Wednesday 3 August 2016

JE UMEZAA MTOTO NJE YA NDOA, FANYA HAYA ILI KUMWEZESHA KURITHI BAADA YA KIFO CHAKO.

Image result for MTOTO


NA  BASHIR  YAKUB - 

Unao  watoto  wa  namna  mbalimbali. Unao  uliowazaa  ndani  ya  ndoa  na  wale uliowazaa  nje  ya  ndoa. Unawapenda  sana  wote  kwa  usawa kwasababu wote  ni  watoto  wako. Kuna  suala  la  kifo  na  ungependa  baada  ya  kifo  chako  watoto  wako  wote  wafaidi  kidogo  ulichochuma. Lakini  je  hilo umelijengea  mazingira.

Ni  muhimu  sana  ujue  kuwa  suala la  watoto  wako  kufaidi  ulichonacho  halitokani  na matakwa  yako, laa  hasha  bali  linatokana  na matakwa  ya  sheria. Wewe  waweza  kuamua  watoto  wako  wote wa  nje  ya  ndoa  na  wale  wa  ndani  ya  ndoa  wapate mali  lakini  baadhi  wakakosa  kutokana  na  msimamo wa sheria.

Ni hapo  unapotakiwa  kuandaa  mazingira  yanayoendana  na  matakwa  ya  sheria  ili  watoto  wako  wote  waweze  kufaidi  machumo yako.

1.FANYA HAYA  ILI  KUWAWEZESHA  WATOTO  WA NJE  YA  NDOA KURITHI.

a. KWA  WAISLAMU.

Kama  wewe  ni  muislam  na  una  mtoto/watoto  nje  ya  ndoa  hakikisha  unaandika  wosia   ambao   utampatia  mali  hata  huyo  mtoto  wa  nje  ya  ndoa. Lakini   lazima  ujue  kuwa  mali  yako  yote uliyonayo  ni 3/3 = (100%).  Hivyo  2/3 ya  mali  yote  ni  lazima  iende  kwa  warithi  halali  ambamo  mtoto  wa  nje  ya  ndoa  hataingia  kabisa.  

Katika  mali  hiyo  ya  2/3 wala  haihitaji  wosia  kwakuwa  tayari  sheria  ya  kiislam  imeeleza  vipi  hiyo  mali  igawanywe.

Uhuru  wako  wa  kugawa mali  kwa wosia upo   katika 1/3 basi  na  si  vinginevyo. Na  ni  kusema  kuwa mtoto/watoto  wa  nje  ya  ndoa  haki yao  ipo  katika  1/3 tu. Ikiwa utampatia  mali  zaidi   ya  1/3  basi anaweza  kunyanganywa .  Kwahiyo  uelewe  kuwa  wosia  utakaoandika  unahusu  1/3 ya  mali  tu. 

Zingatia kuwa  usipoandika  wosia  kugawa 1/3  yote au  sehemu  yake  kwa  mtoto/watoto  uliowazaa  nje  ya  ndoa  basi  hawatapata  mali  kabisa baada  ya  kifo  chako.  Na  hii  ni  kwasababu  watoto  hao  hawaruhusiwi  kurithi  kisheria. 

Kwahiyo utaona kuwa  unachotakiwa  kufanya   ili  hao  watoto  wasikose  ni  kupiga  hesabu  ili  kupata  1/3  ya  mali  yako  na  kuwapa  yote  au  sehemu  yake.

b. KWA  WANAOISHI  MAISHA  YA KIMILA.

Karibia  taratibu  za  kimila  zote  haziruhusu  watoto  wa  nje  ya  ndoa kurithi.  Hii  ina maana  ikiwa  unaishi  maisha  hayo  na  unakufa   hawa  watoto  hawatarithi. Unachotakiwa  kufanya  ili  waweze  kurithi  hata  baada  ya  kifo  chako  ni kuwahalalisha  watoto  hao kabla  hujafa.

Utaratibu  wa  kuwahalalisha  watoto  wa  nje  ya  ndoa  hutofautiana katika  mila  na  mila. Utakachofanya  ni  kufuata  utaratibu  wa  mila  yako  kama  ulivyo  na  kuwahalalisha  watoto hao.  Usiseme  nitaandika  wosia   niwape  mali  hapana. Hii  ni  kwasababu  wosia wataupinga  kuwa  ni  wosia  uliokiuka  taratibu kwa kuwarithisha  wasiostahili. Kinachotakiwa  ni  kuwahalalisha  kwa  mujibu  wa  mila  yako.

c. KWA  WASIO  WAISLAM NA  AMBAO  HAWAISHI  MAISHA  YA  KIMILA.

Hawa  mara  nyingi  ni  wakristo . Sheria  inayotumika  kwao  ni  sheria ya  Urithi  ya  Mwaka 1865. Sheria  hii  nayo  inakataza  mtoto  wa  nje  ya  ndoa  kurithi. Hivyo  basi ili  kumwezesha  kurithi   unatakiwa  kuwa  umeandika  wosia  ambapo utawapatia mali.

Ikiwa  utakufa  bila  kuacha  wosia  hata  kama  ulikuwa  unaishi  nao  hawataruhusiwa  kurithi.  Kinachotakiwa  ni  uandike  wosia   na  wao  uwajumuishe  humo.
Pia  lakini  hii  ni ziada  ni  vema  kuwa  umewatambulisha  kwa  ndugu  zako,  wana  ukoo  na  hata  mke  kama  unaye.

Yote kwa  yote ifahamike kuwa ni  muhimu  kuweka  maandalizi  ya  kisheria katika  suala  la  mirathi. Usipofanya  hivyo  usitegemee   watoto/mtoto wa nje ya ndoa kurithi  mali  zako  lakini  pia  ujue  utakuwa  umekufa  huku  umeanzisha  mgogoro  mkubwa  katika  familia.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI   WA  MAKALA  YA SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI  KILA  JUMANNE..   0784482959,  0714047241  bashiryakub@ymail.com





.  

0 comments:

Post a Comment