Wednesday 13 April 2016

WAWEZA KUMSHITAKI ASKARI ALIYEKUKAMATA/KUKUWEKA NDANI BILA SABABU ZA MSINGI.

Image result for AKIWA  CHHINI  YA  ULINZI

NA  BASHIR  YAKUB - 

Wapo  baadhi  ya  askari  hutumia  nafasi  zao  vibaya. Wapo  wanaojua na  kutekeleza  wajibu  wao  wa  kisheria  na  wapo  wasiotekeleza  wajibu  wao  wa  kisheria. Raia  hulalamika  sana.  Moja ya maeneo  makubwa  yanayolalamikiwa  ni   hili  la  kukamatwa  bila  sababu  za  msingi/kuwekwa  ndani  bila  sababu  za  msingi na  wakati mwingine kufunguliwa  mashtaka  bila  sababu  za  msingi.

Leo  sio  ajabu  askari  kugombea  mwanamke  na  mwanaume  mwenzake  halafu  akamtafutia  sababu  na  kumweka  ndani  au  akambambika shitaka   bila  kosa  lolote. Leo  sio  ajabu kutupiana  maneno  mawili  matatu  na  askari  halafu  ghafla ukaambiwa  umekamatwa  na  bunduki, leo  sio  ajabu  mwenye  hela  kuamua amfunge  nani kwa kutumia  askari . Matukio ni  mengi  yanayofanana  na  haya.

1.KUENDELEA  KWA  MATENDO  YA  KUKAMATWA/KUWEKWA NDANI  BILA  SABABU  ZA  MSINGI.

Hakuna  shaka  matendo  haya  yameendelea  kwasababu  wanaotendewa  huwa  hawachukui  hatua.  Mtu  anakamatwa  anawekwa  ndani  bila  sababu  za  msingi akiachiwa  anashukuru  na kuondoka. Mwingine  anabambikiwa  kesi  inamtesa miaka na miaka ikiisha  anashukuru na kuondoka.  Namna  hii  haiwezi  kuwa suluhu. Kama  hii  itakuwa suluhu  basi  wengi wajiandae kuumia.

Makala  yanazungumzia  kukamata au  kuweka  ndani  bila  sababu  za  msingi( false imprisonment/arrest). Hii  isichanganywe  na kumshitaki  mtu  bila  sababu  za  msingi( malicious prosecution).  Japo  kwa  namna  fulani  yanafanana  lakini  makala  haizungumzii  kushitaki  bila  sababu  za  msingi.

2. NINI  MAANA  YA  KUMWEKA  NDANI  MTU /KUMFUNGA  BILA  SABABU  ZA  MSINGI.

Kumweka  ndani  mtu/kumfunga   bila  sababu  za  msingi  ni kumzuia  mtu bila  hiari  yake  na  bila  sababu  za  msingi.  Kuweka  ndani  ndio  kufunga. Na  kufunga  kisheria  sio  lazima  mtu  aingizwe  selo. Kuzuia  uhuru  wa  mtu  kunatosha  kuitwa  kufunga  kisheria.  Ndio  maana  kufunga  mtu  inaweza  kuwa  kwa  maneno  , kwa  matendo au  vyote.  

Kitendo  cha  askari  kumwambia  mtu  uko  chini  ya  ulinzi  hata  kama  hajamgusa  tayari  ni  kumfunga. Ni  kumfunga  kwasababu  tayari  mtu amepokonywa  uhuru  wake  na  hivyo   hawezi  kuendelea  na  shughuli  zake.

Hivyo  ni  vema  kujua  kuwa  unaweza  kumshitaki  askari  hata  kwa  kukwambia   tu  kuwa uko  chini  ya  ulinzi  kama amefanya hivyo bila  sababu  za  msingi na  kwa  hila( maliciously).

3. JE  KUTOMPELEKA  MTUHUMIWA  MAHAKAMANI  NI  KUFUNGA  BILA  SABABU  ZA MSINGI.

Mtuhumiwa aliyewekwa  ndani   zaidi  ya  masaa  24  bila  kupelekwa  mahakamani  naye  anahesabika  katika  wale  waliofungwa  bila  sababu  za  msingi  hivyo  anaweza  kuwafungulia  mashtaka askari  wa  kituo  kwa  kufanya  hivyo.

Sheria  iko  wazi  kuwa  ikiwa mtuhumiwa alipokamatiwa  ni  karibu  na  mahakama  na  hakuna  umbali  wa  kusababisha   kucheleweshwa  kufikishwa  mahakamani  basi  ndani  ya  muda  mfupi  inatakiwa  mtuhumiwa  afikishwe  mahakamani.

Ikiwa  hilo  halitafanyika  na  huku  lilikuwa  linawezekana  basi  kuendelea  kuzuiliwa  ni  kosa  ambalo  mtendewa  anaweza  kuwashitaki wahusika.  Hii  ni  kwasababu  kutofikishwa  mahakamani   kwa  wakati  kumetafsiriwa  kama  kufungwa au  kuzuiliwa  bila  sababu  za  msingi( false  imprisonment).

4. NAMNA  YA  KUSHITAKI.

Utafungua  shauri  la  madai ya  fidia. Mshitakiwa wa  kwanza  atakuwa  askari  aliyekukamata  au  kukuweka  chini  ya  ulinzi. Hata  wawe  sita  wote  kwa  pamoja  watakuwa  washitakiwa  wa  kwanza.  Wa  pili atakuwa  mkuu  wa  jeshi  la  polisi  na  wa tatu  atakuwa  mwanasheria  mkuu  wa  serikali.

Mkuu  wa  polisi  na  mwanasheria  mkuu  wa  serikali  wanaunganishwa  kutokana  na  matakwa  ya  kisheria.  Na moja  ya  sababu inatokana  na  nafasi  yao  ya  uajiri wao kwa  mlalamikiwa.

5. ILI  USHINDE  UTATAKIWA  KUTHIBITISHA  MAMBO  MAKUU MAWILI.

Kwanza    uthibitishe  kuwa  uliwekwa  chini  ya  ulinzi/kufungwa  bila  hiari  yako. Pili  uthibitishe  kuwa  kuwekwa  kwako  chini  ya  ulinzi  au  kufungwa  kulifanyika  bila  sababu  za  msingi. Kwa  maana ya  kuwa  hakukuwa  na  sababu yoyote  ya  msingi  ya  kukuweka  chini  ya  ulinzi/kukufunga.

6. ILI  ULIPWE  KIASI  CHA  FIDIA  ULICHOOMBA  UTATHIBITISHA  HAYA.

Katika  shauri  hili  utakuwa ukiomba  kulipwa  fidia. Waweza  kuwa  umeomba  milioni  10,20, 50, 100 n,k. Na  ili  ulipwe utatakiwa  kuonesha  kuwa  uliathirika. Kuathirika  kwaweza  kuwa  kuathirika  kiakili( mental suffering), kuaibishwa, kushushiwa  hadhi, kuumia  kimwili, kupotezewa  muda, kuharibiwa  biashara  au/na shughuli  nyingine,  na  hasara nyingine yoyote  iliyotokana  na  kitendo  hicho.

Ikiwa utathibitisha  haya  utakuwa  umefanikiwa  katika  shauri  la  namna  hii.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment