Wednesday 18 January 2017

WANAONUNUA NYUMBA ZA MIRADI MUHIMU KUJUA HAYA.


Image result for APARTMENT  PROJECT

NA  BASHIR  YAKUB -

Hivi karibuni kumeibuka  miradi  mingi  binafsi  na  ya  serikali   hasa kupitia  NHC ya  ujenzi  wa  nyumba   za  pamoja. Miradi ipo  kwa  majina  tofauti  ipo  inayoitwa  APARTMENT, CITY,  VILLAGE,  TOWN, n.k. Baadhi  ipo  kigamboni,  Arusha  na  maeneo  mengine .

Pia  ipo  katika  mitindo  tofauti  ipo  ile  ya  maghorofa   ya  kwenda  juu, maghorofa  ya mshazali,  na  ile  ya  nyumba  moja  moja   lakini  katika  eneo  moja (common ground). 

Kutokana  na  hilo  makala yalenga kukufahamisha  usinunue  tu  kwa kupenda  muonekano,mazingira  na  rangi , bali  pia uwe  na  uhakika  wa  faraja(comfortability)  inayotokana  na mambo mengine  nje ya muonekano,  rangi  na  mazingira.

1.TOFAUTI  KATI  YA  NYUMBA  ZA  MIRADI  NA  NYUMBA  ZA  KAWAIDA.

Ipo  tofauti  kati  ya  nyumba  za  kawaida  tulizozoea  na  hizi  za  miradi  zilizotajwa  humu.  Tofauti  ipo  katika ngeli hizi :

( a )   Taratibu  zake  za  ununuzi.

( b )  Vitu  unavotakiwa kujua  kabla   ya  ununuzi. 

( c )   Sheria  zinazozilinda   na, 

( d )  Maisha   yako  baada  ya  kuwa  umenununua.
Makala  yataeleza   vitu  unavyotakiwa  kujua    vinavyotofautisha   nyumba  hizi  na  nyingine za  kawaida.

 2.     VITU  UNAVYOTAKIWA  KUJUA.

( a )   Uwepo  wa  malipo  na  michango  mbalimbali.  Pamoja na  kuwa ni mali  yako umenunua , kanuni  ya  15( 2 )  ya  The  Unit  Title  Regulations, G.N 357/2009  imeeleza   baadhi  ya  michango. Ipo  michango  kwa  ajili  ya  chama  na  uongozi,  michango  kwa  ajili  ya  maeneo  ya  matumizi  ya  pamoja, michango  kwa  ajili  ya  huduma  mbalimbali  mnazotumia  pamoja. 
Michango  hapa haihusishi bili  zako  za  umeme,maji n.k. Michango  hii  inaweza  kuwa  inalipwa  kila  mwezi   au  vinginevyo   kadri  ya  utaratibu  wa  eneo  husika.

Hii  ni  tofauti  na  nyumba  za  kawaida  ambazo  haziko  katika  mfumo  huu  ambapo  ukinunua  umenunua  hakuna  mchango  wa  chama  au  vinginevyo.

( b )    Uwepo  wa  katiba. Tofauti  na  nyumba  nyingine  ukinunua  utaongozwa  na  sheria  za  kawaida  zinazoongoza nchi na watu  wote  hapa  kuna  katiba  maalum  ya  kuongoza  mkusanyiko  katika  eneo  husika.  Kanuni    ya  14   ya  The  Unit  Titles  Regulations, G.N 357/2009  imeeleza  hatua  hiyo  na  kutoa  mfumo  wa  katiba yenyewe  inavyotakiwa kuwa.

Unachotakiwa  kufanya ni  kuwa  soma  katiba  hiyo  na  masharti  yake  kuona  kama  utayaweza au laah. Jambo hili hakuna  nyumba  za  kawaida.

( c )   Uwepo  wa  sheria  ndogondogo( By  Laws). Sheria  ndogondogo  ni  tofauti  na  katiba hapa  juu. Sheria  ndogondogo  zinaanzishwa  na  kifungu  cha 19 cha   The  Unit  Titles  Act,No 16/2008.  Sheria  ndogondogo  zitatungwa  na  uongozi  wa  eneo  la  mradi   wakati  katiba  haitungwi  na  uongozi  wa  mradi  bali  inachukuliwa  kama  ilivyo  kutoka  Kanuni    ya  14( 2 )   ya  The  Unit  Titles   Regulations, G.N 357/2009. 

Umuhimu  ni  kuwa  kabla  hujanunua  pata  sheria  hizo,  zipitie  uone  kama  unakubaliana  nazo  au  lah. Hii  ni  tofauti  na  ununuzi  nyumba  za  kawaida  ambapo  hamna  kitu  kama  hicho.  

( d )  Uwepo  wa  maeneo  ya  pamoja. Ujue  mapema  ni  maeneo  gani  mtatumia  watu  wote  mnaoishi  hapo  na  ikiwa  utapenda  kushiriki (share) maeneo  hayo  au  hapana.  Korido  za  pamoja, maegesho  ya  magari  ya  pamoja, eneo  la  kuogelea  la  pamoja( swimming pool), viwanja  vya  pamoja, na  maeneo  mengine  kadri  chama  na  sheria  zenu  zitakavyoelekeza.

( e )  Uwepo  wa  chama. Ukinunua  ni  lazima  uwe  mwanachama  wa  chama  hicho.  Najua  wapo  wasiopenda  hizi  habari  za  vyama vyama  lakini  hapa  ni  lazima. Kifungu  cha 35  cha   The  Unit  Titles  Act,No 16/2008  kinasema  katika  nyumba  za  namna  hiyo  lazima  kuwe na  chama.

Na  chama  kitakuwa  na  mikutano  ya  wamiliki  na  mtatakiwa  kuhudhuria. Mikutano  inaweza  kupangwa  kila  baada  ya  muda fulani   ambao  uongozi  utaona  unafaa.

( f  )  Uwepo  wa  uongozi. Kifungu  cha 47  cha   The  Unit  Titles  Act,No 16/2008 kinasema  lazima  kuwe  na  uongozi. Kazi  ya  uongozi  itakuwa  ni  kusimamia  katiba  yenu  na  sheria  zenu  ndogondogo ikiwa  ni  pamoja  kuamua  migogoro  ya  maeneo  hayo.

Mmiliki  utatakiwa  kutii  uongozi  huo  na  hauruhusiwi  kupeleka   mgogoro  wowote  unaohsu  eneo  hilo  mahakamani  kabla  ya  kushitaki  kwa  uongozi  kwa  ajili  ya  usuluhishi.  Kifungu  cha 69  cha   The  Unit  Titles  Act,No 16/2008 kinataka  hivyo.

3.  ANGALIZO

Makala  hayalengi  kwa  namna  yoyote  kuzuia  watu  kununua nyumba  za  namna  hiyo, laa  hasha,  isipokuwa  yanalenga  kutanua  mawazo  ya  wanunuzi  kutoka  kupenda muonekano, rangi za majengo  na  mazingira tu,  kwenda mbali  zaidi  kwenye  maisha  ya  jumla  katika  nyumba  za  namna  hiyo.

Pia  ifahamike  kuwa  haya  yote  na mengine  ambayo  hayakuzungumzwa  humu  yapo  kwa  mujibu  wa  sheria  na  hivyo  kila  aina  ya  nyumba  za namna  hiyo  ni  Lazima  haya  yawepo.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI  WA MAKALA  YA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA   JAMHURI   KILA   JUMANNE..   0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment