Tuesday 12 July 2016

JE WE NI MFANYABIASHARA, JE UNALINDA BIASHARA ZAKO NA WARRANTY.



Image result for WARRANTY
NA  BASHIR  YAKUB - 

1.WARRANTY  NININI  KATIKA BIASHARA.

Warranty  ni  mkataba  kati  ya  mtengeneza  bidhaa  na  mnunua  bidhaa  ambaye  naye  anakwenda  kumuuzia  mtu  wa tatu( mteja). Kunakuwa  na  watu  watatu. Kwanza  ni mtengeneza bidhaa, pili  ni  mnunua  bidhaa  ambaye naye  anakwenda  kuuza(mfanyabiashara)  na  tatu  ni  mnunua  bidhaa (mteja)  anayenunua  kwa  ajili  ya  matumizi.

Kwa  mfano  una  duka  la  simu  kariakoo, we  ni mfanyabiashara.  Yule  aliyekuuzia  simu   kwa mfano  tecno company  huyo  ni  mtengenezaji.   Na anayekuja  kariakoo kununua  simu  kwa  ajili  ya  matumizi   huyo ni  mteja. Kwahiyo  kisheria  Warranty  ni   mkataba  kwa  ajili  ya  hawa  watatu katika kuhakikisha  ubora na  ufanisi  wa  bidhaa.

2. JE  MIMI  KAMA  MFANYABIASHARA NINALAZIMIKA   KUANDIKIWA  MKATABA  WA WARRANTY .

Ndio  unaponunua  bidhaa  popote kwa  ajili  ya  kuuza  tena  ni  lazima  uwepo  mkataba  wa  warranty . Ni  mkataba  wa  warranty  pekee  utakaokuweka  salama  na  bidhaa  uliyonunua. 

Mfanyabiashara  sio  mtengeneza bidhaa  na  hivyo   kwake  sio  rahisi  kujua  ubora, muda  wa  kuishi  wa  bidhaa,pamoja   na  mambo  mengine  yanayohusu  uimara   na  ufanisi  wa  bidhaa  katika  matumizi. 

Ni  kutokana  na  hilo  analazimika  kupata  mkataba  wa  warranty  ambao  ndio uhakiki  na  ithibati  ya ufanisi  na  ubora  wa  bidhaa.

3. JE  KUNA TOFAUTI  KATI  MKATABA  WA  KUNUNUA  BIDHAA  NA  MKATABA  WA  WARRANTY.

Ndio  kuna  tofauti. Mkataba  wa  kununua  bidhaa   ni mkataba  wa  kununua  kama neno lilivyo  na  hueleza kuhusu  manunuzi. Wakati  mkataba  wa  warranty  ni  mkataba  ambao  hauelezi  jambo jingine  lolote  isipokuwa  ubora  katika  matumizi  ya  bidhaa,  ufanisi  wake, muda  wa  matumizi,  na  kila  jambo  linalohusu uimara  na umathubuti  wa  bidhaa.

Pia lazima  ueleze  nini  kitatokea  iwapo  bidhaa  haitafanana  na maelezo   hayo. Ikiwa  bidhaa  itarejeshwa, au  pesa  ya  manunuzi  itarejeshwa  au vinginevyo, ni  lazima  ielezwe. Hii  ndio  huitwa  “warranty  contract.”.

4. JE  WARRANTY  KWA  MDOMO  INAKUBALIKA  KISHERIA.

Ndio  inakubalika  ila  sio  nzuri  kisheria.  Warranty  nzuri  inayoweza  kukusaidia  kubadilishiwa  bidhaa kwa kupewa  nyingine  au  kurudishiwa  fedha  ikiwa  kuna  tatizo  ni  warranty  iliyo  katika  maandishi. Hii  ni  rahisi  kuithibitisha  kuliko  ile  ya  mdomo.

Warranty  ya  mdomo  inahitaji  uwe  na  mashahidi    waliosikia   mtengeneza  bidhaa  akiitoa. Jambo  hili  laweza  kuwa  gumu. Hivyo ni muhimu  kuwa na  mkataba   wa  warranty  wa  maandishi.

5. KUNA  TOFAUTI  GANI  KATI  YA  WARRANTY NA  GUANRANTEE.

Warranty  hutolewa  na  mtengeneza  bidhaa  wakati  guarantee  hutolewa  na  muuza  bidhaa(mwenye duka). Ukienda  kariakoo  kununua  simu  mwenye  duka  atakupa  guarantee. Yeye  anapata  warranty  wewe  anakupa  guarantee.

Na  guarantee  sio  lazima  iandikwe  ila  sheria  inaamini  unapomuuzia  mteja  bidhaa kwa matumizi ni  lazima  iwe  bora  na  imara  na  kinyume  chake  unatakiwa  kumpa  bidhaa  nyingine au  kumrudishia mteja  fedha  yake. 

Ni  jambo  hili  linalomlazimu  mfanyabiashara  kupata  warranty ili  mteja  akirudisha  bidhaa  basi  naye  airudishe  kwa  mtengenezaji  kupitia  mkataba  wa warranty.  Lakini  kama  hana  mkataba  wa warranty  ina  maana  atalazimika kutoa  hela  yake mfukoni  kumrudishia  mteja.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MWANDISHI   WA  MAKALA  YA SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI  KILA  JUMANNE..   0784482959,  0714047241  bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment