa  haki  bila  nyaraka  yoyote  ya  umiliki( deemed  right of  occupancy). Kwa  mtu  anayewekeza  kijijini  huu  si  utaratibu mzuri  kwake. Hapa  mmiliki  atamiliki  ardhi  kijijini  bila  kuwa  na  nyaraka  yoyote  inayomtambulisha  kama  mmiliki   lakini  hilo  halitamwondolea  uhalali wake katika  kumiliki. Wamiliki  wengi  vijijni  humiliki  kwa   mtindo  huu.  Wengi  wana  ardhi  lakini  hawana  nyaraka  yoyote  kudhibitisha  kumiliki.

( b ) Kumiliki  kwa  hati  ya  kimila(customary  certificate). Sura  ya  114 sheria  na  5  ya  1999  ya  ardhi  ya  vijiji  inatambua  uwepo  wa  hati  za  kimila. Hati  hizi  hutolewa  na  halmashauri  za  vijiji  kwa utaratibu  maalum.

( c ) Kumiliki  kwa  hatimiliki( granted  right  of  occupancy). Hatimiliki  hutolewa  kwa  maeneo ya  mijini  tu  lakini  hata  vijijini  zinaweza  kutolewa  ikiwa  ardhi  inachukuliwa  kwa  ajili  ya  uwekezaji au  shughuli  nyingine  za serikali.

4. UTARATIBU  WA  KUPATA HATI  UNAPONUNUA  ARDHI  YA  KIJIJI  KWA  UWEKEZAJI.

( a ) Kwanza  miliki  ardhi  kijijini  kwa  kufuata utaratibu  wote  wa umiliki  ardhi  ya  vijiji  kama  unavyoainishwa  na Sheria  ya  ardhi  ya  vijiji,  sura  ya  114 pamoja  na  kanuni  zake  za mwaka  2001. Kwa  ufupi  uwe  unamiliki  ardhi  ya  kijiji  kihalali.

( b ) Baada  ya  hilo  utafanya  maombi  maalum kwenda  kwa  kamishna  wa  ardhi  makao  makuu  wizara  ya  ardhi  ukiomba  kupatiwa  hati miliki  katika  ardhi  ya  kijiji.

( c ) Katika  maombi  hayo  utaambatanisha  nyaraka zote  za  umiliki. Pia  kama  ni  kampuni  inayoomba  au  taasisi  na  si  mtu  binafsi  basi  pia  nyaraka  za  kuthibitisha  usajili  wake  zitaambatanishwa.

( d ) Kamishna  ataangalia  ikiwa  kila kitu  kinachohitajika  kimefuatwa na  ikiwezekana  atawasiliana  na  uongozi  wa  ardhi  wa  kijiji  husika  ili  kujiridhisha  zaidi.

( e ) Ikiwa  kila  kitu  kitakuwa  vizuri  basi  ardhi  hiyo  itabadilishwa  kutoka  ardhi  ya  kijiji( village  land)  na  kuwa  ardhi  ya  jumla( general  land).

( f ) Ikishakuwa  ardhi  ya  jumla  basi  msajili  wa  hati( registrar  of  titles)   anaweza  sasa  kutoa  hatimiliki  kwa  mwombaji  ambayo  itakuwa  na  hadhi  sawa  na  zile  hati  za mijini.

( g ) Wakati  mwingine  ardhi  iliyoombwa  itamilikishwa kituo cha  uwekezaji  Tanzania( TIC) halafu  kituo  hicho ndicho  kitakachompatia  mwombaji.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment