Wednesday 11 May 2016

JE KUNA SHERIA ASKARI POLISI/JESHI WASILIPE NAULI.

Image result for daladala

NA  BASHIR  YAKUB - 

Mara  kadhaa  nimeliona  hili.  Hata  we  pia  ni  imani   umeliona.  Tunaliona hili  katika  vyombo  vyetu  mbalimbali  vya  usafiri .Tunashuhudia   askari  wetu   wakikataa  kutoa  nauli.  Na hii  ni  kwa jeshi, polisi ,  magereza   na hata  wale  wa  barabarani.  Hata hivyo  sio wote wapo  wanaotoa  .  Na zaidi hawatoi wakiwa  wamevaa  sare.

Lakini  mbona  hawatoi  kwenye  magari tu na si  kwenye Fast jet au Emirates. Sijui  ni kwanini.

Tunahitaji  ufafanuzi  wa  kisheria  kulijua  hili. Tunahitaji  maelezo   ikiwa  inaruhusiwa  kwao  kufanya  hivyo  au  hapana.

1.SHERIA  INAYOONGOZA  JESHI  LA  POLISI.

Jeshi  la  polisi  hutekeleza  kila  jukumu  lake  kwa  mujibu  wa  sheria.  Sheria  kuu  inayoongoza majukumu  yao   ya kila  siku  hujulikana  kama  Sheria  ya  Jeshi  la  Polisi   sura  ya  322.  Humu  umeelezwa  wajibu  na  haki  zao.  Imeelezwa  nini wafanye , nini wasifanye na nini wafanyiwe.

Sambamba  na  sheria  hiyo  pia  zipo  sheria  nyingine  ambazo   hueleza  wajibu  wao  katika  majukumu yao.  Ipo  sheria  ya  kanuni  za  adhabu  sura  ya  16,  ipo  sheria  ya  mwenendo  wa  makosa  ya  jinai   pamoja  na  sheria  ya  ushahidi. Hii  ni  kwakuwa hawa hushughulika  na   makosa  ya  jinai .

Kwa  hiyo  kama  kuna  jambo  lolote  tunahitaji  kujua  kuhusu  hawa basi tunataraji  kulipata  katika  sheria  hizi.  Na  kama  halipo  humu  basi  itabidi   watueleze walikolipata.

2.  SHERIA   YA  JESHI  LA  WANANCHI.

Jeshi  la wananchi  nao  wanayo majukumu  na haki zao za  kisheria. Kubwa kwao ni  kulinda  mipaka.  Wao  nao  wanazo  kanuni  na sheria  zinazowaongoza.  Moja  ya  sheria inayawaongoza  ni  ile  ijulikanayo  kama  The  National  Defence   Act 1966. 

Kwa hiyo  ikiwa  kuna lolote tunahitaji  kujua  kama  ni  haki  yao basi  tunataraji  kulipata katika  sheria  zinazowaongoza  pamoja  na sheria nyinginezo.Kama  halimo  tutahitaji  maelezo  walikolipata.

3. SHERIA  YA  MAGEREZA.

Magereza  nao  ni  sehemu  ya majeshi  ya  usalama.  Kazi  yao  kubwa  ni   kiusimamia  shugughuli  zote  zinazohusu  wafungwa.  Sheria  inayotumika  katika majukumu  yao   huitwa  The  Prison Act, 1967.

Kwa hiyo  ikiwa  kuna lolote tunahitaji  kujua  kama  ni  haki  yao basi  tunataraji  kulipata katika  sheria  zinazowaongoza  pamoja  na sheria nyinginezo.Kama  halimo nao  tutahitaji  watueleze  walikolipata.

4. JE  KATIKA  SHERIA  HIZI  KUNA  SEHEMU  WAMEZUIWA  KULIPA  NAULI.

Hapana,  hakuna  kifungu  chochote katika  sheria hizo  kinachokataza  askari  polisi, jeshi,  au  magereza  kutolipa  nauli.  Yapo  mambo  yanayokatazwa  katika  sheria  hizo  lakini  suala  la  nauli  si  sehemu  ya  hayo  mambo.  
Wakati  mwingine  ni  vigumu  kujua  jambo  hili  lilitoka  wapi  katika  nchi  inayofuata   utawala    wa  sheria.

5. SHERIA  YA  SUMATRA.
Mamlaka  ya  usafiri  wa  nchi  kavu  na  majini  huitwa  SUMATRA. Hawa  kazi  yao  pamoja  na mambo  mengine  ni  kuratibu  taratibu  za  usafiri  wa  nchi  kavu  na  majini .
Usimamizi na uratibu wa nauli ni sehemu ya majukumu  yao.  Sheria  kuu inayowaongoza  huitwa  The Surface and Marine Transport Regulatory  Authority Act. Ni  sheria  namba  9 ya  2001.

Sheria  hii  husomwa  na kanuni  za  SUMATRA.  Si  ndani  ya  kanuni  hizo  wala  hiyo sheria   kunamoelezwa   askari   jeshi  na  polisi  wasilipe  nauli. Jambo  hilo  halipatikani  kabisa.

6. BASI KUTOLIPA  NAULI  IWE  HISANI.

Sisemi  ni  vibaya  kutolipa  nauli  kwa  makundi  haya.  Ninachosema ni  kuwa  iwe  hisani.  Ikiwa  hisani  maana  yake  ni  kuwa  anayetaka  atawatoza  na  asiyetaka  hatawatoza. Ni  kosa  kwao  kulifanya  jambo  hili la lazima na la kisheria. Na  hapo  ndipo lilipo  tatizo. Kumlazimisha mwenye chombo cha usafiri asikutoze nauli hakukubaliki.

Kutolipa nauli  si  haki  ya  yeyote kwa mujibu wa sheria.Hata amiri  jeshi mkuu rais Magufuli  akipanda gari lazima alipe nauli. Hakuna  aliye  juu  ya  sheria. Wao  ni  watumishi  kama  walivyo  watumishi  wengine  wote.  Na  kila  mtumishi  ana umuhimu  wake.

Lakini  pia  kila mtumishi  fulani  anategemea kazi inayofanywa na mtumishi  mwingine  ili  aishi.  Kitu hiki  hufanya  kila  idara  kuwa  na  umuhimu  wake  wa  pekee.Kwa hiyo  kila idara  ni  muhimu tena  sana.

Ni kwa mantiki hii  hatuwezi  kusema  idara  fulani  ilipe  nauli  na  idara  nyingine  isilipe  kwakuwa ni  ya muhimu  zaidi, hapana.Na  kama  hilo  litakuwepo  litakuwa ni  kwa  makubaliano na  mipaka  maalum  kama lilivyo  lile  la  waalimu  wa Dar  es salaam.

Kutokana  na  haya  yafaa  wenye  vyombo  vya  usafiri  wawatoze  nauli  hawa. Ikiwa  hawatawatoza  iwe  ni  kwa  hiari  lakini isiwe  lazima  au  kwa  shinikizo.
Makondakta  na  wenye  magari hawapaswi  hata  kidogo  kuogopa  kudai  nauli  kutoka  kwa  makundi  haya  kwani  hiyo  ni haki  yao  ya  msingi  kama  ilivyo  kwa  abiria  wengine wote. Inakera  sana  kuona  jambo  hili linafanywa  la  lazima na baadhi  ya  askari na wanajeshi.

Hatua unazoweza kumchukulia  abiria  ambaye hajalipa nauli ndizo unazoweza kuyachukulia makundi haya yasipolipa nauli.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com





0 comments:

Post a Comment