Tuesday 9 August 2016

MALI ILIYOPATIKANA KABLA YA NDOA

Image result for NYUMBA  NA  MAGARI

NA  BASHIR  YAKUB - 

Mara  kadhaa  linapoibuka  suala  la  kugawana  mali  pale  ndoa  inapohesabika  kushindikana   masuala  kadhaa  ya  msingi  na  yanayohitaji  uelewa  huwa  yanaibuka. 

Moja  ya  suala  kati  ya  masuala  ambayo  huibuka  ni  hili  la  kutenganisha  na  kufafanua  hadhi  ya  mali  za  wanandoa  ili  mgawanyo uweze  kufanyika  kwa  haki. Yawezekana  mwanandoa  akadhani  ana  haki  katika  mali  fulani  lakini  kumbe  kisheria  hana  haki  hiyo  ni mtazamo  wake  ndio  unamsukuma  kuamini  hivyo. 

Halikadhalika  yawezekana  mwanandoa  kudhani  hana  haki  katika  mali  fulani  kumbe  anayo  haki.  Ili kujua    una  haki  ipi katika  mali  ipi  na  huna  haki  katika  mali  ipi yahitajika  kujua  misingi  ya kisheria  inayotumika  kugawanya   mali  za  wanandoa.

1.KUGAWANA  MALI  ZA  WANANDOA.

Ieleweke  kuwa  tunapoongelea  wanandoa  kugawana  mali  tunaongelea  talaka. Hakuna  kugawana  mali  bila  talaka. Na  kisheria  talaka  inapotoka  tu swali linalofuata ni  habari  ya  mali  na  watoto  kama  wapo.  Mali  si  lazima  magari  na  manyumba  lakini  pia hata  vyombo  vya  ndani  vikiwemo  vitanda, makabati, sahani  n,k  nazo  ni  mali  kwa  mujibu  wa  sheria. Navyo  huhitaji mgao.

2.  JE  KUGAWANA  MALI  NI  NUSU  KWA NUSU ?.

Linapokuja  suala  la  kugawana  mali  wengi hudhani mtindo unaotumika  kugawa  ni  ule  wa    nusu  kwa  nusu.  Jambo  hili  si  kweli  kwakuwa  sheria  ya  ndoa 1971 iliyofanyiwa  marekebisho  2002  haisemi  kuwa  utaratibu  wa  kugawana  mali  ni nusu  kwa  nusu. Sheria  hii  imeweka  msingi  mkuu  wa  kugawana  mali  ambao  ndio  hutumika  katika  mahakama  zetu  katika  kutoa  maagizo  ya  kugawa  mali  za  wanandoa.  

Msingi  uliowekwa  na  sheria  ni  msingi  wa  kiwango  cha  mchango  wa  mwanandoa  katika  kupatikana  kwa mali  husika.  Kiwango  alichochangia  mwanandoa  katika  kupatikana kwa  mali hiyo  ndicho  kitakachokadiriwa  na  kiwango  hicho ndicho atakachopewa. 

Kwa hiyo  kama  ni  nyumba  ya  vyumba  sita  mmoja  anaweza  kupata chumba  kimoja  na mwingine  akapata  vitano kutegemea  na  mchango  wake. 

Na  mchango  hapa  sio  leta  ni lete. Mchango  sio  hela  tu  hata  kazi  za  nyumbani  anazofanya  mama  wa  nyumbani  ambaye  haleti  hela  nazo  huitwa  mchango  ambapo  hukadiriwa  na  kupata  kile  anachostahili.

3.  MALI  KABLA  YA  NDOA  NA  BAADA  YA  NDOA.

Katika  kutenganisha  mali  za  wanandoa   huwa  zinatenganishwa  katika  makundi  makuu  matatu. Kwanza kuna  mali ambazo  mtu  alikuwa  nazo  kabla ya  ndoa   na  wakati  anaingia  katika  ndoa  ameingia  nazo. Kwa  mfano  mwanamke  ameolewa  akamkuta  mwanaume  tayari  ana  nyumba  yake. Pili  kuna  mali  ambazo  zimepatikama  wakati  wawili  wakiwa  katika  ndoa . Kwa  mfano  ndoa  imefungwa  wawili  wakaanza  kuishi  pamoja  na  taratibu wakaanza  kujenga  na  kukamilisha. 

Na  tatu ni  mali  ambazo  zimepatikana  katika  ndoa  lakini zikiwa  hazina  uhusiano  wowote   wa kindoa kwa  mfano kurithi  au  kuzawadiwa mali. Tutaona hapa  chini  mazingatio  ya  sheria  ya  kila  moja  katika  haya.

4. JE  MALI  ILIYOPATIKANA  KABLA  YA NDOA  INAHESABIKA  NI  YA  FAMILIA.

Mali iliyopatikana  kabla  ya  ndoa  na  ikaendelea  kuwepo  kipindi  cha  ndoa inaendelea  kuwa  ya  huyo  mwenye  nayo bila  ushirika  wa  mwenza  wake. Kama  ni  nyumba  mwanamke  alikuwa  nayo  kabla  ya  kuolewa  au  ni  mwanaume  alikuwa  nayo  kabla  ya  kuoa  basi  inaendelea  kuwa  ya kwake  peke  yake  na  haihusiki  katika  mgao  suala  la  mgao  linapojitokeza.

Hata  hivyo  inaweza  kuingizwa  katika  mgao  ikiwa  kuna  mchango  wowote  wa  kuiendeleza uliotolewa  na  mwenza. Kwa mfano  kabla  ya  ndoa  ilikuwa na  vyumba viwili  lakini  katika  kipindi  cha  ndoa  imepanuliwa  na  kufikia  vyumba  vitano,  au  ilikuwa  haina  uzio, au  haina  madirisha  kabla  ya  ndoa  lakini  baadae  vitu  hivi  vikawepo. 

Katika  hali  kama  hiyo  itatakiwa  iingizwe  katika  mgao  na  kutazama kiwango cha  mchango wa  kila  mmoja  katika  uendelezaji  huo.  Ni  hapo  ambapo  mchanganuo  utafanyika ili  kila  mmoja  apate  haki  kutokana  na  kiwango  cha  mchango  wake.

Ikiwa  hakuna uendelezaji  wowote  uliofanyika  katika  mali  yaani  labda  nyumba ilivyokuwa  kabla ya  ndoa  ndivyo  hivyohivyo  ilivyoendelea  kubaki  hata  baada  ya  ndoa  basi  mali  hiyo  haitatakiwa  kuingizwa  katika  mali  za  mgao  bali  itabaki  mali  ya  mwanandoa  mmoja  pekee  ambaye  ndiye  mmiliki  wa tangu  awali.  

Hali  ni  hiyo  hiyo  hata kwa  mali  ambayo  imepatikana  katika  ndoa  lakini  ikiwa  haina  uhusiano  na  kipato  cha  wanandoa,  kwa  mfano  mali ya urithi au  zawadi. Hii  ina  maana ikiwa  mali  hii  itaendelezwa  basi mchango  wa  uendelezaji  utatathiminiwa  na  ikiwa  haitaendelezwa  basi  itabaki  mali  ya  mrithi  au  mpewa  zawadi  pekee  na  haitahusu  mgao.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI   WA  MAKALA  YA SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI  KILA  JUMANNE..   0784482959,  0714047241  bashiryakub@ymail.com

0 comments:

Post a Comment