Tuesday 23 August 2016

KUNUNUA KIWANJA/NYUMBA FUATA HATUA HIZI ZA KISHERIA

Image result for viwanja nyumba
NA  BASHIR   YAKUB -

Mara  nyingi  nimeandika  kuhusu  ardhi  hususan   viwanja  na  nyumba.  Katika  kufanya  hivyo  mara  kadhaa  nimejaribu  kuwatahadharisha  watu namna  mbalimbali  ya  kisheria ya kuepuka   kuingia  katika  migogoro  ya  viwanja  na  nyumba  hasa  wakati  wa  kununua( wanunuzi). 

 Nimewahi  kueleza  namna  au  vitu  vya  msingi ambavyo  hutakiwa  kuwa  katika  mkataba  wa   ununuzi  wa  nyumba  au  kiwanja. 

Nikaeleza  umuhimu  wa  kila  kimoja   na nikasisitiza  kuwa  atayekuwa  amenunua  ardhi na  mkataba  wake  ukajaaliwa   kuwa  na  vitu  hivyo  basi  si  tu  atakuwa  amefanya  manunuzi  bora  lakini  pia  atakuwa  amefanya manunuzi  yanayokubalika  kisheria.

Ifike  hatua  watu waelewe kuwa  migogoro  mingi  ya  ardhi  huanzia  na  kutokuwa makini kwenye  manunuzi. Kutokupata  ushauri  wa  kisheria   ikiwa  ni  pamoja  na  kutopitia  hatua   za  msingi za kisheria  kabla  ya  manunuzi,  kuandikiwa  mikataba ya  manunuzi  isiyokidhi  vigezo  vya  kisheria  ikiwemo  ile  ya  serikali  za  mitaa  ambayo  hairuhusiwi  kabisa kisheria  ni  kati  ya sababu chache  kati  ya  nyingi  zitakazokupelekea  uingie  katika  mgogoro. 

Leo  nitaeleza  hatua  moja   ya  msingi  sana  ambayo  hutakiwi ufanye  manunuzi  ya  ardhi  bila  kuipitia.

1.HATUA  TANO  ZA  KUFUATA   UNUNUAPO   NYUMBA/KIWANJA. 

Ziko  hatua  tano  muhimu  za  kupitia  pale  unapo kuwa  katika  mchakato  wa    kununua  ardhi. Umuhimu  wa  hatua  hizi  ni  kuwa  kwanza  kabisa  si  rahisi  kujikuta  katika  mgogoro  unapokuwa    umezipitia.  

Lakini  pili  hata  bahati  mbaya   utokee  mgogoro   basi  wewe  uliyepitia hatua  hizo  utakuwa  salama  na  kama  ni  kesi  basi  wewe  upo  katika  mazingira  mazuri  ya  kushinda.  

Hatua  ya  kwanza  huitwa  hatua  kabla  ya  mkataba( pre contractual  stage). 

Hatua  hii inayo  mambo  yake  ya  msingi  na  ya  kisheria     ambayo  kuyafuata  kwako  kwaweza  kukuweka  mbali  na hatari  ya  kununua  ardhi  yenye  mgogoro  au  itayokuingiza  katika  mgogoro  .

 Hatua  hii  ndiyo  nitakayoeleza   kama  msingi  wa  makala  ya  leo  kama  tutakavyoona.  Kabla  ya  kueleza  hatua  hiyo  ni  vema  pia  nikazitaja  hatua  nyingine   japo  kwa  ufupi. 

Hatua  ya pili  huitwa  hatua  ya  mkataba( contractual  stage). Hii  ni  hatua  ya  kupitia  na  kujiridhisha  na  mkataba    wa  manunuzi  ikiwa  ni  pamoja  na  kuusaini. 

Hatua  ya  tatu  huitwa  “pre completion  stage”,  hatua  ya nne  huitwa  hatua  ya  kumalizia ( completion stage)  na  hatua  ya  tano  na  ya  mwisho  huitwa  hatua  baada  ya  kumalizia ( post  completion  stage).

2.  USINUNUE  NYUMBA/KIWANJA  BILA  KUPITIA  HATUA  HII.

Kama  nilivyoeleza  hapo  juu  hatua  nitakayojadili  hapa  huitwa  hatua  kabla  ya  mkataba au “pre contractual  stage”.  Jambo  kubwa   ambalo  huhusishwa  katika  hatua  hii  ni  kufanya  utafiti  wa kitaalam  uitwao “official  search” . 

Katika  hatua  hii  mlengwa  anayetaka  kununua ardhi  kupitia  ofisi  ya  mwanasheria  ataandika  barua  kwenda  kwa  msajili  wa  ardhi  kumuuliza  taarifa  kamili  za  nyumba  au  kiwanja  anachotaka  kununua. 

Msajili  wa  ardhi atapekua  katika  kumbukumbu  zake  rasmi  na  kutoa  majibu  sawa  na  kile  kilicho  katika  kumbukumbu  zake.

3.  MAMBO  MUHIMU  UTAKAYOULIZA  KWENYE   BARUA  YA   MSAJILI.

Kwanza  katika  barua  yako  utahitaji  kujua   jina la mmiliki  linalosomeka   katika  nyaraka  za  serikali. Hii  itakusaidia  kulinganisha  jina  la  anayekuuzia  na  lile  linasomeka  katika  kumbukumbu   za  serikali. 

Kwa  kujua  jina  tu utaepuka kununua ardhi  kutoka kwa mtu  ambaye  si  mmiliki  halisi. 

Pili  utahitaji  kujua  iwapo  ardhi  hiyo  imewekwa  kama  dhamana  popote  katika  taasisi  za  fedha. Kama  imewekwa  dhamana  basi  taarifa  zitaonesha. Hii  ni  kwasababu  taasisi  za  fedha  hutuma  taarifa  kwa  msajili  wa  ardhi  katika  kila  ardhi  inayowekwa  kwao  kama  dhamana.  

Tatizo  la  kununua  ardhi  iliyowekwa  dhamana  bila  kujua  ni  aidha  ukubali  kuingia  hasara  kulipa  deni  ili  nyumba  ubaki  nayo  au   uwe  mpole  nyumba  uliyonunua  iuzwe  upate  hasara. 

Tatu  utaweza  kujua  iwapo  ardhi  hiyo  ni  ya  wanandoa   hasa  iwapo  wanandoa hao   wana  mgogoro. Hii  ni  kwasababu   sheria  humpa  haki  mwanandoa  kuweka  zuio  katika  ardhi  ya  familia  iwapo  mmoja  wao ana  wasiwasi mwenzake   anaweza  kuuza ardhi  hiyo. 

 Kwahiyo  ikiwa  taarifa  kama  hizo  tayari  zimepelekwa  ardhi   basi  utakapopitia  hatua  hii  kabla  ya  kununua  utaoneshwa  taarifa hizo  na  hivyo  kuepuka  kununua mali  ya  familia  kitu   ambacho  ni  kama  kupoteza. 

Nisisitize  kuwa hatua hii  ni  muhimu  sana  kwakuwa ni  hatua  pekee  ya kujiridhisha  na uhalali  wa  ardhi  unayotaka  kununua. Nathubutu  kusema  kuwa  usinunue  kiwanja/nyumba  bila  kupitia  hatua  hii.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI   WA  MAKALA  YA SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA JAMHURI  KILA  JUMANNE..   0784482959,  0714047241  bashiryakub@ymail.com

1 comments:

  • Paul Mdiya0 says:
    13 April 2020 at 05:15

    asante kwa ushauri na somo lenye manufaa. je nawezaje kupata kitabu cha sheria ya ardhi ?

Post a Comment