Wednesday 1 February 2017

KULINDA MAHITAJI YA WATOTO WADOGO KWENYE MIRATHI.

Image result for watoto mirathi

Na  Bashir   Yakub - 

1.NI  WAKATI  GANI  WANATAKIWA  KULINDWA.

Ni  ule  wakati  ambao  marehemu  ameacha  mali  lakini  bado  hajapatikana  msimamizi  wa  mirathi  kwa  ajili  ya   kusimamia  mali  hizo huku  kukiwa  kuna  watoto  wanaohitaji  mahitaji  muhimu  kutoka  katika  mali  hizo.  Pengine hajapatikana  msimamizi  wa  mirathi  kwakuwa  kuna  mgogoro  mahakamani,   au  ndugu  hawaelewani, au  msimamizi  wa  mirathi  aliyeteuliwa  hajulikani  alipo,   au  kuna  utata  katika  wosia n.k. 

Chochote  kile  ambacho  kitasababisha  msimamizi  wa mirathi  achelewe  kupatikana  basi  ujue  ni  wakati  huo  ambapo  mahitaji  na  maslahi  ya  mtoto  yanatakiwa  kulindwa.

2.  YAPI  MAHITAJI  YA  WATOTO  WADOGO.       

Mahitaji  ya  watoto  wadogo  ni  kama  ada  za  shule,  mavazi, matibabu,  na  kila  ambacho  ni  muhimu   kwa  ustawi  wa  mtoto. Na  kwa  suala  la  ada mtoto  si  lazima  awe  mdogo  sana  bali  hata  wale  wa  kidato  cha  tano,  sita,  chuo  nao  waweza  kuwa  watoto  ambao  maslahi  yao  ni  muhimu  kulindwa .

3.  WATOTO  WANAOSTAHILI  KULINDWA.

Watoto  wanaostahili  kulindwa  ni  wale  ambao  watakuwa  ni  warithi  halali  wa  marehemu.  Ni  wale  ambao  hakuna mgogoro  kuwa  ni  warithi  au  si  warithi. Aidha  ikiwa  kuna  mgogoro  kama  watoto  au  mtoto  fulani  ni  mrithi  halali  au  si  mrithi  basi  pia  unaweza  kuomba   kulinda maslahi  yake    ambapo  mahakama  itaamua  ikiwa  anastahili  au  hastahili.

4.  NINI  UFANYE  KULINDA  MAHITAJI  YA WATOTO.

( a )  Mtu  yeyote  mwanafamilia,  ndugu,  mzazi  aliyebaki,mlezi  anatakiwa  kupeleka  maombi  mahakamani   akiiomba  mahakama   kusimamia  baadhi  ya  mali  kwa  muda  ili  kupata  mahitaji  ya  watoto  wakati  wakisubiri  utatuzi  wa  mgogoro  katika  familia.

( b ) Atapeleka  maombi  hayo kwa  kutumia  Fomu  namba  7   ya  Kanuni  za  Mirathi ( The  Probate  Rules).

( c ) Katika  maombi  atataja  tarehe   ya  siku  alipokufa  marehemu   na  wapi  alikuwa  akikaa    kabla  ya  kifo  chake.

( d ) Ataeleza  ikiwa  marehemu aliacha  wosia  au  hapana  na  ikiwa  kuna  mtu  yeyote  amekwisha    fungua  mirathi   katika  mahakama yoyote.

( e )  Ataeleza mali  zilizopo  na  zipi  kati  ya  hizo  anaomba  kuzitumia  ili  kulinda  maslahi  ya watoto/mtoto.

( f  ) Pia  ataambatanisha  kiapo  kwa  kutumia  Fomu  namba  6  ya  kanuni  za  mirathi ( The  Probate  Rules).

( g  )  Baada  ya  hapo atasikilizwa  na  maamuzi  yatatolewa.

5.   UMUHIMU  WA  KUFANYA HIVI.       

Mara nyingi   mtu  anapokufa  kwenye  familia  hubaki  migogoro.  Na  wakati  mwingine  mgogoro  huwa  umefikishwa  hadi  mahakamani.  Mgogoro  unapokwenda  mahakamani  haijulikani  ni  lini  utakwisha.  Haijulikani  utaisha  baada  ya  miaka  mitatu,  miaka  minne  ama  mitano.

Katika  mazingira  yenye  sura  kama  hii ikiwa  kuna  watoto/mtoto  yuko  shule  ambaye  alikuwa  akimtegemea  marehemu  kusoma  ina  maana  hatakuwa na  msaada   na  pengine   itafikia  hatua  atatakiwa  kuacha   masomo.

 Lakini  si  masomo  tu   bali  pia wako  katika  hatari  ya  kupoteza  hata  mahitaji  muhimu   kwakuwa  aliyekuwa  anatoa mahitaji  hayupo  tena.  Hii  ni  kwasababu  haijulikani  mgogoro  utaisha  lini .

Ni  katika mazingira  haya  unapotakiwa  kuchukua  hatua  zilizoelezwa humu  ili  kuyalinda  maslahi  ya  watoto/mtoto kwa  kuwapatia  mahitaji muhimu  kutoka  mali  za  marehemu  kwa   muda  ili   kusubiri  mgogoro  wa  ndugu/wanafamilia  uishe.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA  YA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA   JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com



0 comments:

Post a Comment