Tuesday 12 April 2016

NANI KAKWAMBIA DENI HALIFUNGI ?.

Image result for WAFUNGWA

NA  BASHIR  YAKUB  -

Ni  ukweli  usiofichika  kuwa  kisheria  deni  linafunga. Hii  ni  tofauti  na  wengi  wanavyoamini.  Wako  watu  hukopeshwa  hela  na  hukaidi  kulipa  au  kulipa  bila  kuzingatia  makubaliano  kwa  kuamini  kuwa  mdai  wake  hatakuwa  na  la kufanya  kwakuwa  deni  halifungi.

Na  hii  mara  nyingi  huwatokea  wale  ambao  wametoa  mikopo   bila  hata  rehani  yoyote. Mkopo  kwa  rehani  huwa  haumsumbui  mtoa  mkopo  kwakuwa   mrejeshaji  anapokaidi  rehani huchukuliwa.  Lakini  pasipo  na  rehani  huwa  inahitajika  nguvu  za  ziada  kumfanya  mdeni  alipe.

Ni vema kuliweka  sawa  hili  la  deni  kufunga  ili wale waliodhulumiwa  haki  zao  wachukue  hatua  na  wale  wenye  mpango  wa  kudhulumu  kwa  mgongo  wa  deni  halifungi waache au  wadhulumu  lakini  wakijua  kuwa  hatua  dhidi  yao  zaweza  kuchukuliwa.

1.KUFUNGWA.

Moja  ya  tofauti  inayojulikana  sana  kati  ya  kesi  za  jinai  na  mashauri  ya  madai   ni  hii  kuwa  kesi  za  jinai  mtu  atakamatwa  atazuiliwa   na  pengine   baadae  akionekana  ana  hatia  adhabu  yake  itakuwa  kufungwa. Hii  ni  tofauti  na  zile  za  madai ambapo  hamna  kukamatwa  wala  kuzuiliwa na  hukumu  zake  hazihusu  kufunga.

Kwa  ujumla(general rule) kesi  za  madai  hazifungi  isipokuwa  yapo  mazingira ambapo  zinaweza  kufunga. Moja  ya  mazingira  hayo  ni pale ukaidi  wa  kutolipa  deni unapojitokeza.  Tutaona  zaidi  kuhusu  hili.

2.  NINI  UFANYE  KUMFUNGA MDENI.

Kwanza  kabisa  ni  lazima  ufungue  kesi  ya  msingi   ya  kudai  kile unachodai likiwemo deni.  Utadai  kulipwa  kutokana  na  makubaliano  uliyonayo  na  mdeni.  Kesi   itaendelea  mpaka  hukumu  itakapotolewa.
Hukumu  itakapotolewa  ikiwa  umeshinda   basi  mahakama  itaamuru  kulipwa  kwa  deni  lako.

Muda  utatolewa  ili  mdeni  aweze  kulipa  deni. Kama  mda  uliotolewa  utapita  bila kutekeleza  kilichoamuliwa  basi  mdai  ana  haki  ya  kuiomba  mahakama  kwa  maombi  maalum kukamata  mali  yoyote  aliyonayo  mdeni  ikiwa  anayo.  

Kama  hana  mali  yoyote  inayoweza  kukamtwa  na  kuuzwa   ili  kulipa  deni  basi hapo  ndipo  mdai  utaomba  katika  maombi  yako   kuwa  mdeni akamatwe  na  kufungwa  kama   mfungwa  wa  madai.

3.   JE  KUFUNGA  KUNAMALIZA  DENI.

Hapana  kufunga  hakumalizi  deni.  Kufungwa  ni  adhabu  kwa  ukaidi  wa  kutotiii amri  halali  ya  mahakama  iliyotaka  kulipa  deni  kwa  wakati.  Kufungwa  sio  mbadala  wa  deni.  Ni  adhabu  ya  ukaidi. Kutokana  na  hilo  mtu  atafungwa  na  akirudi   ataendelea  kudaiwa  na  atatakiwa  kulipa  deni  lake  kama  kawaida.

4.   MDENI  KUKAMATWA.

Amri  ya  xxi   kanuni  ya  35 ( 1 ) ya  sheria  ya  mwenendo  wa  mashauri  ya  madai inasema  kuwa  mdai  anapokuwa  ameomba  kukamatwa  kwa  mdeni  basi  mahakama  kabla  haijakamata inaweza  kutoa  taarifa  ya  kumwita  mdeni  afike  mahakamani  kueleza  kwanini  asikamatwe  na  kufungwa.

Hii  ina  maana ikiwa  ataitikia wito  huo  basi  atatakiwa  ajibu kwanini  asifungwe. Akijibu kuwa  hataki  kufungwa basi  nafasi  ya  kulipa  muda  huohuo  hutolewa. Na  kama  hawezi  kulipa muda  huo basi atakamatwa  na  taratibu    za  kifungo  cha  madai  zitafuata.

Pia  kanuni  ndogo  ya ( ii)  inaendelea  kusema  kuwa  ikiwa  hatatokea   mahakamani  siku  hiyo  basi  mahakama  moja  kwa  moja itatoa   hati  ya  kukamatwa  kwake ili afungwe.

Pia  ukamataji  wa mdeni  katika  hili  utahusika  na   polisi   na  si  madalali  wa  mahakama( court brockers) kama  ilivyozoeleka katika  mashauri  ya  madai.  Polisi  watahusika  hapa kama  wanavyohusika  katika  shughuli  nyingine  za  kijinai  kwakuwa  itakuwa  ni  amri  ya  mahakama.

Kwahiyo  deni  linafunga na  kesi  ya  madai  inafunga.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment